06. Msimamo wa Maswahabah na Taabi´uun juu ya Sunnah

Kuna bibi alikuja kwa as-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ´anh) akimuomba mirathi yake ambapo akamwambia: “Hakuna katika Qur-aan kitu chochote juu ya hilo na sijui kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekuhukumia kitu.” Lakini hata hivyo akamwambia kuwa atawauliza watu. Alipofanya hivo (Radhiya Allaahu ´anh) akaambiwa na baadhi yao kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimpa bibi 1/6 ambapo (Radhiya Allaahu ´anh) akawa amempa fungu lake.

´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) alikuwa akiwausia wafanya kazi wake wawahukumu watu kwa Qur-aan, wasipopata hukumu katika Qur-aan wahukumu kwa Sunnah. Pindi walipotatizika kuhusu kipomoko cha mwanamke kilichokufa kwa sababu ya kushambuliwa na mtu, akawauliza Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) hukumu ya hilo ambapo Muhammad bin Salamah na al-Mughiyrah bin Shu´bah (Radhiya Allaahu ´anhumaa) wakashuhudia mbele yake kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alihukumu kutolewe mtumwa aliye bora kabsia au kijakazi ambapo (Radhiya Allaahu ´anhum) akawa amemuhukumia hivo.

Pindi ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) alipotatizika kuhusu mwanamke kukaa eda nyumbani kwake baada ya kufariki mume wake akaelezwa na Furay´ah bint Maalik bin Sinaan, ambaye alikuwa ni dadake Abu Sa´iyd (Radhiya Allaahu ´anhumaa), ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) baada ya kufariki mume wake alimwamrisha kubaki nyumbani kwake mpaka muda wa eda uishe ambapo (Radhiya Allaahu ´anh) akawa amehukumu hivo. Kadhalika alihukumu kwa kutumia Sunnah kwa kumsimamishia adhabu ya kunywa pombe al-Waliyd bin ´Uqbah.

Pindi ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) alipofikiwa na khabari kuwa ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) anakataza hajj Tamattu´ ndipo ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) akafanya hajj na ´umrah pamoja na kusema kwamba hawezi kuacha Sunnah ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa maneno ya mtu yeyote.

Pindi baadhi ya watu walipopingana na Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) juu ya hajj Tamattu´ kwa sababu ya maoni ya Abu Bakr na ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) waliokuwa wanaonelea kufanya hajj peke yake alisema Ibn ´Abbaas:

“Mnakaribiwa kuangukiwa na mawe kutoka mbinguni! Nawaambieni aliyosema Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na nyinyi mnanambia aliyosema Abu Bakr na ´Umar?”

Ikiwa yule ambaye anakwenda kinyume na Sunnah kwa sababu ya maneno ya Abu Bakr na ´Umar kunachelea juu yake kuadhibiwa, tusemeje hali ya mwenye kwenda kinyume navyo [Qur-aan na Sunnah] kwa sababu ya ambao ni duni kuliko wao [Abu Bakr na ´Umar] au kwa sababu tu ya maoni na Ijtihaad yake?

Pindi baadhi ya watu walipovutana na ´Abdullaah bin ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) katika baadhi ya Sunnah aliwaambia:

“Je, sisi tumeamrishwa kumfuata ´Umar au kufuata Sunnah?”

Wakati ´Imraan bin Huswayn (Radhiya Allaahu ´anhumaa) alipokuwa anamweleza mtu kuhusu Sunnah ambapo akamwambia amweleze kuhusu Qur-aan, ´Imraan (Radhiya Allaahu ´anh) alikasirika na kumwambia:

“Sunnah ndio inaifasiri Qur-aan.”

Bila ya Sunnah tusingelijua kuwa dhuhr ni Rakaa´ nne, maghrib tatu, fajr mbili na tusingelijua ufafanuzi wa hukumu za zakaah na ufafanuzi wa hukumu zingine zilizotajwa na Sunnah na mapokezi kutoka kwa Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) katika kuziadhimisha Sunnah na uwajibu wa kuzitendea kazi na wakati huo huo kumtahadharisha yule mwenye kwenda kinyume nazo. Hayo yamepokelewa kwa wingi.

Katika hayo vilevile pindi ´Abdullaah bin ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa) alipokuwa anasimulia maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Msiwazuie wajakazi wa Allaah na misikiti ya Allaah.”

Mtoto wake mmoja akasema:

“Ninaapa kwa Allaah! Nitawazuia.”

´Abdullaah akamkasirikia na akamtukana vibaya sana na kumwambia:

“Mimi nakueleza alivyosema Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wewe unasema kuwa utawazuia?”

Wakati ´Abdullaah bin al-Mughaffal al-Muzaniy (Radhiya Allaahu ´anh), ambaye alikuwa ni Swahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), alipomuona ndugu yake mmoja anarusha jiwe akamkataza kufanya hivo na kumwambia:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekataza kurusha jiwe na kusema kuwa haliwindi viwindwa na wala halimuumizi adui. Bali linavunja jino na kutoa jicho nje.”

Baada ya hapo akamuona anarusha jiwe ambapo akamwambia:

“Ninaapa kwa Allaah! Sintokuzungumzisha kamwe. Nakukataza kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekataza kurusha jiwe kisha unarudi kufanya hivo?”

al-Bayhaqiy amesimulia kwamba Ayyuub as-Sikhtiyaaniy, ambaye alikuwa Taabiy´ mtukufu, amesema:

“Mtu akielezwa Sunnah kisha ukamsikia anasema ´tuacheni na mambo haya`, basi utambue kuwa ni mpotevu.”

al-Awzaa´iy (Rahimahu Allaah) amesema:

“Sunnah inaihukumu Qur-aan.”

Bi maana inayafungamanisha yale iliyoyataja kwa kuachia au inasimbulia yale ambayo hayakutajwa kwenye Qur-aan. Allaah (Subhaanah) amesema:

وَأَنزَلْنَا إِلَيْكَ الذِّكْرَ لِتُبَيِّنَ لِلنَّاسِ مَا نُزِّلَ إِلَيْهِمْ وَلَعَلَّهُمْ يَتَفَكَّرُونَ

“Tumekuteremshia Ukumbusho ili uwabainishie watu yaliyoteremshwa kwao na huenda wakapata kuzingatia.” (16:44)

Vilevile imetangulia kuwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Tanabahini! Hakika mimi nimepewa Kitabu na kingine mfano wake.”

al-Bayhaqiy amepokea kutoka kwa ´Aamir ash-Sha´biy (Rahimahu Allaah) kuwa siku moja aliwaambia baadhi ya watu:

“Mmeangamia pale mlipoacha mapokezi.”

Akimaanisha Hadiyth Swahiyh.

al-Bayhaqiy amepokea tena kutoka kwa al-Awzaa´iy (Rahimahu Allaah) kwamba siku moja aliwaambia baadhi ya marafiki zake:

“Utapofikiwa na Hadiyth kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tahadhari na kuonelea kinyume. Kwani hakika Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa ni mfikishaji kutoka kwa Allaah.”

al-Bayhaqiy amesimulia vilevile kutoka kwa mtukufu Imaam Sufyaan ath-Thawriy (Rahimahu Allaah) kwamba amesema:

“Elimu nzima ni kuwa na utambuzi juu ya mapokezi.”

Maalik bin Anas (Rahimahu Allaah) amesema:

“Hakuna katika sisi yeyote isipokuwa anarudi na kurudiwa isipokuwa mtu mwenye kaburi hili.”

kisha akaashiria kaburi la Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Abu Haniyfah (Rahimahu Allaah) amesema:

“Inapokuja Hadiyth kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tunaikubali na kuitendea kazi.

ash-Shaafi´iy (Rahimahu Allaah) amesema:

“Nitapoona Hadiyth Swahiyh kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) halafu nisiitendee kazi, basi nakushuhudisheni kuwa akili yangu imenitoka.”

Amesema (Rahimahu Allaha) tena:

“Nitaposema maoni na kukaja Hadiyth kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tofauti na vile nilivyosema, yatupeni maoni yangu ukutani.”

Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) alisema kuwaambia baadhi ya marafiki zake:

“Msinifuate kichwa mchunga mimi, wala Maalik wala ash-Shaafi´iy. Chukueni pale tunapochukua.”

Amesema (Rahimahu Allaha) tena:

“Nashangazwa na watu wanaojua mlolongo wa wapokezi na kusihi kwake kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kisha wanaenda kwenye maoni ya Sufyaan. Allaah (Subhaanah) anasema:

فَلْيَحْذَرِ الَّذِينَ يُخَالِفُونَ عَنْ أَمْرِهِ أَن تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“Watahadhari wale wanaokhalifu amri yake, isije ikawapata fitnah au ikawasibu adhabu iumizayo.” (24:63)

Kisha akasema:

“Hivi mnajua nini fitnah? Fitnah ni shirki. Huenda pale ataporudisha baadhi ya maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaingiwa moyoni mwake na kitu katika upindaji na hatimaye akaangamia.”

al-Bayhaqiy amepokea kutoka kwa Mujaahid bin Jabr, ambaye ni Taabiy´ mtukufu, ya kwamba amesema pindi alipokuwa akifasiri maneno Yake (Subhaanah):

فَإِن تَنَازَعْتُمْ فِي شَيْءٍ فَرُدُّوهُ إِلَى اللَّـهِ وَالرَّسُولِ

“Mkizozana katika jambo basi lirudisheni kwa Allaah na Mtume.” (04:59)

“Kurudi kwa Allaah ina maana kurudi katika Kitabu Chake. Kurudi kwa Mtume ina maana kurudi katika Sunnah.”

al-Bayhaqiy amepokea vilevile kutoka kwa az-Zuhriy (Rahimahu Allaah) ya kwamba amesema:

“Wanachuoni wetu waliotangulia walikuwa wakisema ´kushikamana na Sunnah ndio kufaulu´.”

Muwaffaq-ud-Diyn Ibn Qudaamah (Rahimahu Allaah) katika kitabu chake “Rawdhwat-un-Naadhwiriy” alipokuwa akibainisha misingi ya hukumu amesema yafuatayo:

Msingi wa pili wa dalili ni Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Maneno ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni dalili kutokana na ushahidi wa miujiza yake na kwa kuwa Allaah ameamrisha kumtii na vilevile akakataza kwenda kinyume na amri yake.”

Haafidhw Ibn Kathiyr (Rahimahu Allaah) amesema pindi alipokuwa akifasiri maneno Yake (Ta´ala):

لَّا تَجْعَلُوا دُعَاءَ الرَّسُولِ بَيْنَكُمْ كَدُعَاءِ بَعْضِكُم بَعْضًا ۚ قَدْ يَعْلَمُ اللَّـهُ الَّذِينَ يَتَسَلَّلُونَ مِنكُمْ لِوَاذًا ۚ فَلْيَحْذَرِ الَّذِينَ يُخَالِفُونَ عَنْ أَمْرِهِ أَن تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“Msifanye kumwita Mtume baina yenu ni kama mnavyoitana nyinyi kwa nyinyi. Hakika Allaah anawajua wale wanaoondoka kwa kunyemelea miongoni mwenu. Hivyo basi, watahadhari wale wanaokhalifu amri yake, isije ikawapata fitnah au ikawasibu adhabu iumizayo.” (24:63)

“Juu ya amri ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambayo ni njia, mfumo, mwenendo, Sunnah na Shari´ah yake. Maneno na vitendo vinatakiwa kupimwa kwa maneno na matendo yake; yatakayoafikiana navyo yatakubaliwa na yatakayovikhalifu atarudishiwa mwenye nayo yeyote awaye. Imethibiti al-Bukhaariy, Muslim na wengineo kusimulia ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Atayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu kitarudishwa.”

Bi maana aogope na atahadhari yule mwenye kwenda kinyume na Shari´ah ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa ndani na kwa nje.

أَن تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ

“… isije ikawapata fitnah… “

Kwenye mioyo yao katika kufuru, unafiki au Bid´ah.

أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“… au ikawasibu adhabu iumizayo.”

Bi maana duniani kwa kuuawa, kuadhibiwa, kutiwa jela na mengineyo.

Imaam Ahmad amepokea: amenihadithia ´Abdur-Razzaaq: amenihadithia Ma´mar, kutoka kwa Hammaam bin Munabbih aliyesema: Abu Hurayrah amenieleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mfano wangu na nyinyi ni kama wa mtu aliyekonga moto. Ulipoangaza vilivyoko pembezoni mwake ikawa vipepeo na wadudu wanavutikiwa na moto ule na hivyo kuanza kutumbukia ndani yake. Akawa anajaribu kuwazuia lakini hata hivyo wanamshinda na hatimaye wanatumbukia ndani. Huu ndio mfano wangu mimi na nyinyi ambapo najaribu kukuzuieni na Moto lakini hata hivyo mnanishinda na kutumbukia ndani yake.”

as-Suyuutwiy (Rahimahu Allaah) katika kijitabu chake kwa jina “Miftaah-ul-Jannah fiy al-Ihtijaaj bis-Sunnah” amesema yafuatayo:

“Tambua, Allaah akurehemu, kwamba yule mwenye kupinga Hadiyth ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) – sawa iwe ni maneno au vitendo kwa kuzingatia yale masharti yake yanayojulikana katika misingi kuwa ni hoja – anakufuru na kutoka katika Uislamu na atafufuliwa pamoja na mayahudi na manaswara au pamoja na wale anaowataka Allaah katika mapote ya kikafiri.”

Mapokezi kutoka kwa Maswahabah, Taabi´uun na wanachuoni waliokuja baada yao juu ya kuadhimisha Sunnah, uwajibu wa kuitendea kazi na matahadharisho kwa yule mwenye kwenda kinyume nayo ni mengi sana. Nataraji zile Aayah, Hadiyth na mapokezi tuliyoyataja ni yenye kutosheleza na kumkinaisha yule mwenye kutafuta haki.

Tunamuomba Allaah sisi na waislamu wengine wote atuwafikishe kwa yale anayoyaridhia, atusalimishe kutokamana na sababu zinazopelekea katika ghadhabu Zake na atuongoze sisi sote katika njia iliyonyooka. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia na yukaribu.

Swalah na salaam zimwendee mja na Mtume Wake; Mtume wetu Muhammad, kizazi chake, Maswahabah wake na wale wataowafuata kwa wema.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ujuwb-ul-´Amal bis-Sunnah
  • Imechapishwa: 23/10/2016