Miongoni mwa mambo hayo ni kwamba baadhi yao wanafikiria kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anahudhuria maulidi. Kwa ajili hiyo wanasimama kwa ajili yake hali ya kumtolea salamu na kumkaribisha, jambo ambalo ni batili kubwa na ujinga mbaya. Hakika Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hatotoka kaburini mwake kabla ya siku ya Qiyaamah, hawasiliani na mtu yeyote na wala hahudhurii mikusanyiko yao. Bali atakaa ndani ya kaburi lake mpaka siku ya Qiyaamah. Roho yake iko ngazi ya juu kabisa kwa Mola wake Peponi. Allaah (Ta´ala) amesema katika Suurah “al-Mu´minuun”:

ثُمَّ إِنَّكُم بَعْدَ ذَٰلِكَ لَمَيِّتُونَ  ثُمَّ إِنَّكُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ تُبْعَثُونَ

“Kisha nyinyi, baada ya hayo, ni wenye kufa. Kisha hakika nyinyi Siku ya Qiyaamah mtafufuliwa.”[1]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mimi ndiye wa kwanza ambaye nitayefukuliwa na kaburi siku ya Qiyaamah, mimi ndiye mwombezi wa kwanza na ndiye wa kwanza atakayeitikiwa maombezi yake.”[2]

Swalah na amani zimwendee yeye.

Aayah na Hadiyth hii tukufu na Aayah na Hadiyth nyenginezo zilizo na maana kama hiyo zote zinajulisha kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wafu wengine watatoka ndani ya makaburi yao siku ya Qiyaamah. Hili ni jambo ambalo kuna maafikiano kati ya wanazuoni wa Kiislamu na hakuna mzozo kati yao. Kwa hiyo inatakikana kwa kila muislamu kuzinduka juu ya jambo hili, kutahadhari na yale yaliyozuliwa na wajinga na watu mfano wao katika Bid´ah na mambo ya ukhurafi ambayo Allaah hakuyateremshia hoja yoyote.

[1] 23:15-16

[2] Muslim (2278).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr minal-Bid´ah, uk. 12-13
  • Imechapishwa: 12/01/2022