1- al-Ahnaf bin Qays ameeleza ya kwamba ´Umar bin al-Khattwaab amesema:

“Ahnaf! Anayezungumza sana hutumbukia katika makosa mengi. Anayetumbukia katika makosa mengi hupotea haya yake. Anayepoteza haya yake hupoteza uchaji wake. Anayepoteza uchaji wake moyo wake umekufa.”

2- ´Aliy bin Bakkaar amesema:

“Allaah amefanya kila kitu kina milango miwili mbali na ulimi ambao una milango mine. Midomo ni yenye kutazamana na meno ni yenye kutazamana.”

3- Ni wajibu kwa mwenye busara kuwa mwadilifu juu ya masikio yake kuhusiana na kinywa chake na atambue kuwa amepewa masikio mawili na mdomo mmoja ili asikilize zaidi na kuzungumza kidogo. Kuna khatari akisema kitu akajuta. Hata hivyo hatojuta endapo atanyamaza. Ni rahisi kurudisha kitu ambacho mtu alikinyamazia kuliko kitu alichokizungumzia. Pindi mtu anapotamka neno, neno linammiliki. Asipotamka neno, neno halimmiliki. Ajabu ni mtu anaweza kutamka kitu kinachoweza kuwa na madhara. Ni kwa nini mtu asinyamaze? Kuna khatari neno likafanya neema kuondoka.

4- Abuud-Dardaa´ amesema:

“Inatosha kwako kuwa dhalimu kwa kugombana siku zote. Inatosha kwako kuwa mtenda dhambi kwa kujadiliana siku zote. Inatosha kwako kuwa muongo kwa kuzungumza siku zote. Isipokuwa tu maneno kwa ajili ya Allaah (Tabaarak wa Ta´ala).”

5- Ka´b-ul-Ahbaar amesema:

“Usalama una sehemu kumi. Tisa katika hizo zinapatikana katika kunyamaza.”

6- al-Awzaa´iy amesema:

“Hakuna aliyewekwa katika balaa kubwa katika dini yake kama mtu mwenye kuzungumza pasina mipaka.”

7- Khaalid bin al-Haarith amesema:

“Kunyamaza ni pambo la mwanachuoni na baya kwa mjinga.”

8- Lau sifa nzuri katika kunyamaza ingelikuwa kunampamba mwanachuoni tu na kumfanya mbaya mjinga basi ingelitosha kuwa wajibu kwa mtu kunyamaza kadri na anavyoweza. Anayetaka kusalimika na madhambi basi aseme kile kinachokubalika kwake na aseme kidogo katika kile kinachokubalika kwake. Hakuna anayethubutu kusema sana isipokuwa mtu hodari au mpumbavu.

9- Wanachuoni wengi wameacha kupokea kutoka kwa watu wenye kuzungumza sana. Sa´iyd amesema:

“Nilimuuliza al-Hakam ni kwa nini haandiki kutoka kwa Zaadhaan. Akajibu: “Alikuwa akiongea sana.”

10- Ulimi wa mwenye busara unakuwa nyuma ya moyo wake. Anapotaka kuongea anarejea kwenye moyo wake. Yakiwa na manufaa na yeye, anazungumza. Vinginevyo anayaacha. Moyo wa mjinga unakuwa kwenye ncha ya ulimi wake. Yale yanayomjia kwenye ulimi ndio huzungumza. Yule asiyeuangalia ulimi wake haielewi dini yake.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 44-47
  • Imechapishwa: 12/11/2016