4- Anas (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah anapomtakia mja Wake kheri, basi humharakishia adhabu duniani, na anapomtakia mja Wake shari, humcheleweshea adhabu ya dhambi yake mpaka siku ya Qiyaamah.”[1]

Miongoni mwa dalili za Allaah kumtakia kheri mja Wake ni kumuharakishia adhabu juu ya dhambi zake hapa duniani. Mtu anatenda dhambi kwa wingi. Hakuna yeyote ambaye amekingwa na kukosea isipokuwa Mitume (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam) katika yale ambayo Allaah amekadiria. Hadiyth inasema:

“Kila mmoja wenu ni mwenye kukosea na mbora wa wenye kukosea ni wale wenye kutubia.”[2]

Mtu hufanya madhambi na mambo mengi yanayoenda kinyume. Allaah akimtakia kheri mja Wake, basi humuharakishia adhabu juu ya madhambi yake hapa duniani ili asafishwe na aingie Peponi akiwa hana madhambi.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… na anapomtakia mja Wake shari, humcheleweshea adhabu ya dhambi yake mpaka siku ya Qiyaamah.”

Anamcheleweshea adhabu pamoja na kwamba anatenda dhambi, anazini na anakwenda kinyume na maamrisho ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Pamoja na haya yote anaishi ndani ya neema na akiwa na afya njema. Hii ni alama mbaya ili aendelee kubaki na madhambi yake. Siku ya Qiyaamah anarejea kwa Allaah akiwa na madhambi yake yote; hakukufutwa dhambi hata moja. Matokeo yake anaadhibiwa kwayo siku ya Qiyaamah. Hioy ni dalili inayoonyesha kwamba mtu kuwa na afya njema siku zote sio dalili inayoonyesha kheri.

Vilevile inafahamsiah kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amekadiria mambo ya kheri na shari. Amekadiria shari kwa hekima Yake na amekadiria kheri kwa hekima Yake. Hakadirii chochote na kujaribu na kutoa mtihani isipokuwa ni kutokana na hekima kubwa.

[1] at-Tirmidhiy (2396), al-Haakim (8799) na Abu Ya´laa (4254). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaami´” (308).

[2] at-Tirmidhiy (2499), Ibn Maajah (4251) na Ahmad (13049) kupitia kwa Anas. Cheni ya wapokezi wake ni dhaifu.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: I´aanat-ul-Mustafiyd bi Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 435-436
  • Imechapishwa: 15/08/2019