06. Mtume aliwapiga vita washirikina wote bila kubagua

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Msingi wa tatu ni kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuja kwa watu waliokuwa ni wenye kutofautiana katika ´ibaadah zao. Miongoni mwao kuna ambao walikuwa wakiabudu Malaika, wengine walikuwa wakiwaabudu Mitume na waja wema, wengine wakiabudu mawe na miti na wengine wakiabudu mwezi na jua. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwapiga vita na hakutofautisha kati yao. Dalili ni maneno Yake (Ta´ala):

وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ كُلُّهُ لِلَّـهِ

“Na piganeni nao mpaka kusiweko fitina na dini yote iwe kwa ajili ya Allaah.”[1]

Dalili ya jua na mwezi ni maneno Yake (Ta´ala):

وَمِنْ آيَاتِهِ اللَّيْلُ وَالنَّهَارُ وَالشَّمْسُ وَالْقَمَرُ ۚ لَا تَسْجُدُوا لِلشَّمْسِ وَلَا لِلْقَمَرِ وَاسْجُدُوا لِلَّـهِ الَّذِي خَلَقَهُنَّ إِن كُنتُمْ إِيَّاهُ تَعْبُدُونَ

“Na katika ishara Zake, ni usiku na mchana na jua na mwezi. Hivyo basi msisujudie jua na wala mwezi; bali msujudieni Allaah ambaye aliyeviumba [hivyo] ikiwa Yeye pekee mnamwabudu.”[2]

Dalili ya Malaika ni maneno Yake (Ta´ala):

وَلَا يَأْمُرَكُمْ أَن تَتَّخِذُوا الْمَلَائِكَةَ وَالنَّبِيِّينَ أَرْبَابًا

“Na wala hakuamuruni kuwafanya Malaika na Manabii kuwafanya miungu.”[3]

Dalili ya Mitume ni maneno Yake (Ta´ala):

وَإِذْ قَالَ اللَّـهُ يَا عِيسَى ابْنَ مَرْيَمَ أَأَنتَ قُلْتَ لِلنَّاسِ اتَّخِذُونِي وَأُمِّيَ إِلَـٰهَيْنِ مِن دُونِ اللَّـهِ ۖ قَالَ سُبْحَانَكَ مَا يَكُونُ لِي أَنْ أَقُولَ مَا لَيْسَ لِي بِحَقٍّ ۚ إِن كُنتُ قُلْتُهُ فَقَدْ عَلِمْتَهُ ۚ تَعْلَمُ مَا فِي نَفْسِي وَلَا أَعْلَمُ مَا فِي نَفْسِكَ ۚ إِنَّكَ أَنتَ عَلَّامُ الْغُيُوبِ

“Na pale Allaah atakaposema: “Ee ‘Iysaa mwana wa Maryam! Je, wewe uliwaambia watu: “Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni miungu miwili pasi na ya Allaah?” Atasema: “Utakasifu ni Wako! Hainipasi mimi kusema yasiyo kuwa haki kwangu; ikiwa nimesema hayo basi kwa hakika Ungeliyajua – Unayajua yale yote yaliyomo katika nafsi yangu na wala [mimi] sijui yale yaliyomo katika nafsi Yako; hakika Wewe ni Mjuzi wa ghaibu.”[4]

Dalili ya waja wema ni maneno Yake (Ta´ala):

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ يَدْعُونَ يَبْتَغُونَ إِلَىٰ رَبِّهِمُ الْوَسِيلَةَ أَيُّهُمْ أَقْرَبُ وَيَرْجُونَ رَحْمَتَهُ وَيَخَافُونَ عَذَابَهُ

“Hao wanaowaomba [wao wenyewe] wanatafuta kwa Mola wao njia [na] kumkurubia kadri wanavyoweza, na wanataraji rehema Yake na wanakhofu adhabu Yake.”[5]

Dalili ya miti na mawe ni maneno Yake (Ta´ala):

أَفَرَأَيْتُمُ اللَّاتَ وَالْعُزَّىٰ وَمَنَاةَ الثَّالِثَةَ الْأُخْرَىٰ

“Je, mmeona al-Laat na al-‘Uzzaa na Manaat mwengine wa tatu?”[6]

Abu Waaqid al-Laythiyy (Radhiya Allaahu ´anh) amesema:

“Tulitoka pamoja na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwenda Hunayn na sisi ndio punde tu tumetoka katika ukafiri. Washirikina walikuwa na mkunazi unaoitwa “Dhaat Anwaatw” wakiuadhimisha na kutundika silaha zao. Tukapita karibu na mkunazi huo tukasema: “Ee Mtume wa Allaah, tufanyie Dhaat Anwaatw kama jinsi na wao walivyokuwa na Dhaat Anwaatw. Ndipo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Subhaan Allaah! Haya ndio yale yale yaliyosemwa na watu wa Muusa: “Tufanyie mungu kama jinsi na wao walivyokuwa na mungu.” Ninaapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko Mikononi Mwake; mtafuata desturi za waliokuwa kabla yenu.””[7]

MAELEZO

Msingi wa nne ni kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwajia watu wenye kutofautiana katika ´ibaadah zao. Baada yake ametaja msingi wa nne ambao mwenye kuuelewa na kuufahamu vizuri basi atakuwa ameielewa dini ya washirikina na ya Mitume. Sambamba na hilo ataelewa tofauti kati yake. Ni msingi ambao ni muhimu na ulio wazi kabisa ambapo ndani yake (Rahimahu Allaah) amebainisha uhakika wa shirki na yale waliyokuwemo washirikina. Kadhalika ameweka wazi uhakika wa yale Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliyolingania kwayo, aliyoelekeza na yale Allaah aliyomtuma kwayo.

Yule ambaye ataielewa misingi hii minne kama inavyostahiki basi atajua dini ya washirikina na dini ya Mitume kielimu. Katika msingi wa kwanza tumetangulia kusema kuwa [washirikina wa kale] wanakubali Tawhiyd-ur-Rubuubiyyah na kwamba wao hawapingi ya kwamba Allaah ndiye Muumbaji, Mruzukaji, Mwenye kuyaendesha mambo, Muhuishaji, Mfishaji na ndiye Mwenye kuwaruzuku viumbe. Walikuwa wanayajua haya. Na ndio maana walikuwa wenye kukubali pale wanapoulizwa:

وَلَئِن سَأَلْتَهُم مَّنْ خَلَقَهُمْ لَيَقُولُنَّ اللَّـهُ

“Na ukiwauliza: “Ni nani kawaumba? Bila shaka watasema: “Allaah”.”[8]

Kama tulivyotangulia kusema.

Katika msingi wa pili amebainisha kuwa walikuwa wakisema kwamba wao hawakuwaomba na kuwaelekea isipokuwa ni kwa sababu ya kutaka kujikurubisha na kutafuta uombezi kutoka kwao. Kwa msemo mwingine ni kwamba hawakuwaelekea kwa sababu walikuwa wanaitakidi kuwa miungu yao ni yenye kuumba na kuruzuku. Walikuwa wanajua kuwa Muumbaji na Mruzukaji ni Allaah pekee. Kilichowafanya wao kuwaabudu ni kwa sababu ya kutaka uombezi kutoka kwao na wawakurubishe kwa Allaah. Allaah (Ta´ala) amesema ya kwamba walisema:

مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ

“Hatuwaabudu isipokuwa kwa lengo la kutukurubisha kwa Allaah ukaribu.”[9]

وَيَقُولُونَ هَـٰؤُلَاءِ شُفَعَاؤُنَا عِندَ اللَّـهِ

“Na wanasema: “Hawa ni waombezi wetu mbele ya Allaah”.”[10]

Hii ndio ilikuwa shirki yao. Walikuwa wakisema ya kwamba wanawaomba na kuwaelekea ili wawakurubishe na wawaombee kwa Allaah. Allaah ndiye Mwenye kuruzuku na Mwenye kuumba (Subhaanahu wa Ta´ala).

Tumetangulia kuzungumzia juu ya uombezi na kusema kuwa kuna uombezi aina mbili:

1 – Uombezi wenye kuridhiwa. Huu ni ule uombezi wenye kutolewa idhini na Allaah na kuuridhia. Ni kama mfano wa uombezi wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa watu wataosimama katika uwanja ili (Subhaanah) aweze kuwahukumu. Vilevile atawaombea waliokuwa wakimuabudu Allaah peke yake ili waweze kuingia Peponi kwa idhini na ridhaa Yake (Subhaanah).

2 – Uombezi batili. Huu ni ule uombezi ambao washirikina wanauomba kutoka kwa asiyekuwa Allaah kama Mitume, waja wema, Malaika, jini au mti. Huu ni uombezi batili. Allaah (Ta´ala) amesema juu yake:

فَمَا تَنفَعُهُمْ شَفَاعَةُ الشَّافِعِينَ

“Basi hautowafaa uombezi wowote ule wa waombezi.”[11]

مَا لِلظَّالِمِينَ مِنْ حَمِيمٍ وَلَا شَفِيعٍ يُطَاعُ

“Madhalimu hawatokuwa na rafiki wa dhati na wala mwombezi anayetiiwa.”[12]

Huu ni uombezi batili kwa sababu umetafutwa kutoka kwa asiyekuwa Allaah na wakafanya Tawassul kwao kwa kufanya shirki. Kwa ajili hii ndio maana ikawa ni uombezi batili.

Halafu akataja msingi wa tatu ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuja kwa watu wenye ushirikina aina mbalimbali. Kuna ambao walikuwa wakiabudia Mitume, Malaika, waja wema, jini, miti, mawe na jua na mwezi. Aliwapiga vita wote. Maswahabah waliwapiga vita wote na hawakutofautisha kati yao. Ametaja Aayah zenye kufahamisha juu ya hilo. Amesema (Jalla wa ´Alaa):

وَلَا يَأْمُرَكُمْ أَن تَتَّخِذُوا الْمَلَائِكَةَ وَالنَّبِيِّينَ أَرْبَابًا ۗ أَيَأْمُرُكُم بِالْكُفْرِ بَعْدَ إِذْ أَنتُم مُّسْلِمُونَ

“Na wala hakuamuruni kuwafanya Malaika na Manabii kuwafanya miungu. Je, anakuamrisheni ukafiri baada ya nyinyi kuwa waislamu?”

Amefanya ´ibaadah wanayofanyiwa Malaika na Mitume kuwa ni kufuru. Kisha akataja kisa cha ´Iysaa na manaswara:

مَا قُلْتُ لَهُمْ إِلَّا مَا أَمَرْتَنِي بِهِ أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ رَبِّي وَرَبَّكُمْ ۚ وَكُنتُ عَلَيْهِمْ شَهِيدًا مَّا دُمْتُ فِيهِمْ ۖ فَلَمَّا تَوَفَّيْتَنِي كُنتَ أَنتَ الرَّقِيبَ عَلَيْهِمْ ۚ وَأَنتَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ

“Sijawaambia lolote ila yale Uliyoniamrisha kwayo kwamba: Mwabuduni Allaah Mola wangu na Mola wenu. Na nilikuwa juu yao shahidi wakati nilipokuwa nao. Uliponichukua juu [mbinguni] Ulikuwa Wewe ni Mwenye kuchunga juu yao – na Wewe juu ya kila kitu ni Mwenye kushuhudia.”[13]

Akataja kuhusu miti, mawe na waja wema:

أَفَرَأَيْتُمُ اللَّاتَ وَالْعُزَّىٰ وَمَنَاةَ الثَّالِثَةَ الْأُخْرَىٰ

“Je, mmeona al-Laat na al-‘Uzzaa na Manaat mwengine wa tatu?”[14]

al-Laat alikuwa ni mja mwema.

al-Manaat ilikuwa ni jiwe.

al-´Uzzaa ilikuwa ni mti.

Pamoja na hivyo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) wakawapiga vita. Hawakutofautisha kati yao. Shirki ni kitu kimoja hata kama vinavyoabudiwa vitakuwa aina mbalimbali. Anayeabudu jua, mwezi, Malaika, Mitume, waja wema na nyota wote ni washirikina. Amesema (Ta´ala):

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ

“Na hawakuamrishwa chochote kile isipokuwa wamwabudu Allaah hali ya kumtamasia Yeye dini.”[15]

وَقَضَىٰ رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ

“Mola wako amehukumu kwamba msimwabudu yeyote isipokuwa Yeye pekee.”[16]

فَاعْبُدِ اللَّـهَ مُخْلِصًا لَّهُ الدِّينَ

“Basi mwabudu Allaah pekee ukimtakasia Yeye dini.”[17]

فَإِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ

“Kwa hiyo Mungu wenu wa haki ni Mungu mmoja tu.”[18]

Mwenye kwenda kinyume na Aayah hii na nyenginezo zenye maana kama hiyo, basi ameshirikisha. Ni mamoja awe amewafanyia hivo Mitume, waja wema, Malaika, jini, nyota, jua, mwezi au vinginevyo. Ndio maana Allaah (Jalla wa ´Alaa) akawa ameteremsha juu yao:

وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ كُلُّهُ لِلَّـهِ

“Na piganeni nao mpaka kusiweko fitina na dini yote iwe kwa ajili ya Allaah.”

Shirki huitwa pia kuwa ni fitina. Kwa mfano maneno Yake (Ta´ala):

وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ كُلُّهُ لِلَّـهِ

“Na piganeni nao mpaka kusiweko fitina na dini yote iwe kwa ajili ya Allaah.”[19]

Bi maana mpaka Allaah asishirikishwe.

Vivyo hivyo husemwa fitina kwa kukusudia tofauti, maasi na kadhalika. Lakini katika Aayah hii kinachokusudiwa ni kumshirikisha Allaah. Amesema (Jalla wa ´Alaa):

يَسْأَلُونَكَ عَنِ الشَّهْرِ الْحَرَامِ قِتَالٍ فِيهِ ۖ قُلْ قِتَالٌ فِيهِ كَبِيرٌ ۖ وَصَدٌّ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ وَكُفْرٌ بِهِ وَالْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَإِخْرَاجُ أَهْلِهِ مِنْهُ أَكْبَرُ عِندَ اللَّـهِ ۚ وَالْفِتْنَةُ أَكْبَرُ مِنَ الْقَتْلِ

“Wanakuuliza kuhusu miezi mitukufu [kama inafaa] kupigana humo. Sema: “Kupigana humo ni [dhambi] kubwa. Na kuzuia [watu kufuata] njia ya Allaah na kumkanusha Yeye na [kuzuia watu wasiende] al-Masjid al-Haraam na kuwatoa watu wake humo ni [dhambi] kubwa zaidi mbele ya Allaah. Na fitina ni mbaya zaidi kuliko kuua.”[20]

Fitina bi manaa shirki.

Ni dalili yenye kufahamisha kuwa ni wajibu kwa watawala kuwapiga vita wenye kumuabudu asiyekuwa Allaah yeyote awaye. Watapowalingania katika dini ya Allaah na kuwaelekeza na wasiitikie, basi ni wajibu kuwapiga vita ikiwa wana uwezo wa kufanya hivo:

فَاتَّقُوا اللَّـهَ مَا اسْتَطَعْتُمْ

“Basi mcheni Allaah muwezavyo.”[21]

وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ كُلُّهُ لِلَّـهِ

“Na piganeni nao mpaka kusiweko fitina na dini yote iwe kwa ajili ya Allaah.”[22]

انفِرُوا خِفَافًا وَثِقَالًا وَجَاهِدُوا بِأَمْوَالِكُمْ وَأَنفُسِكُمْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ ۚ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ

“Tokeni mwende [vitani] mkiwa wepesi na wazito na fanyeni jihaad kwa mali zenu na nafsi zenu katika njia ya Allaah. Hivyo ni kheri kwenu mkiwa mnajua.” [23]

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا هَلْ أَدُلُّكُمْ عَلَىٰ تِجَارَةٍ تُنجِيكُم مِّنْ عَذَابٍ أَلِيمٍ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَتُجَاهِدُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ بِأَمْوَالِكُمْ وَأَنفُسِكُمْ ۚ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ

“Enyi mlioamini! Nikujulisheni biashara itakayokuokoeni na adhabu iumizayo? Mumuamini Allaah na Mtume Wake na mfanye Jihaad katika njia ya Allaah kwa mali zenu na nafsi zenu. Hivyo ndiyo bora kwenu mkiwa mnajua.”[24]

Miongoni mwa yanayohusiana na ´ibaadah ya kuabudu mawe na miti ni pamoja vilevile na Hadiyth ya Abu Waaqid al-Laythiyy pindi walipotoka kwenda katika Hunayn na ndio walikuwa karibuni wametoka katika kufuru. Mara wakapita pembezoni mwa washirikina ambao walikuwa wakiabudu mkunazi, wakiuadhimisha na wakitundika silaha zao na kusema kwamba wakifanya hivo silaha ndio zinakuwa na bahati zaidi na nguvu. Waislamu wale wakawa wamesema:

“Tufanyie Dhaat Anwaatw kama jinsi na wao walivyokuwa na Dhaat Anwaatw. Ndipo Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Subhaan Allaah! Haya ndio yale yale yaliyosemwa na watu wa Muusa: “Tufanyie mungu kama jinsi na wao walivyokuwa na mungu.”

Akafanya (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kitendo cha wao kuomba wafanyiziwe mti wauabudu ni kama msemo wa wana wa israaiyl waliposema wafanyiziwe mungu kama ambavyo na wao wako na mungu.

Kwa hivyo watu wakisema kuwa wanataka mti wa kuabudu, jiwe la kuabudu, kaburi la kuabudu au ambalo watatundika silaha zao juu, kuliomba, kulitaka uokozi na kuliwekea nadhiri ni kama mfano wa maneno ya wana wa israaiyl:

اجْعَل لَّنَا إِلَـٰهًا كَمَا لَهُمْ آلِهَةٌ

“Tufanyie nasi mungu kama walivokuwa [hawa] wana miungu.”[25]

Huu ni msingi mkubwa pamoja na misingi iliyotangulia.

[1] 08:39

[2] 41:37

[3] 03:80

[4] 05:116

[5] 17:57

[6] 53:19-20

[7] at-Tirmidhiy (2180), Ahmad (05/218), Ibn Abiy ´Aaswim (76) na Ibn Hibbaan (6702). Ni Swahiyh kwa mujibu wa Ibn Hajar katika “al-Iswaabah” (04/216).

[8] 43:87

[9] 39:03

[10] 10:18

[11] 74:48

[12] 40:18

[13] 05:117

[14] 53:19-20

[15] 98:05

[16] 17:23

[17] 39:02

[18] 22:34

[19] 08:39

[20] 02:217

[21] 64:16

[22] 08:39

[23] 09:41

[24] 61:10-11

[25] 07:138

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Qawaa´id al-Arba´ah, uk. 19-24
  • Imechapishwa: 23/03/2023