8 – Nguvu za makafiri juu ya waislamu

Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walilihoji tatizo hili katika kipindi cha uhai wake. Ndipo Allaah (Jalla wa ´Alaa) akatoa jibu la kimbingu kwa maswali yote. Pindi waislamu walipofikwa na yakufikwa katika siku ya Uhud, wakahoji tatizo hili. Wakasema:

“Ni vipi washirikina watatushinda na kututawala ilihali sisi ndio tuko katika haki na wao wako katika batili?”

Allaah akawajibu na kusema:

أَوَلَمَّا أَصَابَتْكُم مُّصِيبَةٌ قَدْ أَصَبْتُم مِّثْلَيْهَا قُلْتُمْ أَنَّىٰ هَـٰذَا ۖ قُلْ هُوَ مِنْ عِندِ أَنفُسِكُمْ

“Nyinyi – ulipokusibuni msiba ambao nyinyi mmekwisha watia mara mbili mfano wa huo – mnasema: “Umetoka wapi huu?” Sema: “Huo ni kutoka kwenu wenyewe.””[1]

وَلَقَدْ صَدَقَكُمُ اللَّـهُ وَعْدَهُ إِذْ تَحُسُّونَهُم بِإِذْنِهِ ۖ حَتَّىٰ إِذَا فَشِلْتُمْ وَتَنَازَعْتُمْ فِي الْأَمْرِ وَعَصَيْتُم مِّن بَعْدِ مَا أَرَاكُم مَّا تُحِبُّونَ ۚ مِنكُم مَّن يُرِيدُ الدُّنْيَا وَمِنكُم مَّن يُرِيدُ الْآخِرَةَ ۚ ثُمَّ صَرَفَكُمْ عَنْهُمْ لِيَبْتَلِيَكُمْ

“Hakika Allaah amekwishakusadikishieni ahadi Yake mlipowaua vikali kwa idhini Yake mpaka mliposhindwa na mkazozana katika amri na mkaasi baada ya Yeye kukuonyesheni yale mnayoyapenda. Miongoni mwenu wako wenye kutaka dunia na miongoni mwenu wako wenye kutaka Aakhirah. Kisha akakugeuzeni nyuma mbali nao [hao maadui] ili Akujaribuni.”[2]

Katika jibu hili la kiungu akabainisha kuwa makafiri kushinda ni kwa sababu ya waislamu wenyewe. Yote hayo yamepitika baada ya wao kuwa na tofauti na kuasi amri ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuyapupia mambo ya kidunia. Washambuliaji waliokuwa juu ya mlima walikuwa wakiwazuia makafiri kuwashambulia waislamu kwa upande wa nyuma. Pindi washirikina walipoanza kushindwa mwanzoni mwa vita, wakatamani ngawira. Hivyo wakawa wameacha amri ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ili nao waweze kupata vishawishi vya kidunia.

[1] 03:165

[2] 03:152

  • Mhusika: Imaam Muhammad Amiyn ash-Shanqiytwiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Islaam diyn al-Kaamil, uk. 21-22
  • Imechapishwa: 14/06/2023