3- al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa Ibn Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba amesema:

“Si katika sisi yule mwenye kujipiga kwenye mashavu, akachana nguo na akaita kwa mayowe ya kipindi cha kikafiri.”[1]

Mara nyingi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hulitumia neno hili juu ya maasi yanayofanywa na watu. Lengo ni kuyatahadharisha. Ni kama mfano wa maneno yake:

“Mwenye kutufanyia ghushi si katika sisi.”[2]

“Si katika sisi yule mwenye kujifananisha na wasiokuwa sisi.”[3]

Hadiyth hii imekuja pia kwa mtindo huo. Hadiyth inaonyesha kuwa anatengwa mbali yule mtu mwenye kufanya hivo. Lakin hiyo haina maana kwamba anatoka nje ya Uislamu. Lengo ni kuwafanya watu wakimbie mbali na kitendo hicho. Bora ya yaliyosemwa ni kwamba ni miongoni mwa matamshi yenye kushtua ambayo hayatakiwi kufasiriwa. Lakini hata hivyo mtu anatakiwa kuamini kwamba mwenye kufanya dhambi hiyo hatoki nje ya dini kwa sabbau zipo dalili zengine zenye kuonyesha kuwa wale watu wenye kufanya madhambi makubwa yaliyo chini ya shirki hawatoki nje ya dini. Kuomboleza ni katika madhambi makubwa yaliyo chini ya shirki. Hakumtoi mtu nje ya dini.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kujipiga kwenye mashavu… “

Anajipiga kwenye mashavu kwa sababu ya kusitikika kutokana na msiba, kama walivokuwa wanafanya watu kabla ya kuja Uislamu. Kwa sababu kilichowekwa katika Shari´ah ni kusubiri. Kujipiga kwenye mashavu ni kinyume chake kabisa. Mara nyingi huwa hivo.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… akachana nguo… “

Anachana nguo kwa sababu ya kusitikika kutokana na msiba.

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“… na akaita kwa mayowe ya kipindi cha kikafiri.”

Bi maana asiite wakati wa msiba kwa matamshi yaliyokuwa yakisemwa wakati wa kipindi cha kikafiri.

Makusudio ya kipindi cha kikafiri ni kile kipindi kabla ya kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Baada ya kutumilizwa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) haifai kusema kwamba watu wanaishi katika kipindi cha kikafiri. Hili halifai kabisa. Kwa sababu Allaah ameondosha kipindi hichi kwa kule kumtuma Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hata hivyo kuna uwezekano kwamba zimebaki baadhi ya sifa za kipindi cha kikafiri. Kitendo kinaweza kuwa miongoni mwa kipindi cha kikafiri au miongoni mwa sifa za kipindi cha kikafiri. Lakini haina maana kwamba mwenye kukifanya anakuwa miongoni mwa watu wa kipindi cha kikafiri. Haijuzu kusema namna hiyo baada ya kutimilizwa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Miongoni mwa wito wa kipindi cha kikafiri ni kule kutamka matamshi yake. Kama mfano wa kuita kuwa kuwataka msaada na nusura wengine kwa njia ya ushabiki, umji, uvyama na mfano wake. Yote hayo ni katika matamshi ya kipindi cha kikafiri. Kadhalika kufanya ushabiki juu ya maoni na madhehebu yasiyokuwa na dalili yoyote. Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) amesema:

“Makusudio ya kipindi cha kikafiri ni kila mwenye kufanya ushabiki juu ya madhehebu au kabila.”[4]

Ushabiki wa kipindi cha kikafiri unaingia katika kupiga mayowe ya kipindi cha kikafiri. Haijuzu kwa muislamu kufanya ushabiki na mwanachuoni yeyote au madhehebu yoyote na akatupilia mbali vyengine vyote. Huu ndio ushabiki wa kipindi cha kikafiri. Kadhalika mtu akafanya ushabiki wa kabila lake likiwa liko kwenye makosa. Mshairi amesema:

Hivi mimi ni mwengine ikiwa sio kutoka katika Ghaziyyah?

Pindi wanapopotea, hupotea, na pindi Ghaziyyah wanaposhika njia ya sawa, nami nashika njia ya sawa

Ni wajibu kwa muislamu kuifuata haki ni mamoja inatoka kwa imamu wake, kabila lake au mtu mwengine. Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amesema:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُونُوا قَوَّامِينَ بِالْقِسْطِ شُهَدَاءَ لِلَّـهِ وَلَوْ عَلَىٰ أَنفُسِكُمْ أَوِ الْوَالِدَيْنِ وَالْأَقْرَبِينَ

“Enyi walioamini! Kuweni wasimamizi wa uadilifu mtoapo ushahidi kwa ajili ya Allaah japokuwa ni dhidi ya nafsi zenu au wazazi wawili au jamaa wa karibu.”[5]

Haijuzu kufanya ushabiki kwa madhehebu, watu wala kwa makabila. Muislamu anaifuata haki pasi na kujali ni yenye kutoka wapi. Hafanyi ushabiki. Haiachi haki ilio na yule mgomvi wake. Muislamu ni mwenye kuzunguka na haki popote inapokwenda. Ni mamoja iko katika madhehebu yake, imamu wake, kabila lake au hata adui yake. Ni bora kurejea katika haki kuliko mtu aendelee kushikamana na batili. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَإِذَا قُلْتُمْ فَاعْدِلُوا وَلَوْ كَانَ ذَا قُرْبَىٰ

“Mnaposema basi fanyeni uadilifu japokuwa ni jamaa wa karibu.”[6]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Sema haki japokuwa ni chungu.”[7]

[1] al-Bukhaariy (1294) na Muslim (103).

[2] Muslim (283) na Ahmad (9396) kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh).

[3] at-Tirmidhiy (2695) kupitia kwa Ibn ´Amr. Hadiyth ni nzuri. Tazama ”Swahiyh-ul-Jaami´” (5434).

[4] Tazama ”Zaad-ul-Ma´aad” (2/428).

[5] 04:135

[6] 06:152

[7] Ibn Hibbaan (361), at-Twabaraaniy katika ”Makaarim-ul-Akhlaaq” (1), al-Qadhwaa´iy katika ”Musnad-ush-Shihaab” (1/378) na al-Bayhaqiy katika ”Shu´b-ul-Iymaan” (4/243) kupitia kwa Abu Dharr. Cheni ya wapokezi ni dhaifu sana.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: I´aanat-ul-Mustafiyd bi Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 434-435
  • Imechapishwa: 15/08/2019