5- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Ukubwa wa malipo ni pamoja na ukubwa wa mitihani. Hakika Allaah (Ta´ala) anapowapenda watu basi huwapa huwajaribu. Yule mwenye kuridhia basi hupata radhi Zake na yule mwenye kuchukia basi hupata hasira Zake.”[1]

Hii ni Hadiyth nyingine. Mtunzi wa kitabu (Rahimahu Allaah) amezitaja zote kwa pamoja kwa sababu msimulizi na mapokezi wake ni mmoja, naye ni Anas na mwengine ni at-Tirmidhiy. Kwa ajili hiyo ndio maana amezitaja kwa mtiririko mmoja.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ukubwa wa malipo ni pamoja na ukubwa wa mitihani.”

Bi maana mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Yule mwenye kupewa mtihani akisubiri na akaridhia makadirio na mipango ya Allaah basi Allaah anamlipa thawabu duniani na Aakhirah. Amesema (Ta´ala):

وَمَن يُؤْمِن بِاللَّـهِ يَهْدِ قَلْبَهُ ۚ وَاللَّـهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ

“Yeyote   anayemuamini Allaah, basi huuongoza moyo wake. – Allaah kwa kila kitu ni mjuzi.”

Hapa mtu analipwa kwa sababu ya kuvuta subira na kutarajia malipo kutoka kwa Allaah. Makusudio ya misiba katika Hadiyth ni majaribio na mitihani. Mtu anaweza kupewa mtihani kwa matatizo, maradhi, kufilisika na kufisha ndugu. Miongoni mwa watu wako ambao wanapewa misiba mingi na yenye kufuatana. Hii ni alama nzuri midhali yule mwenye kupewa misiba ni muumini na mwenye kusubiria.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hakika Allaah (Ta´ala) anapowapenda watu basi huwapa huwajaribu.”

Hii ni hekima nyingine. Waislamu wenye kupatwa na majaribio na mitihani ni dalili inayoonyesha mapenzi ya Allaah juu yao. Pindi Allaah anapowapenda basi anawapa majaribio kwa ajili ya kuyapunguza madhambi yao ili waende huko Aakhirah wakiwa hawana madhambi. Kinachopata kufahamika ni kwamba asipowapenda watu basi huwazuilia mitihani ili waende huko Aakhirah wakiwa na madhambi yao na hivyo awaadhibu kwayo.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yule mwenye kuridhia basi hupata radhi Zake… “

Yule mwenye kuridhia makadirio na mipango ya Allaah basi hupata radhi za Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kama malipo.

“… yule mwenye kuchukia basi hupata hasira Zake.”

Yule mwenye kuchukia makadirio na mipango ya Allaah basi hupata hasira za Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kama malipo. Hii ni dalili inayoonyesha kwamba mtu analipwa alivyotenda. Yule mwenye kuridhia Qadar ya Allaah na akavumilia mitihani basi hupata radhi na mapenzi ya Allaah. Asiyefanya hivo Allaah humchukia. Lengo na misiba hii ni majaribio na mtihani ili kudhihiri ni nani mwenye mvumilivu na ni nani asiyekuwa mvumilivu. Kisha baada ya hapo Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amlipe kila mmoja kwa uadilifu.

[1] at-Tirmidhiy (2396) na Ibn Maajah (4031). Nzuri kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaami´” (2110).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: I´aanat-ul-Mustafiyd bi Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 436-437
  • Imechapishwa: 15/08/2019