07. Hadiyth “Wakati tulipokuwa tumekaa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)… “

Hadiyth ya saba

7- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza akisema:

“Wakati tulipokuwa tumekaa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuja mtu akisema: “Ee Mtume wa Allaah! Nimeangamia!” Akasema: “Ni kipi kilichokuangamiza?” Akajibu: “Nimemwingilia mke wangu ilihali nimefunga.”

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Nimemsibu mke wangu katika Ramadhaan.”

Mtume wa Allaah akasema: “Unaweza kupata mtumwa ukamwacha huru?” Akajibu: “Hapana.” Akasema: “Unaweza kufunga miezi miwili mfululizo?” Akajibu: “Hapana.” Akasema: “Unaweza kupata chakula cha kuwalisha masikini sitini?” Akajibu: “Hapana.” Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akanyamaza. Tulipokuwa katika hali hiyo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaja na chombo kilicho na tende ambapo akauliza: “Yuko wapi muulizaji?” Akajibu: “Ni mimi hapa.” Akamwambia: “Chukua ukatoe swadaqah.” Akasema: “Hivi kuna ambaye ni fakiri kuliko mimi, ee Mtume wa Allaah? Ninaapa kwa Allaah hakuna kati ya milima miwili hii watu wa nyumba ambao ni mafukara kuliko watu wa nyumbani kwangu.” Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akacheka mpaka yakaonekana magego yake. Kisha akasema: “Walishe watu wa nyumbani kwako.”

Hukumu zinazochukuliwa kutoka katika Hadiyth:

1- Kumwingilia mke mchana wa Ramadhaan ni miongoni mwa machafu yenye kuangamiza. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimuunga mkono juu ya maneno yake “nimeangamia” na ilihali hakuwa hivo. Alimfanyia jambo kuwa lepesi.

2- Kumwingilia mke mchana wa Ramadhaan kunawajibisha kutoa kafara. Kafara inatakiwa kutolewa kwa mpangilio; kumwacha mtumwa huru, asipopata basi afunge miezi miwili mfululizo, asipoweza alishe masikini sitini.

3- Kafara haianguki kwa kutokuweza. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakumuangushia nayo kwa sababu ya ufakiri wake. Katika Hadiyth hakuna kinachofahamisha juu ya kuanguka.

4- Kujuzu kumtolea kafara mwingine hata kama atakuwa ni mtu ajinabi.

5- Inafaa kwake kula katika chakula hicho na kuwalisha familia yake midhali imetoka kwa mwingine asiyekuwa yeye.

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdullaah bin ´Abdir-Rahmaan al-Bassaam
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Taysiyr-ul-´Allaam Sharh ´Umdat-il-Ahkaam, uk. (01/322-323)
  • Imechapishwa: 25/05/2018