119. Ni njia zipi zinazokubalika Kishari´ah kumtibu aliyefanyiwa uchawi?

Kuna masuala; kuhusu hukumu ya kuondoa au kuagua uchawi kwa aliyefanyiwa uchawi. Hapana shaka kwamba kusibiwa na uchawi ni maradhi na yanayohitajia dawa. Allaah (Jalla wa ´Alaa) hakuteremsha ugonjwa wowote isipokuwa kateremsha vilevile dawa yake. Aliyefanyiwa uchawi atatibiwa kwa kitu gani? Tutamtibu kwa Ruqyah inayokubalika Shari´ah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitibiwa kwa kufanyiwa Ruyqah. Jibriyl ndiye alimfanyia Ruqyah kwa Suurah “al-Falaq”. Kwa hivo mgonjwa anatibiwa kwa Qur-aan, du´aa na madawa yanayoruhusiwa. Haya hayana ubaya. Kwa sababu huku ni kuagua uchawi kutoka kwa yule aliyerogwa kwa yale yaliyowekwa na Allaah katika Shari´ah. Kwa sababu Allaah hakuteremsha ugonjwa wowote isipokuwa kateremsha vilevile dawa yake.

Ama kuondosha au kuagua uchawi kwa kutumia uchawi mwingine haijuzu. Bali ni kujitibu kwa aliyoharamisha Allaah. Ni kujitibu kwa kufuru. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Jitibuni na wala msijitibu kwa haramu.”[1]

Uchawi nii miongoni mwa mambo ya haramu makubwa. Vipi basi tutamtibu aliyerogwa kwa kutumia uchawi? ´Abdullaah bin Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Hakika Allaah hakufanya kupona kwenu kwa yale aliyowaharamishia.”[2]

Uchawi ni miongoni mwa yale mambo makubwa yaliyoharamishwa. Kwa hivyo haijuzu kumtibu kwao aliyerogwa. Tunatakiwa kumtibu aliyefanyiwa uchawi kama tunavyoyatibu maradhi mengine yote kwa kutumia Ruqyah ya Qur-aan, du´aa, du´aa za kinga zilizowekwa katika Shari´ah na madawa yaliyoruhusiwa. Haya ndio anayotibiwa kwayo aliyefanyiwa uchawi. Kuhusu yanayosemwa ambayo yanaenda kinyume na hayo, nayo ni kujuzisha kutibu uchawi kwa kutumia uchawi mwingine, ni kauli inayorudishwa na kauli batili. Haijuzu kuitendea kazi. Kwa sababu inakwenda kinyume na dalili za Kishari´ah kutoka katika Kitabu cha Allaah na Sunnah za Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Ni wajibu kuzisafisha jamii za Kiislamu kutokamana na wachawi na matendo yao. Wasiachwe huru katika mji wakaharibu baina ya watu na wakaeneza uchawi kati ya watu. Bali ni wajibu kuwapiga vita na kuwasambaratisha. Yule ambaye atajulikana ya kuwa anatumia uchawi, basi apelekwe mahakamani ili apewe adhabu yake ya Kishari´ah ili waja na mji visalimike naye. Haitakiwi kuwapa nafasi, kuwatumia, kuwatetea na kusema kwamba waachwe eti wawatibu watu. Wao wanawatibu watu kwa shari na kwa uchawi. Matokeo yake tunazidisha shari juu ya shari nyingine na uchawi juu ya uchawi mwingine.

[1] Ameipokea Abu Daawuud (3874).

[2] Ameipokea al-Bukhaariy ikiwa na cheni ya wapokezi pungufu (10/81).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 152-153
  • Imechapishwa: 04/02/2019