08. Tofauti kati ya ukafiri kwa fomu ya kihakika na isiyokuwa ya kihakika

Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema kuhusiana na maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mambo mawili kwa watu ni kufuru; kutukaniana nasabu na kuomboleza juu ya maiti.”

“Ina maana kwamba sifa mbili hizi zinapatikana kwa watu. Sifa zote mbili hizo ni kufuru kwa sababu ni katika matendo ya makafiri. Zinapatikana kwa watu. Lakini haina maana kwamba yule anayetumbukia katika aina moja wapo ya kufuru ni kafiri kabisa mpaka kukite kwake ukafiri wa kihakika. Kama ambavyo vilevile haina maana kwamba anayesifika kwa aina moja wapo ya imani anakuwa ni muumini wa kihakika mpaka kukite kwake asli na imani ya kihakika. Kuna tofauti kati ya kufuru yenye kutajwa kwa njia ya kihakika kama mfano:

“Baina ya mtu na shirki na kufuru ni kuacha swalah.”

na kufuru yenye kutajwa kwa njia isiyokuwa ya kihakika.”[1]

Itapobainika kwamba yule mwenye kuacha swalah pasi na udhuru ni kafiri ukafiri wenye kumtoa katika Uislamu kwa mujibu wa dalili hizi, itabaini kuwa maoni ya Imaam Ahmad bin Hanbal ndio ya sawa. Vilevile ndio moja ya maoni ya ash-Shaafi´iy. Imetajwa na Ibn Kathiyr pindi alipokuwa akifasiri maneno ya Allaah (Ta´ala):

فَخَلَفَ مِن بَعْدِهِمْ خَلْفٌ أَضَاعُوا الصَّلَاةَ وَاتَّبَعُوا الشَّهَوَاتِ ۖ فَسَوْفَ يَلْقَوْنَ غَيًّا

“Baada yao wakaja watu waovu. Walipoteza swalah na wakafuata matamanio; basi watakutana na adhabu kali.”[2]

Vilevile Ibn-ul-Qayyim ametaja katika “Kitaab-us-Swalaah” ya kwamba ni moja katika maoni mawili ya Shaafi´iyyah na at-Twahaawiy ameinukuu kutoka kwa ash-Shaafi´iy mwenyewe.

[1] Iqtidhwaa’-us-Swiraat al-Mustaqiym, uk. 70.

[2] 19:59

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Hukm Taarik-is-Swalaah, uk. 11-12
  • Imechapishwa: 22/10/2016