11. Maoni ya maimamu kuhusu ni wapi panaposwaliwa swalah ya ´iyd

Muheshimiwa Shaykh na Muhaddith kwa jina maarufu Ahmad Muhammad Shaakir ana utafiti mzuri na wenye kunufaisha kuhusiana na swalah ya ´Iyd mahali pa uwanja na kuhudhuria kwa wanawake. Napendelea nimnukuu kutokana na faida inayopatikana ndani yake. Amesema (Rahimahu Allaah):

“Je, hii leo Imaam ana haki ya kuwaendea wanawake na kuwapa mawaidha? Maoni ya wanachuoni juu ya suala hili ni mengi. ´Allaamah al-´Ayniy al-Hanafiy amesema baada ya Hadiyth ya Abu Sa´iyd (Radhiya Allaahu ´anh):

“Hadiyth inafahamisha kwamba mtu anatakiwa kwenda mahali pa uwanja na kusiswaliwe msikitini isipokuwa kwa dharurah tu. Ibn Ziyaad amepokea kutoka kwa Maalik ambaye amesema: “Sunnah ni kutoka kwenda katika jangwa isipokuwa kwa watu wa Makkah wanaotakiwa kubaki msikitini.” [1]

Katika “al-Fataawaa al-Hindiyyah” imekuja:

“Kutoka kwenda kwenye jangwa kuswali swalah ya ´Iyd ndio Sunnah hata kama kutakuwa na nafasi ya kutosha katika msikiti mkubwa. Wanachuoni wako katika hili na ndio sahihi.”[2]

Maalik anasema:

“Watu wasiswali swalah za ´Iyd sehemu mbili kama ambavyo vilevile hawatakiwi kuswali katika misikiti yao. Hata hivyo wanatakiwa kutoka kama jinsi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alivyokuwa akitoka. Ibn Wahb ameeleza kutoka kwa Yuunus kutoka kwa Ibn Shihaab ambaye amesema: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akitoka akienda mahali pa uwanja na baada ya hapo watu wengine wote wakaiga hilo.”[3]

Ibn Qudaamah al-Hanbaliy amesema:

“Sunnah ni kuswali swalah ya ´Iyd mahali pa uwanja. ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) aliamrisha hilo wakati al-Awzaa´iy na watu wa maoni wakaonelea kuwa ni jambo zuri. Kadhalika ndio maoni ya Ibn-ul-Mundhir. Kumesimuliwa kutoka kwa ash-Shaafi´iy kwamba anaonelea kuwa bora ni kuswali kwenye msikiti wa mji ikiwa ni mkubwa kwa sababu ndio sehemu bora na safi zaidi, na ndio maana watu wa Makkah wanaswali katika msikiti Mtukufu.

Kuhusu sisi, tunaona kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akitoka na kwenda mahali pa uwanja na anauacha msikiti wake. Vivyo hivyo ndio yaliyofanywa na makhaliyfah baada yake. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) haachi kitu kilicho bora zaidi pamoja na ukaribu wake na badala yake akajikalifisha kufanya kitu kilicho pungufu pamoja na umbali wake. Ni jambo halikuwekwa kwa Ummah wake kuacha kitu kilicho bora. Jengine ni kuwa sisi tumeamrishwa kumfuata Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kumuigiliza. Ni jambo lisilowezekana kilichoamrishwa kikawa kina upungufu na kilichokatazwa kikawa ndio kikamilifu zaidi. Isitoshe haikupokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba aliswali swalah ya ´Iyd msikitini isipokuwa kwa dharurah. Vilevile haya ndio maafikiano ya waislamu; siku zote na kila pahali wanatoka na kwenda mahali pa uwanja na kuswali swalah ya ´Iyd uwanjani hata kama msikiti utakuwa mpana au si mpana. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiswali mahali pa uwanja pamoja na utukufu wa Msikiti wake.”[4]

Ibn Qudaamah “Isitoshe haikupokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba aliswali swalah ya ´Iyd msikitini isipokuwa kwa dharurah… ” anaashiria Hadiyth ya Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh):

“Walipatwa na mvua siku ya ´Iyd ambapo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akawaswalisha msikitini.”[5]

Ameipokea al-Haakim na imesahihishwa na adh-Dhahabiy[6].

Imaam ash-Shaafi´iy amesema:

“Tumefikiwa na khabari ya kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika swalah za ´Iyd alikuwa akitoka na kwenda mahali pa uwanja Madiynah na hali kadhalika yakafanywa na waliokuja baada yake. Kitendo hichi kinafanywa na watu wa miji yote isipokuwa Makkah. Hatukufikiwa na khabari yoyote kuwa kuna yeyote katika Salaf aliswali ´Iyd isipokuwa katika msikiti wao. Ninafikiri – na Allaah ndiye anajua zaidi – ya kuwa hilo ni kutokana na kwamba msikiti Mtukufu ndio sehemu bora kabisa duniani na kwa ajili hiyo ndio maana hawakupenda kuswali sehemu nyingine. Nimesema haya kwa sababu hawakuwa na nafasi kubwa sehemu za kando ya Makkah. Kadhalika sijui kuwa waliwahi kuswali ´Iyd wala swalah ya kuomba mvua pahala kwengine. Ikiwa wakazi wa mji wana msikiti ambapo watu wote wa mji watapata nafasi ndani yake kwa ajili ya sikukuu, basi naonelea kuwa wasiuache. Hata hivyo ikiwa hakutokuwa nafasi ya kuwatosha, basi imechukizwa kwa Imaam kuwaswalisha ndani yake na hivyo swalah isikaririwe. Kukinyesha au kukawepo udhuru mwengine, aswali msikitini na asitoke kwenda jangwani.”[7]

´Allaamah Ibn-ul-Haajj amesema:

“Sunnah endelevu ni swalah za ´Iyd ziswaliwe sehemu ya uwanja. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Swalah moja katika msikiti wangu huu ni bora mara elfu moja kuliko misikiti mingine yote isipokuwa msikiti Mtakatifu. Swalah moja ndani yake ni bora mara laki kuliko misikiti mingine yote.”[8]

Pamoja na fadhila zote hizi (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitoka kwenda uwanjani kuuacha msikiti. Hii ni dalili ya wazi kabisa juu ya kwamba mtu anatakiwa kutoka kwenda mahali pa uwanja kuswali swalah za ´Iyd. Hii ndio Sunnah. Kuziswali misikitini ni Bid´ah kwa mujibu wa madhehebu ya Maalik (Rahimahu Allaah). Hata hivyo sio Bid´ah endapo kutakuwa na dharurah inayopelekea kufanya hivo. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufanya hivo wala hakuna yeyote katika makhaliyfah zake waongofu baada yake aliyefanya hivo. Jengine ni kuwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwaamrisha wanawake, kukiwemo wenye hedhi na wanawali, kutoka kwenda katika swalah za ´Iyd. Umm ´Atwiyyah (Radhiya Allaahu ´anh) alisema wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipowaamrisha wanawake kutoka kwenda kuswali swalah ya ´Iyd:

“Ee Mtume wa Allaah, mmoja wetu hana Jilbaab.” Akasema: “Dada yake ampe moja katika Jilbaab zake ili aweze kushuhudia mema na du´aa ya waislamu.”[9]

Hivyo kukasunishwa swalah katika uwanja wa wazi ili kuonyesha desturi za Kiislamu.”[10]

Sunnah ya kiutume iliyopokelewa katika Hadiyth Swahiyh inathibitisha kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akitoka na kwenda kuswali swalah za ´Iyd kwenye jangwa nje ya mji. Baada ya hapo waislamu wa mwanzo waliendelea kutendea kazi hili na hawakuwa wakiswali swalah za ´Iyd misikitini isipokuwa kukiwepo dharurah ya mvua na mfano wake. Haya ndio madhehebu ya maimamu wanne na maimamu wengine – Allaah awawie radhi.

Sijui yeyote aliyeenda kinyume na hili isipokuwa ash-Shaafi´iy (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye anaonelea kuswali msikitini ikiwa kuna nafasi ya kuwatosha watu wote wa mji. Pamoja na hivyo haonelei kuwa kuna tatizo lolote kuswali jangwani hata kama kutakuwa nafasi ya kuwatosha msikitni. Vilevile ameweka wazi (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba imechukizwa kuswali swalah za ´Iyd msikitini ikiwa kutakuwa hakuna nafasi ya kuwatosha watu wa mji.

Hadiyth zote hizi Swahiyh, kitendo cha kizazi cha mwanzo na maneno ya wanachuoni yanathibitisha kuwa ni Bid´ah kuswali swalah za ´Iyd misikitini. Yanaafikiana hata na maoni ya ash-Shaafi´iy, kwa sababu hakuna msikiti wowote katika miji yetu ambao unaweza kuwatosha watu wa mji wote.”[11]

[1] ´Umdat-ul-Qaariy (6/281-282).

[2] al-Fataawaa al-Hindiyyah (1/118).

[3] al-Mudawwanah al-Kubraa (1/171).

[4] al-Mughniy (2/229-230).

[5] al-Haakim katika “al-Mustadrak” (1/295).

[6] Kusema kuwa Hadiyth hii ni Swahiyh ni jambo linalohitajia kujadiliwa, kwa sababu ni yenye kuzunguka kwa ´Iysaa bin ´Abdil-A´laa bin Abiy Farwah ambaye amesikia kutoka kwa Abu Yahyaa ´Ubaydullaah at-Taymiy ambaye amesimulia kutoka kwa Abu Hurayrah. Vilevile imepokelewa na Abu Daawuud (01/180), Ibn Maajah (01/394) na al-Bayhaqiy (03/210). Cheni ya wapokezi hii ni dhaifu na haijulikani, kama alivyosema Haafidhw katika “at-Taqriyb”. Isitoshe mwalimu wake Abu Yahyaa ´Ubaydullaah bin ´Abdillaah bin Mawhab ana hali isiyojulikana. adh-Dhahabiy amesema:

“´Ubaydullaah ni mdhaifu.” (Mukhtaswar Sunan al-Bayhaqiy” (01/160/01))

Amesema pia juu yake:

“Anakaribia kutojulikana na Hadiyth yake ni munkari.” (Miyzaan-ul-I´tidaal)

Kuafikiana kwake na al-Haakim juu ya kwamba ni Swahiyh katika “Talkhiysw al-Mustadrak”, ni moja katika makosa yake mengi ambayo tunatarajia atasamehewa. Ndio maana Haafidhw amesema kwa kukata kabisa katika “Talkhiysw-ul-Habiyr”, uk. 144, na “Buluugh-ul-Maraam” (02/99) ya kwamba mlolongo wa wapokezi ni dhaifu. Ndio maana maneno ya an-Nawawiy katika “al-Majmuu´” (05/05):

“Mlolongo wa wapokezi wake ni mzuri” (al-Majmuu´ (5/5))

si nzuri. Ni kana kwamba alitegemea kule Abu Daawuud kuinyamazia Hadiyth. Hata hivyo hili si lolote, kwa sababu Abu Daawuud mara nyingi hunyamazia mambo ambayo waziwazi ni dhaifu, jambo ambalo limetajwa katika vitabu vya isitilahi na kadhalika nimeyabainisha katika “Swahiyh Sunan Abiy Daawuud.”

[7] Kitaab-ul-Umm (1/207).

[8] al-Bukhaariy na Muslim.

[9] al-Bukhaariy na Muslim.

[10] al-Madkhal (283).

[11] Taaliki ya ´Allaamah Ahmad Shaakir juu ya “al-Jaamiy´” (2/421-424) ya at-Tirmidhiy.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swalaat-ul-´Iydayn, uk. 29-36
  • Imechapishwa: 13/05/2020