09. Kuwaendea makuhani, waganga na wachawi

Kuna mambo yanayofanywa na watu ambayo yanaitia kasoro ´Aqiydah. Kwa mfano kuwaendea wachawi na makuhani kwa ajili ya kutibiwa kwao na kutafuta dawa kwao. Mtu kasibiwa na maradhi na anataka kutibu haya maradhi. Hakuna ubaya kujitibisha. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Enyi waja wa Allaah! Jitibisheni na wala msijitibishe kwa kitu cha haramu.”[1]

Akijitibu kwa mambo yanayoruhusu hakuna lawama juu yake. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Allaah hakuteremsha maradhi yoyote isipokuwa kateremsha pia dawa yake. Kajua yule aliyeuijua na hakuijua yule ambaye hakuijua.”

Hakuna lawama juu yake ikiwa atajitibu kwa dawa ambayo kateremsha Allaah (Subhaanah) katika dawa zinazoruhusiwana, matabano ya Kishari´ah na du´aa mbalimbali. Hakuna juu yake lawama kwa hilo. Hizi ni sababu katika sababu zinazoruhusiwa. Ama lau atataka kujitibu kwa kitu cha haramu, hili halijuzu. Kwa mfano akajitibu kwa kumchinjia asiyekuwa Allaah kwa makuhani na wachawi, akajitibu kwa hirizi na mambo mengine ya Kishaytwaan kwa ajili ya ponyo. Huyu kajitibu kwa haramu iliyo kubwa ambayo nayo ni shirki. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yeyote atakayemwendea kuhani au mpiga ramli na akamsadikisha kwa ayasemayo, basi ameyakufuru yale aliyoteremshiwa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”[2]

Wameipokea waandishi wa “as-Sunan”.

Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake:

“Yeyote atakayemwendea kuhani hazitokubaliwa swalah zake kwa siku arubaini.”[3]

Haijuzu kuwaendea makuhani kwa ajili ya kujitibu, kwa ajili ya kuwauliza mambo yaliyofichikana, kuuliza mambo ya mustakabali kwa mfano kutakuwa nin? Lini ataoa? Lini atasafiri? Lini lini? Huku ni kumshirikisha Allaah (´Azza wa Jall). Kwa kuwa ameenda kwa wale wanaodai kujua elimu iliyojificha kuwauliza mustakabali wake na kuhusu mambo yake. Huyu hakumtegemea Allaah na hakuamini kuwa hakuna ajuaye ghaibu isipokuwa Allaah pekee (Subhaanahu wa Ta´ala).

[1] Abu Daawuud (3874), at-Twabaraaniy (649) na al-Bayhaqiy (19465). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaamiy´” (2643).

[2] Abu Daawuud (3904), Ibn Maajah (639) na ad-Daarimiy (1136). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”as-Silsilah as-Swahiyhah” (3387).

[3] Muslim (2230).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah al-Islaamiyyah as-Swahiyhah https://www.youtube.com/watch?v=KqoTCYds6Cs&t=13s
  • Imechapishwa: 07/02/2019