06. Sura ya kwanza: Ubainifu wa maana ya Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah, maumbile yake na kwamba washirikina walikuwa wakiikubali

Tawhiyd kwa maana yake yenye kuenea ni kuitakidi upwekekaji wa Allaah (Ta´ala) kwa uola, kumtakasia Yeye ´ibaadah na kumthibitishia majina Yake na sifa Zake. Tawhiyd imegawanyika aina tatu; Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah, Tawhiyd-ul-Uluuhiyyah na Tawhiyd-ul-Asmaa´ was-Swifaat. Kila aina ina maana yake ambayo ni lazima kuibainisha ili ipate kubainika tofauti kati ya aina hizi:

1- Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah. Ni kumpwekesha Allaah (Ta´ala) kwa matendo Yake kwa njia ya kwamba mtu aamini kuwa Yeye pekee ndiye muumbaji wa viumbe wote:

اللَّـهُ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ

”Allaah ni muumbaji wa kila kitu.”[1]

Kwamba Yeye ndiye muumbaji wa viumbe wote wakiwemo wanadamu na wengineo:

وَمَا مِن دَابَّةٍ فِي الْأَرْضِ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ رِزْقُهَا

“Hakuna kiumbe chochote kitembeacho katika ardhi isipokuwa riziki yake iko kwa Allaah.”[2]

Kwamba Yeye ndiye mfalme wa wafalme na mwendeshaji wa mambo ya ulimwenguni yote; anampa na kumvua utawala amtakaye, anamtukuza na anamdhalilisha amtakaye, ni muweza wa kila jambo, anaendesha usiku na mchana na anahuisha na anafisha:

قُلِ اللَّـهُمَّ مَالِكَ الْمُلْكِ تُؤْتِي الْمُلْكَ مَن تَشَاءُ وَتَنزِعُ الْمُلْكَ مِمَّن تَشَاءُ وَتُعِزُّ مَن تَشَاءُ وَتُذِلُّ مَن تَشَاءُ ۖ بِيَدِكَ الْخَيْرُ ۖ إِنَّكَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ تُولِجُ اللَّيْلَ فِي النَّهَارِ وَتُولِجُ النَّهَارَ فِي اللَّيْلِ ۖ وَتُخْرِجُ الْحَيَّ مِنَ الْمَيِّتِ وَتُخْرِجُ الْمَيِّتَ مِنَ الْحَيِّ ۖ وَتَرْزُقُ مَن تَشَاءُ بِغَيْرِ حِسَابٍ

“Sema: “Ee Allaah, mfalme uliyemiliki ufalme wote, unampa ufalme umtakaye, na unamwondoshea ufalme umtakaye, na unamtukuza umtakaye, na unamdhalilisha umtakaye, kheri imo mkononi mwako – hakika Wewe juu ya kila jambo ni muweza. Unauingiza usiku ndani ya mchana na unauingiza mchana ndani ya usiku na unatoa kilicho hai kutokana na kilicho mfu na unatoa kilicho mfu kutokana na kilicho hai na unamruzuku umtakaye bila ya hesabu.”[3]

Allaah amepinga kuwa na mshirika na msaidizi katika ufalme kama alivyopinga (Subhaanah) kuwa na mshirika katika uumbaji na utoaji riziki. Amesema (Ta´ala):

هَـٰذَا خَلْقُ اللَّـهِ فَأَرُونِي مَاذَا خَلَقَ الَّذِينَ مِن دُونِهِ

”Huu ni uumbaji wa Allaah, basi nionyesheni ni kitu gani walichokiumba wasiokuwa Yeye.”[4]

أَمَّنْ هَـٰذَا الَّذِي يَرْزُقُكُمْ إِنْ أَمْسَكَ رِزْقَهُ

“Au ni nani huyu ambaye atakuruzukuni ikiwa [Allaah] atazuia riziki Yake?”[5]

Kama alivyotangaza upwekekaji Wake wa uola juu ya viumbe wote. Amesema:

الْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ

“Himdi zote njema zinamstahikia Allaah, Mola wa walimwengu.”[6]

إِنَّ رَبَّكُمُ اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ يُغْشِي اللَّيْلَ النَّهَارَ يَطْلُبُهُ حَثِيثًا وَالشَّمْسَ وَالْقَمَرَ وَالنُّجُومَ مُسَخَّرَاتٍ بِأَمْرِهِ ۗ أَلَا لَهُ الْخَلْقُ وَالْأَمْرُ ۗ تَبَارَكَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ

“Hakika Mola wenu ni Allaah ambaye ameumba mbingu na ardhi katika siku sita kisha akalingana juu ya ‘Arshi; anafunika usiku kwa mchana unaufuatia upesiupesi na [ameumba] jua na mwezi na nyota – vyote vimetiishwa kwa amri Yake. Zindukeni! Uumbaji ni Wake pekee na kupitisha amri. Amebarikika Allaah Mola wa walimwengu.”[7]

Allaah amewafanya viumbe wote kuwa na maumbile ya kukubali uola kiasi cha kwamba mpaka wale washirikina ambao wamefanya washirika katika ´ibaadah wanakiri kupwekeka Kwake katika uola. Amesema (Ta´ala):

قُلْ مَن رَّبُّ السَّمَاوَاتِ السَّبْعِ وَرَبُّ الْعَرْشِ الْعَظِيمِ سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ ۚ قُلْ أَفَلَا تَتَّقُونَ قُلْ مَن بِيَدِهِ مَلَكُوتُ كُلِّ شَيْءٍ وَهُوَ يُجِيرُ وَلَا يُجَارُ عَلَيْهِ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ ۚ قُلْ فَأَنَّىٰ تُسْحَرُونَ

“Sema: “Nani Mola wa mbingu saba na Mola wa ‘Arshi tukufu?” Watesema: ”Ni ya Allaah pekee.” Sema: ”Je, basi hamumchi Allaah?” Sema: ”Nani katika mikono Yake uko ufalme wa kila kitu Naye ndiye alindaye na wala hakilindwi chochote kinyume Naye ikiwa mnajua?” Watasema: ”Ni Allaah pekee.” Sema: ”Basi vipi mnazugwa?”[8]

Hakuna kundi lolote la wanadamu linalotambulika kupingana na Tawhiyd hii. Bali mioyo imeumbwa na maumbile ya kuikubali kiasi kikubwa kuliko ilivyoumbwa na maumbile ya kukubali vitu vyengine vilivyopo. Kama walivosema Mitume katika yale ambayo Allaah amesimulia kutoka kwao:

قَالَتْ رُسُلُهُمْ أَفِي اللَّـهِ شَكٌّ فَاطِرِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ

“Wakasema Mitume wao: “Je, kuna shaka kuhusiana na Allaah, mwanzilishi wa mbingu na ardhi.”[9]

Aliyeshuhurika zaidi kujitia ujinga na kudhihirisha kwamba hakuna Mola ni Fir´awn. Lakini hata hivyo kwa ndani alikuwa akiyakinisha. Muusa alimwambia:

قَالَ لَقَدْ عَلِمْتَ مَا أَنزَلَ هَـٰؤُلَاءِ إِلَّا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ بَصَائِرَ

“Akasema: “Hakika umekwishajua kwamba hakuna aliyeteremsha haya isipokuwa Mola wa mbingu na ardhi kuwa ni dalili za kuonekana dhahiri.”[10]

Amesema kumuhusu na watu wake:

وَجَحَدُوا بِهَا وَاسْتَيْقَنَتْهَا أَنفُسُهُمْ ظُلْمًا وَعُلُوًّا

“Wakazipinga kwa dhuluma na majivuno na hali kuwa nafsi zao zimeziyakinisha. “[11]

Vivyo hivyo watu ambao leo wanapinga Mola, ambao ni wakomunisti, wanapinga kwa dhahiri kwa ajili ya kiburi. Vinginevyo kwa ndani ni lazima wakiri kuwa hakuna kilichopo isipokuwa kuna ambaye amekifanya kipatikane, kwamba hakuna kiumbe chochote isipokuwa kina muumbaji na kwamba hakuna athari yoyote isipokuwa ina aliyeifanya athari hiyo. Amesema (Ta´ala):

أَمْ خُلِقُوا مِنْ غَيْرِ شَيْءٍ أَمْ هُمُ الْخَالِقُونَ  أَمْ خَلَقُوا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ ۚ بَل لَّا يُوقِنُونَ

“Au wameumbwa pasipo na kitu chochote au wao ndio waumbaji au wameumba mbingu na ardhi? Bali hawana yakini.”[12]

Zingatia ulimwengu wote; juu yake na chini yake, kwa nyanja zake zote, utaona kuwa ni wenye kushuhudia kuthibitisha muundaji Wake, mwendeshaji Wake na mfalme Wake. Kukanusha na kupinga muundaji Wake katika akili na maumbile ni sawa na kukanusha na kupinga ulimwengu. Hakuna tofauti kati ya hayo mawili. Kwa sababu ulimwengu sahihi unathibitisha kuwepo kwa muumbaji. Yale ambayo wakomunisti wanayojigamba kwayo hii leo katika kupinga uwepo wa Mola ni kwa njia ya kiburi tu na hakutokamani na akili timamu na fikira za usawa. Yule ambaye hii ndio hali yake akili yake imemwondoka na amewaita watu kumchezea shere. Mshairi amesema:

Ni vipi ataasiwa mungu na akakanushwa na mwenye kukanusha

ilihali katika kila kitu kuna alama kinachofahamisha kuwa Yeye ni mmoja

[1] 39:62

[2] 11:06

[3] 03:26-27

[4] 31:11

[5] 67:21

[6]  01:02

[7] 07:54

[8] 23:86-89

[9] 14:10

[10] 17:102

[11] 27:14

[12] 52:35-36

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 21-24
  • Imechapishwa: 23/01/2020