08. Watu wa kwanza kuingia Motoni siku ya Qiyaamah

Mtu wa kwanza atakayeingia Motoni siku ya Qiyaamah ni watu aina tatu:

1- Mtu ambaye Allaah kampa elimu ambapo akaifunza. Lakini hata hivyo ameifunza kwa kujionyesha. Hakuifunza kwa ajili ya Allaah. Huyu ataletwa siku ya Qiyaamah na aambiwe na Allaah: “Ulifanya nini?” Atasema: “Ee Mola Wangu! Nilijifunza elimu kwa ajili yako na nikaifunza.” Allaah atamwambia: “Umesema uongo. Ulijifunza elimu na ukaifunza ili uambiwe ni ´mwanachuoni` na kumeshasemwa.” Kisha Allaah ataamrisha akamatwe na kutupwa Motoni.

2- Mtu wa pili ni yule ambaye Allaah kampa mali nyingi mabapo anaitoa swadaqah na hapitwi na mambo ya kheri isipokuwa anatoa pesa zake. Lakini hata hivyo anakusudia kusifiwa na wala hakusudii thawabu za Allaah. Huyu ataletwa siku ya Qiyaamah na kuambiwa: “Uliifanyia nini mali yako?” Atasema: “Ee Mola Wangu! Sikuacha mlango wowote Uliotaka watu wajitolee isipokuwa nilijitolea.” Allaah atamwambia: “Umesema uongo. Ulitoa ili uambiwe wewe ni ´mkarimu sana` na kumeshasemwa.” Kisha ataamrisha akamatwe na kutupwa Motoni.

3- Mtu wa tatu ni yule aliyepambana Jihaad katika njia ya Allaah, kawapiga vita makafiri kwelikweli. Lakini hata hivyo hakusudii Uso wa Allaah ila anachokusudia aambiwe kuwa ni ´shujaa na jasiri`. Ataletwa siku ya Qiyaamah. Allaah amuulize: “Ulifanya nini?” Atasema: “Ee Mola Wangu” Nilipigana vita kwa ajili Yako mpaka nikauawa shahidi.” Allaah atamwambia: “Umesema uongo.” Ulipigana ili uambiwe kuwa wewe ni ´shujaa` na kumeshasemwa. Kisha ataamrisha akamatwe na atupwe Motoni.

Enyi waja wa Allaah! Huku ndio kujionyesha. Tutahadhari jambo la kujionyesha lisiingie ndani ya matendo yetu.

Lakini mtu ni mtu. Wakati fulani anaweza kujiwa na shaytwaan na akamtia wasiwasi wa kupenda sifa na matapo. Natija yake akafanya ´ibaadah kwa kuonekana na hivyo watu wakaanza kumsifu. Lakini asili yeye alikuwa hakusudii kujionyesha. Asili mwanzoni mwa tendo alikuwa hakusudii kujionyesha. Shaytwaan amemjia katikati ya kitendo na akamghuri kupenda sifa na matapo na matokeo yake akaingiwa ndani ya moyo wake na kitu katika mambo hayo. Huyu akitubu kwa Allaah papohapo na akaomba kinga kwa Allaah dhidi ya shaytwaan na akaacha kujionyesha na akaendelea kumtakasia nia Allaah kwa matendo hatodhurika. Lakini akiendelea kujionyesha, basi kitendo chake kinabatilika. Kwa sababu kujionyesha kubaporomosha matendo. Kwani  mtu  huyo hakukusudia kwa matendo yake Uso mtukufu wa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Allaah anakubali tu kile kinachofanywa kwa ajili ya kukusudia Uso Wake mtukufu, hali ya kuwa yupee hana mshirika. Haya ni miongoni mwa mambo yanayoitia kasoro ´Aqiydah. Huenda yakawa ni yenye kufichikana kwa baadhi ya watu.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah al-Islaamiyyah as-Swahiyhah https://www.youtube.com/watch?v=KqoTCYds6Cs&t=13s
  • Imechapishwa: 31/01/2019