Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:

“Katika Sunnah hakuna kipimo [Qiyaas]. Sunnah hailinganishwi na kitu kingine.”

MAELEZO

Haya ambayo Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) anathibitisha juu ya ´Aqiydah ya Kiislamu na Shari´ah zake kwa ujumla ndio yanayothibitishwa na Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah katika kila zama na mahali. Haifai kuleta vipimo visivyokuwa na msingi katika Qur-aan na Sunnah. Malinganishi kama haya hayatakiwi kutumiwa katika Sunnah. Wala haitakiwi kutumia vipimo katika majina na sifa za Allaah. Hukumu za Qur-aan ziko wazi kabisa. Zimebainishwa na wanachuoni wanaowafuata Salaf ambao wameisoma Qur-aan na kuelewa maana na hukumu zake. ´Abdur-Rahmaan as-Sulamiy amesema:

“Wale tuliosoma Qur-aan kwao, ´Uthmaan bin ´Affaan, ´Abdullaah bin Mas´uud na wengineo, wametuhadithia kwamba: “Baada ya kuhifadhi Aayah kumi pamoja na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), tulikuwa hatuzivuki mpaka kwanza tujifunze ile elimu na matendo yaliyomo ndani yake.” Hivyo tukajifunza Qur-aan, elimu na matendo.”

Watu hawa ndio maimamu wa Salaf na wabebaji wa elimu waliosafiri kwenda mashariki na magharibi kwa ajili ya kuikusanya Sunnah. Wakati huo Sunnah ilikuwa imesambaa kwenye vifua vya watu na madaftari yao. Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) akawafanya kuitumikia na akawasaidia kubainisha hukumu za Qur-aan na kukusanya yale yote yaliyosikiwa kutoka katika Sunnah tukufu ya Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hata kama hakuna yeyote awezaye kuikusanya Sunnah yote si kwenye kifua chake wala madaftari yake, lakini imekusanywa yote katika vitabu vya wanachuoni. Sunnah imekusanywa na hakuna Hadiyth hata moja inayokosekana. Hayo yako wazi sana.

Allaah amewateua wanaume ambao wameweza kuifikia elimu yenye manufaa ambao wameweza kutenganisha kati ya Hadiyth dhaifu, Swahiyh na zile Hadiyth zilizozuliwa ambazo zimeundwa na maadui wa dini. Wamezua cheni za wapokezi na baadaye wakazinasibisha kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haya wanayatambua wanafunzi. Wanayasoma na kuyasikia kwenye vitabu. Mara nyingi wanachuoni wanasema kuwa Hadiyth fulani imezuliwa, dhaifu sana, Swahiyh au nzuri kwa mujibu wa kanuni sahihi na salama. Yote hayo ni kwa fadhilah za Allaah kisha kwa juhudi za wale walioteuliwa na Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) juu ya kitendo hichi kitukufu ili dini yote kwa ´Aqiydah na Shari´ah iwe safi na takasifu. Ni ujira mkubwa ulioje walionao! Ni ujira mkubwa ulioje walionao wale ambao wanafikisha na kuitumikia elimu sahihi! Fadhilah kubwa inapatikana kwa kuwa woa ni warithi wa Manabii na Mitume (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam). Mitume ndio wakati na kati baina ya Allaah (Subhaanah) na waja Wake. Hakukubaki Nabii yeyote. Wote wamefariki na wa mwisho wao alikuwa ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye ndiye mbora wao. Wamebaki wale waaminifu juu ya Shari´ah yake, nao si wengine ni wanachuoni wanaowafunza watu hatua kwa hatua. Hawa wameirithi elimu ya Qur-aan na Sunnah na wakafahamu vyema hukumu. Wamefahamu makusudio ya Allaah juu ya waja Wake na wakawafikishia Ummah kwa kuwafunza, kuwatungia, ulinganizi, fatwa na kutatua matatizo na mizozo mbalimbali. Yote haya yanafanywa na wanachuoni. Hakuna yeyote awezaye kuiziba kazi yao. Hakuna yeyote awezaye kusimama nafasi yao. Inatosha wao kuwa ni warithi wa Manabii na wa Mitume ili kuthibitisha fadhilah na utukufu wao. Imekuja katika Hadiyth Swahiyh:

“Hakika wanachuoni ni warithi wa Mitume. Hakika Mitume hawakurithi dinari wala dirhamu, bali wamerithi elimu. Hivyo basi yule atakayejichumia nayo basi amejichumia fungu kubwa.”[1]

[1] at-Tirmidhiy (2682) na Ibn Maajah (223).

  • Mhusika: ´Allaamah Zayd bin Muhammad al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Latwiyfah ´alaa Usuwl-is-Sunnah al-Muniyfah, uk. 31-32
  • Imechapishwa: 02/10/2019