Swalah na salaam zimwendee Mtume wetu Muhammad, ahli zake na Maswahabah zake wote.

Amma ba´d:

Himdi ni Zake Allaah kutokana na majina mazuri na sifa kamilifu na neema Zake nyingi alizonazo. Swalah na salaam zimwendee Muhammad aliyetumwa kuja kutengeneza dini na dunia na Aakhirah.

Amma ba´d:

Huu ni ujumla mfupi ulio na mambo muhimu kabisa katika mambo ya dini na misingi ya imani. Ni mambo ambayo haja na dharurah inapelekea kuyatambua. Nimefanya kwa mtindo wa swali na jibu kwa kuwa ni jambo liko karibu na kufahamu na kufahamisha. Vilevile ni jambo liko wazi kujifunza na kufunza.

Swali 1: Ni ipi tafsiri ya Tawhiyd? Vigawanyo vyake ni vingapi?

Jibu: Tafsiri ya Tawhiyd ya jumla iliokusanya aina zake zote ni:

Elimu ya mja, itikadi, kukiri na kuamini kwake kupwekeka kwa Allaah kwa kila sifa ya ukamilifu. Vilevile kuamini ya kwamba hakuna mshirika wala kitu kilicho na sehemu katika ukamilifu Wake. Hali kadhalika ina maana ya kwamba mtu aamini kuwa Yeye ndiye ana haki ya kuabudiwa na viumbe pasina kujali inahusiana na ´ibaadah aina gani.

Katika tafsiri hii kunaingia vigawanyo vitatu vya Tawhiyd:

1- Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah: Kukiri ya kwamba Mola amepwekeka katika kuumba, kuruzuku, kuyaendesha mambo na kulea.

2- Tawhiyd Asmaa´ was-Swifaat: Kuthibitisha yale yote ambayo Allaah amejithibitishia katika nafsi Yake Mwenyewe na ambayo amemthibitishia Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) miongoni mwa majina mazuri na sifa kuu. Uthibitishaji huu unatakiwa kuwa pasi na kushabihisha na kufananisha na sifa za viumbe, pasi na kupotosha na kukanusha.

3- Tawhiyd-ul-´Ibaadah: Ni mtu kumpwekesha na kumtakasia Allaah aina zote za ´ibaadah bila ya kumshirikisha katika chochote katika hayo.

Hivi ndivyo vigawanyo vya Tawhiyd. Mtu hawezi kuwa mpwekeshaji mpaka avitekeleze vyote.

  • Mhusika: Imaam ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahamm-ul-Muhimmaat, uk. 17-18
  • Imechapishwa: 25/03/2017