Kuwaamini Mitume ina maana ya kuwasadikisha wote, kuanzia wale ambao Allaah amewataja kwa majina na wale ambao hakuwataja kwa majina, kuanzia wale wa mwanzo wao mpaka wa mwisho wao. Wa mwisho wao ni Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kuwaamini Mitume inatakiwa iwe kwa njia ya ujumla. Kuhusu kumwamini Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) inatakiwa iwe kwa upambanuzi na kuamini kuwa yeye ndiye Mtume wa mwisho na kwamba hakuna Mtume mwengine baada yake. Asiyeamini hivo basi huyo ni kafiri.

Jengine ni kwamba kuwaamini Mitume haina maana ya kupetuka mipaka kwao na kuzembea katika haki zao. Hivi ni tofauti na wanavyofanya mayahudi na manaswara ambao wamoja wamevuka mipaka na wengine wakazembea kwa baadhi ya Mitume mpaka wakawafanya kuwa wao ni wana wa Allaah. Amesema (Ta´ala):

وَقَالَتِ الْيَهُودُ عُزَيْرٌ ابْنُ اللَّـهِ وَقَالَتِ النَّصَارَى الْمَسِيحُ ابْنُ اللَّـهِ

“Mayahudi wanasema: “‘Uzayr ni mwana wa Allaah” na manaswara wanasema: “al-Masiyh ni mwana wa Allaah.””[1]

Suufiyyah na wanafalsafa wamezembea na kupunguza haki za Mitume pale walipowafadhilisha viongozi wao juu yao. Waabudia mizimu na wakanamungu wamewakufuru Mitume wote. Mayahudi wamemkufuru ´Iysaa na Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam). Manaswara wamemkufuru Muhammad. Ambaye atawaamini baadhi yao na akawakufuru wengine, basi amewakufuru wote. Amesema (Ta´ala):

إِنَّ الَّذِينَ يَكْفُرُونَ بِاللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيُرِيدُونَ أَن يُفَرِّقُوا بَيْنَ اللَّـهِ وَرُسُلِهِ وَيَقُولُونَ نُؤْمِنُ بِبَعْضٍ وَنَكْفُرُ بِبَعْضٍ وَيُرِيدُونَ أَن يَتَّخِذُوا بَيْنَ ذَٰلِكَ سَبِيلًا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْكَافِرُونَ حَقًّا

“Hakika wale waliomkufuru Allaah na Mitume Wake na wanataka kufarikisha baina ya Allaah na Mitume Wake na wanasema: “Tunawaamini baadhi na tunawakanusha baadhi” na wanataka kuchukua njia iliyo baina ya hayo – basi hao ndio makafiri wa kweli.”[2]

لَا نُفَرِّقُ بَيْنَ أَحَدٍ مِّن رُّسُلِهِ

“Hatutafautishi baina ya yeyote kati ya Mitume Wake.”[3]

[1] 09:30

[2] 04:150-151

[3] 02:285

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Min Usuwl ´Aqiydah Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 20-21
  • Imechapishwa: 12/05/2022