112. al-´Ayyaashiy upotoshaji wake wa kwanza wa al-Maa-idah

al-´Ayyaashiy amesema:

“´Amr bin Shimr amepokea kutoka kwa Jaabir ambaye amesimulia kuwa Abu Ja´far amesema kuhusiana na Aayah:

الْيَوْمَ يَئِسَ الَّذِينَ كَفَرُوا مِن دِينِكُمْ فَلَا تَخْشَوْهُمْ وَاخْشَوْنِ

“Leo wamekata tamaa wale waliokufuru juu ya dini yenu, hivyo basi msiwaogope na niogopeni Mimi.”[1]

“Wakati al-Qaa´im[2] atapojitokeza Banuu Umayyah watakata tamaa. Wao ndio wamekufuru. Wamekata tamaa juu ya kizazi cha Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”[3]

Tazama uongo huu na upotoshaji wa kipumbavu! Aayah hii iliteremshwa wakati wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pindi Allaah alipoifanya dini Yake na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kushinda na kuwaaibisha maadui wake wanafiki. Kisha mpumbavu huyu anasema:

“Wakati al-Qaa´im atapojitokeza… “

Anazua uongo huu ili apate kuwakufurisha Banuu Umayyah. Wale wanaowakufurisha Maswahabah wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuipotosha Qur-aan kwa kuiongeza na kuipunguza si jambo lenye kushangaza wakaikengeusha Qur-aan ili wawakufurishe Banuu Umayyah. Ni ubaya ulioje wa I´tiqaad hii iliyozuliwa ambayo inapelekea kukengeushwa kwa Qur-aan ambayo haiingiliwi na batili si kwa mbele yake wala kwa nyuma yake. Yule ambaye atajaribu kuingiza batili yoyote katika Qur-aan basi Allaah atamfedhehesha kama alivyowafedhehesha Baatwiniyyah hawa.

[1] 05:03

[2] al-Mahdiy.

[3] Tafsiyr al-´Ayyaashiy (1/292).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intiswaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 160-161
  • Imechapishwa: 23/04/2018