Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Kauli Yake (Ta´ala):

وَمَا تَكُونُ فِي شَأْنٍ وَمَا تَتْلُو مِنْهُ مِن قُرْآنٍ وَلَا تَعْمَلُونَ مِنْ عَمَلٍ إِلَّا كُنَّا عَلَيْكُمْ شُهُودًا إِذْ تُفِيضُونَ فِيهِ

“Hushughuliki katika jambo lolote wala husomi humo chochote katika Qur-aan na wala hamtendi ‘amali yoyote isipokuwa Tunakuwa ni mashahidi juu yenu mnaposhughulika nayo.”[1]

MAELEZO

Hii ni dalili ya ngazi ya pili:

وَمَا تَكُونُ فِي شَأْنٍ

“Hushughuliki katika jambo lolote… “

Hapa anazungumzishwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika jambo lolote unalokuwemo. Ni mamoja katika mambo ya ´ibaadah au mengineyo katika matendo yote, kutikisika kwako na mengineyo.

 وَمَا تَتْلُو مِنْهُ مِن قُرْآنٍ

“… wala husomi humo chochote katika Qur-aan… “

Bi maana kutoka kwa Allaah kwa sababu Qur-aan ni yenye kutoka kwa Allaah (´Azza wa Jall). Vilevile kuna uwezekano dhamira ikawa ni yenye kurudi katika shani. Hivyo itakuwa na maana kwamba katika hali ambayo unakuwa ni mwenye kusoma Qur-aan.

وَلَا تَعْمَلُونَ مِنْ عَمَلٍ

“… wala hamtendi ‘amali yoyote… “

Hapa ni kwa Ummah mzima; kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wengineo. Inahusiana na matendo ya kheri na matendo ya shari.

إِلَّا كُنَّا عَلَيْكُمْ شُهُودً

“… isipokuwa Tunakuwa ni mashahidi… “

Bi maana tunakuona na tunakushuhudieni. Hii ni dalili ya maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… basi Yeye anakuona.”

إِذْ تُفِيضُونَ فِيهِ

“… mnaposhughulika nayo.”

Mnapoibashiri na kuifanya. Hapa kuna dalili juu ya ngazi ya pili katika ngazi za Ihsaan na kwamba Yeye (Jalla wa ´Alaa) anamuona kila mtendaji kwa kitendo chake. Anamuona (Subhaanahu wa Ta´ala) na anamjua. Hafichiki Kwake:

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَخْفَىٰ عَلَيْهِ شَيْءٌ فِي الْأَرْضِ وَلَا فِي السَّمَاءِ

“Hakika Allaah hakifichiki Kwake chochote katika ardhi wala katika mbingu.”[2]

[1] 10:61

[2] 03:05

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 226-227
  • Imechapishwa: 27/01/2021