08. Mke mwema hamtii mume wake uzito katika matumizi

Katika sifa za mke mwema ni kutomtia mume uzito kwa matumizi na kutumia mali ya mume kwa israfu na ubadhirifu. Anatakiwa kuwa mkati na kati:

وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامً

“Na wale ambao wanapotoa huwa hawafanyi israfu na wala hawafanyi uchoyo na wanakuwa wastani baina ya hayo.”[1]

Wacha tuzingatie katika mlango huu yale ambayo Abu Sa´iyd na Jaabir wamepokea kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba siku moja alisimama na kukhutubu Khutbah ndefu na akataja mambo ya duniani na Aakhirah na akasema:

“Mwanzoni mwa kuangamia kwa wana wa israaiyl ilikuwa ni mwanamke wa fakiri alikuwa akimkalifisha [mume wake] nguo na vipodozi yale anayokalifisha mwanamke wa tajiri. Kulikuwa mwanamke mmoja wa ki-israaiyl mfupi ambaye alikuwa akitumia mbao mbili za miguu na alikuwa na pete yenye kufungwa ambayo alikuwa akiijaza miski. Akatoka nje kati ya wanawake wawili warefu. Wakatuma mtu awafuate [hawa wanawake watatu]. Akawajua wale wanawake wawili warefu na akawa hakumjua yule mwanamke wa miguu ya mbao.”[2]

Mara ya kwanza wana wa israaiyl kuangamia ilianza kwa mwanamke wa fakiri mmoja kumkalifisha mume wake vipodozi na mapambo ambayo mwanamke wa tajiri anamkalifisha mume wake. Tazama huyu mwanamke mfupi amevyofanya israfu, ubadhirifu wa mali katika mambo yasiyokuwa na faida, udanganyifu na kutokinaika na yale Aliyomuandikia Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Mwanamke mwenye kuvaa viatu vya kisigino kirefu anafanana na mwanamke huyu. al-Lajnah ad-Daaimah wametoa fatwa ifuatayo:

“Kuvaa viatu vya kisigino kirefu haijuzu. Kwa sababu vinamtia mwanamke khatarini. Shari´ah imemwamrisha mtu kujiepusha na mambo ya khatari. Allaah (Ta´ala) Amesema:

وَلَا تُلْقُوا بِأَيْدِيكُمْ إِلَى التَّهْلُكَةِ

“Wala msijitupe kwa mikono yenu katika maangamizi.”[3]

وَلَا تَقْتُلُوا أَنفُسَكُمْ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ بِكُمْ رَحِيمًا

“Wala msijiue. Kwani hakika Allaah kwenu ni Mwenye huruma.”[4]

Vilevile vinamuonyesha mwanamke kuwa mrefu na makalio zaidi ya alionayo, jambo ambalo kuna udanganyifu ndani yake na ni kuonyesha baadhi ya mapambo ambayo imeharamishwa kuyaonesha.”

[1] 25:67

[2] Ibn Khuzaymah katika ”Kitaab-ut-Tawhiyd” (487). Imaam al-Albaaniy amesema kuwa ni Swahiyh katika ”as-Swahiyhah” (591).

[3] 02:195

[4]  04:29

  • Mhusika: Shaykh ´Abdur-Razzaaq bin ´Abdil-Muhsin al-´Abbaad
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifaat-uz-Zawjah as-Swaalihah, uk. 36-38
  • Imechapishwa: 22/07/2018