Somo letu liko katika msingi wa pili ambao ni msingi wa uadilifu. Kuhusiana na mwenye kufanya dhambi kubwa ni jambo litakuja moja kwa moja baada yake. Uadilifu kwa mujibu wao ni kupinga Qadar. Mu´tazilah na Jabriyyah wamekosea katika jambo hili. Ni pande mbili zinazogongana.

Mu´tazilah wanaamini kuwa mja amejitosheleza kwa matendo yake na Allaah juu yake hana mipango wala makadirio. Mja mwenyewe ndiye mwenye kujitegemea kwa matendo yake na kwamba mambo hutokea bila kukadiriwa na hayakuandikwa katika Ubao uliohifadhiwa. Wale waliopetuka zaidi katika wao husema kwamba wala Allaah hakuyajua kabla ya kutokea kwake. Kwa msemo mwingine wanapinga ujuzi wa Allaah. Hawa ni makafiri bila shaka. Kwa sababu wakipinga elimu ya Allaah ni makafiri. Lakini wengi wao wanaamini kuwa Allaah alijua lakini hata hivyo hakuyakadiria. Mambo yalivyo ni kwamba alijua kuwa mambo hayo yatatokea lakini bila Yeye kuyakadiria. Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema katika “al-Waasitwiyyah”[1]:

Aina ya kwanza wale ambao wanapinga elimu wamekwishapotea au wenye kusema hivo ni wachache wakati wa Shaykh. Ama wale wengine waliokuja nyuma bado ni wenye kuendelea kusema kuwa Allaah alijua lakini hata hivyo hakukadiria. Mja mwenyewe ndiye aliyezusha bila Allaah kumkadiria. Hawa ndio Qadariyyah. Wameitwa “Qadariyyah” kwa sababu wanapinga Qadar. Wanachupa mpaka katika kuthibitisha matendo ya waja na wanasema kwamba wao wenyewe ndio wenye kuyazusha bila Allaah kuwakadiria.

Kuhusu Jabriyyah ni Jahmiyyah na wale wenye kuchukua ´Aqiydah yao. Wao wanaona kinyume na hivo. Wanachupa mpaka katika kuthibitisha Qadar na matakwa na wanapinga matendo ya waja na wanasema kuwa mja ametenzwa nguvu na hana jambo la kutaka mwenyewe katika matendo yake. Wanaona kuwa mja anaendeshwa kama bendera inavyopepeswa angani. Wamechupa mpaka katika kuthibitisha Qadar na matakwa ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) na wamepinga matendo ya waja na wamewazingatia kuwa ni wenye kulazimishwa juu ya matendo yao na hawana kabisa jambo la wao kutaka wenyewe wala matakwa. Kwa ajili hiyo wakaitwa “Jabriyyah” kwa sababu wanaamini utenzwaji nguvu.

[1]Uk. 36.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh ´Aqiydat-il-Imaam Mujaddid Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab, uk. 29-31
  • Imechapishwa: 04/03/2021