Haafidhw Ibn Hajar al-´Asqalaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

688- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kusahau ilihali amefunga ambapo akala au akanywa, basi aikamilishe funga yake. Hakika si vyenginevyo Allaah ndiye kamlisha na kumnywesha.”[1]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

689- Katika upokezi wa al-Haakim imekuja:

“Mwenye kufungua katika Ramadhaan kwa kusahau basi hakuna juu yake kulipa wala kafara.”[2]

Nayo ni Swahiyh.

MAELEZO

Mfungaji akila au akinywa kwa kusahau hakuna kinachomlazimu, kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kusahau ilihali amefunga ambapo akala au akanywa, basi aikamilishe funga yake. Hakika si vyenginevyo Allaah ndiye kamlisha na kumnywesha.”

Lakini lazima kwake ajizuie pale tu atapokumbuka hata kama yuko na tonge au glasi ya maji kinywani mwake; ni lazima kwake kuyatema. Kwa sababu udhuru umeondoka.

Kadhalika endapo atakula au atakunywa kwa kudhani kuwa jua limekwishazama na baadaye ikaja kubainika kuwa bado halijazama; swawm yake ni sahihi. Asmaa´ bint Abiy Bakr (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Siku moja ya mawingu wakati wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tulifuturu. Kisha baadaye jua likachomoza.”

Lau ingelikuwa ni lazima kulipa basi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) angelibainisha jambo hilo. Isitoshe ni jambo linaloingia katika ujumla wa maneno Yake (Ta´ala):

وَلَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ فِيمَا أَخْطَأْتُم بِهِ وَلَـٰكِن مَّا تَعَمَّدَتْ قُلُوبُكُمْ

”Hapana dhambi juu yenu katika yale mliyoyakosea, lakini isipokuwa katika yale yaliyoyakusudia nyoyo zenu.”[3]

na:

رَبَّنَا لَا تُؤَاخِذْنَا إِن نَّسِينَا أَوْ أَخْطَأْنَا

“Ee Mola wetu! Usituchukulie tukisahau au tukikosea.”[4]

Allaah (Ta´ala) akasema:

“Nimekwishafanya.”[5]

[1] al-Bukhaariy (1933) na Muslim (1155).

[2] al-Haakim (1/430).

[3] 33:5

[4] 2:286

[5] Muslim (126).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ash-Sharh al-Mukhtaswar ´alaa Buluugh-il-Maraam (2/414-418)
  • Imechapishwa: 24/04/2020