09. Mfano wa nne kuonyesha jinsi Raafidhwah wanavodai kuwa Maswahabah wamepotosha Qur-aan

al-Qumiy (02/295) amesema alipotaja sanadi yake mpaka kwa mtu asiyejulikana:

“Abu Baaswiyr ameeleza kwamba alimsomea Abu ´Abdillaah:

هَـٰذَا كِتَابُنَا يَنطِقُ عَلَيْكُم بِالْحَقِّ

“Hiki Kitabu Chetu kinatamka [kushuhudia] juu yenu kwa haki.”[1]

Hivo akasema: “Kitabu hakitamki na wala hakitotamka. Ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndiye mwenye kutamka kwa Kitabu. Allaah (Ta´ala) Alisema:

هذا بكتابنا ينطق عليكم بالحق

Huyu hapa kwa Kitabu Chetu anatamka [anashuhudia] juu yenu kwa haki.”

Akasema: “Mimi siisomi hivo.” Akasema: “Ninaapa kwa Allaah ya kwamba hivo ndivyo jinsi Jibriyl alivoiteremsha kwa Muhammad, lakini ni moja katika upotoshaji katika Kitabu cha Allaah.””

Allaah Amemtakasa Abu ´Abdillaah na uongo huu na upotoshaji.

Hii ni moja miongoni mwa Aayah ambapo Allaah Anaeleza yatayowapitikia makafiri siku ya Qiyaamah wanapothibitisha matendo yao na kukemewa na kukutana na fadhaa zote hizo. Kitabu kinachotamka hapa ni kitabu cha matendo kisichoacha [tendo] kubwa wala dogo. Makusudio sio Qur-aan, enyi wapotoshaji waongo! Allaah (Ta´ala) Amesema:

وَلِلَّـهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۚ وَيَوْمَ تَقُومُ السَّاعَةُ يَوْمَئِذٍ يَخْسَرُ الْمُبْطِلُونَ وَتَرَىٰ كُلَّ أُمَّةٍ جَاثِيَةً ۚ كُلُّ أُمَّةٍ تُدْعَىٰ إِلَىٰ كِتَابِهَا الْيَوْمَ تُجْزَوْنَ مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ

“Na ni wa Allaah Pekee ufalme wa mbingu na ardhi. Na Siku itakayosimama Saa [Qiyaamah], watakhasirika Siku hiyo wabatilifu. Na utaona kila ummah umepiga magoti [kwa kunyenyekea]. Kila ummah utaitwa kwenye Kitabu chake: “Leo mtalipwa yale mliyokuwa mkiyatenda.”[3]

Siku ya Qiyaamah kila Ummah utaitwa kwenye Kitabu Chake cha matendo ambayo Malaika waliandika. Akakazia hilo kwa kusema:

هَـٰذَا كِتَابُنَا يَنطِقُ عَلَيْكُم بِالْحَقِّ

“Hiki Kitabu Chetu kinatamka [kushuhudia] juu yenu kwa haki.”

Bi maana chenye kuleta matendo yenu yote pasina kuongeza wala kuzidisha. Allaah (Ta´ala) Amesema:

وَوُضِعَ الْكِتَابُ فَتَرَى الْمُجْرِمِينَ مُشْفِقِينَ مِمَّا فِيهِ وَيَقُولُونَ يَا وَيْلَتَنَا مَالِ هَـٰذَا الْكِتَابِ لَا يُغَادِرُ صَغِيرَةً وَلَا كَبِيرَةً إِلَّا أَحْصَاهَا ۚ وَوَجَدُوا مَا عَمِلُوا حَاضِرًا ۗ وَلَا يَظْلِمُ رَبُّكَ أَحَدًا

“Na kitawekwa Kitabu [daftari la rekodi ya vitendo vyote], basi utaona wahalifu ni wenye khofu kwa yale yaliyokuwemo ndani yake na watasema: “Ole wetu! [Tumeangamia]. Kitabu hiki kina nini, hakiachi dogo wala kikubwa isipokuwa kimekidhibiti?” Na watakuta yale [yote] waliyoyatenda yamehudhuria. Na Mola wako Hamdhulumu yeyote.”[3]

Maana ya Kauli ya Allaah:

إِنَّا كُنَّا نَسْتَنسِخُ مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ

“… hakika Sisi Tulikuwa Tunaandika yale [yote] mliyokuwa mkiyatenda.”[4]

ni kwamba tulikuwa tukiamrishwa na Allaah kuandika matendo yenu yatayoshuhudia juu yenu. Tazama Tafsiyr ya Ibn Kathiyr[5].

Tazama jinsi huyu Baatwiniy anavojaribu kubatilisha maana ya Aayah hizi ambazo zinaelezea khasara na aibu itakayowapata makafiri siku ya Qiyaamah ili kuzipitisha katika ´Aqiydah yao.

[1] 45:29

[2] 45:27-29

[3] 18:49

[4] 45:29

[5] 12/366.

 

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intiswaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 39-40
  • Imechapishwa: 19/03/2017