08. Tafsiri inapatikana katika kisomo

22- Abul-Qaasim amesema: Muhammad bin Rizqillaah ametuhadithia: ´Uthmaan bin Ahmad ametuhadithia: ´Iysaa bin Muusa ametuhadithia: Nimemsikia baba yangu akisema: Nimemsikia Sufyaan bin ´Uyaynah akisema:

“Yale yote Aliyojisifu kwayo Allaah (Ta´ala) katika Qur-aan tafsiri yake inapatikana kwa kule kuyasoma bila kuyafanyia namna wala  kuyapigia mfano.”

23- Ahmad bin Naswr alisema kumwambia Sufyaan bin ´Uyaynah:

“Ni lazima nikuulize. Nisipokuuliza wewe, ni nani nitamuuliza?” Akasema: “Sawa uliza.” Nikasema: “Vipi kuhusu Hadiyth kutoka kwa ´Ubaydah, kutoka kwa ´Abdullaah, kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hakika Allaah (´Azza wa Jall) atazibeba mbingu kwenye kidole, ardhi kwenye kidole… “

“Nyoyo za wanaadamu ziko kati ya vidole viwili katika vidole vya Mwingi wa huruma (´Azza wa Jall)… “

“Allaah (´Azza wa Jall) anashangaa na anacheka.”?

Sufyaan akasema: “Ziko kama zilivyopokelewa. Tunazithibitisha na kuzihadithia pasi na kuzifanyia namna.”

24- Abu Bakr al-Khallaal amesema: Ahmad bin Muhammad bin Waasil al-Muqri’ amenikhabarisha: al-Haytham bin al-Khaarijah ametuhadithia: al-Waliyd bin Muslim ametuhadithia:

“Nilimuuliza Maalik bin Anas, Sufyaan ath-Thawriy, al-Layth bin Sa´d na al-Awzaa´iy kuhusu khabari zinazohusiana na sifa. Wakasema: “Zipitishe kama zilivyokuja.”

25- Yahyaa bin ´Ammaar amesema:

“Hawa ndio maimamu wa miji. Maalik alikuwa imamu wa Hijaaz, ath-Thawriy alikuwa imamu  wa ´Iraaq, al-Awzaa´iy alikuwa imamu wa Shaam na al-Layth alikuwa imamu wa Misri na Afrika magharibi.”

26- Abu ´Ubayd amesema:

“Hadiyth hizi ni Swahiyh. Wapokezi waaminifu wamezinukuu baadhi kutoka kwa wengine mpaka zimetufikia. Pasi na shaka tunaonelea kuwa ni za kweli. Lakini tukiulizwa vipi anaweka unyayo Wake na ni vipi anacheka, tunasema hatuzifasiri na hatukumuona yeyote akizifasiri.”

26- al-´Abbaas bin Muhammad ad-Duuriy amesema: Nimemsikia Yahyaa bin Ma´iyn akisema: Nimeshuhudia Zakariyyaa bin ´Adiy akimuuliza Wakiy´:

“Ee Abu Sufyaan! Unasemaje kuhusu Hadiyth hizi, kama mfano wa Kursiy ni mahala pa miguu miwili na nyenginezo?” Wakiy´ akasema: “Tulikutana na Ismaa´iyl bin Abiy Khaalid, Sufyaan na Mis´aar wakihadithia Hadiyth hizi na wala hawafasiri kitu.”

  • Mhusika: Imaam Muwaffaq-ud-Diyn bin Qudaamah al-Maqdisiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Dhamm-ut-Ta’wiyl, uk. 17-19
  • Imechapishwa: 02/06/2018