2- Muslim amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mambo mawili kwa watu ni kufuru; kutukaniana nasabu na kuomboleza juu ya maiti.”[1]

Bi maana sifa mbili. Watu wanaingia watu wote mpaka waislamu. Wako waislamu wenye sifa za kipindi cha kikafiri na sifa za kufuru zisizowatoa nje ya Uislamu.

Kufuru kusudiwa ni aina ndogo. Kufuru inapotajwa kwa fomu isiyotambulika kunakusudiwa ile aina ndogo. Kufuru inapotajwa kwa fomu ya kihakika kunakusudiwa ile aina kubwa. Mfano wa hilo ni pale (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliposema:

“Baina ya mtu na shirki na kufuru ni kuacha swalah.”[2]

Haina maana kwamba kila mtu mwenye sifa ya kufuru basi anakuwa ni kafiri. Katika hali hii anakuwa na sifa moja wapo miongoni mwa sifa za kufuru. Kadhalika kuhusiana na unafiki;  haina maana kwamba kila mtu mwenye sifa ya unafiki basi anakuwa ni mnafiki. Katika hali hii anakuwa na sifa moja wapo miongoni mwa sifa za unafiki.

Sifa ya kwanza ni kutukaniana nasabu. Tayari kumekwishatangulia maelezo juu ya hilo katika mlango wa uliotangulia.

Sifa ya pili ni kuomboleza juu ya maiti. Kuomboleza maana yake ni mtu kuonyesha mahuzuniko waziwazi kwa kufiliwa. Hivo ndivo watu wa kipindi cha kikafiri walivyokuwa wanafanya. Kilicho cha wajibu ni kwamba mtu anatakiwa kufanya subira wakati wa kufariki kwa ndugu na wapenzi. Hata hivo hiyo haina maana kwamba mtu asihisi maumivu na kulia. Kulia hakukatazwi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alilia wakati alipofariki mtoto wake Ibraahiym na akasema:

“Macho yanatokwa na machozi na moyo unahuzunika na hatusemi isipokuwa yale yenye kumridhisha Mola wetu. Hakika ni wenye kuhuzunika kwa kutengana na wewe Ibraahiym.”[3]

Kufanya hivi ni katika kuwa na huruma na ni kitu ambacho mtu hawezi kukizuia.

Aayah inafahamisha kuwa kuwa na subira na kuridhia ni katika sifa za imani. Hadiyth inafahamisha kwamba kuonyesha mahuzuniko waziwazi ni katika sifa za kufuru. Ni mambo mawili yaliyo kinyume moja kwa jengine.

[1] Muslim (67).

[2] Muslim (82).

[3] al-Bukhaariy (1303), Muslim (2315) na Ahmad (13014) kupitia kwa Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: I´aanat-ul-Mustafiyd bi Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 433-434
  • Imechapishwa: 14/08/2019