10. Hadiyth “Mfano wa kile ambacho amenitumiliza kwacho Allaah katika uongofu na elimu… “

76- Abu Muusa (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mfano wa kile ambacho amenitumiliza kwacho Allaah katika uongofu na elimu ni kama mfano wa mvua iliyotua juu ya ardhi. Ikapatikana katika ardhi hiyo kipande kizuri; kikayakubali na kuyapokea yale maji na kuotesha majani na nyasi nyingi. Kukapatikana kipande kingine kikavu; kiliyazuia maji na Allaah akawanufaisha watu kwayo. Wakanywa kutoka katika maji hayo, wakanywesheleza na wakalima. Kipande kingine ikawa ni changaforo; ikawa haizuii maji na wala haitoshi majani. Huyo ni mfano wa yule aliyeifahamu dini ya Allaah (Ta´ala) na  Allaah akamnufaisha kwa yale niliyotumilizwa nayo; amejifunza na yeye akafunza. Na mfano wa yule ambaye hakunyanyua kwa hiyo elimu kichwa chake na wala hakukubali uongofu wa Allaah ambao mimi nimetumilizwa nao[1].”[2]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

[1] Imaam al-Qurtwubiy na wengineo walioisherehesha Hadiyth:

“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amelinganisha mfano wa yale aliyokuja nayo katika dini ni kama mvua iliyoenea ambayo imenyesha pindi watu wanapoihitajia. Hivo ndivo ilivyokuwa hali ya watu kabla ya kutumilizwa kwake. Kama ambavyo mvua inahuisha ardhi iliokufa, basi vivyo hivyo elimu ya dini inazihuisha nyoyo zilizokufa. Halafu akawafananisha wasikilizaji na ardhi zilizotofautiana zinazoteremkiwa na mvua hiyo. Katika wao wako ambao wametenda na wakafunza. Hao ni kama ardhi yenye rutuba. Imeyameza maji na ikanufaika yenyewe kwanza na  ikaota mimea ambapo wengine pia wakanufaika nayo. Kundi lingine wametumia muda wao wote kukusanya elimu pasi na kufanyia kazi yale mapendekezo yake au hawakunufaika na yale waliyokusanya. Lakini hata hivyo wamewafikishia wengine. Hao ni kama mfano wa ardhi yenye chumvi au ardhi kavu ambayo haiyakubali maji au kuwaharibia wengine. Ameyataja makundi haya mawili ya kwanza yenye kusifiwa pamoja kwa sababu ni yenye kushirikiana katika kunufaisha. Kundi la tatu na lenye kusemwa vibaya amelitaja kivyake kwa sababu halina manufaa yoyote – na Allaah ndiye mjuzi zaidi.”

[2] Swahiyh.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Adhwiym bin ´Abdil-Qawiy al-Mundhiriy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (1/141-142)
  • Imechapishwa: 24/09/2018
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy