05. Madhehebu ya Salaf ndio sahihi na kuwaraddi wanaosema kuwa madhehebu ya waliokuja nyuma ndio wajuzi na wenye hekima zaidi kuliko madhehebu ya Salaf

Tumetangulia kubainisha mfumo wa Salaf na kutoa dalili za uwajibu wa kushikamana nayo. Hapa tunataka kuthibitisha kuwa madhehebu ya Salaf ndio mfumo sahihi. Hilo ni kwa njia mbili:

Ya kwanza: Mfumo wa Salaf umethibitishwa na Qur-aan na Sunnah. Yule ambaye atafuatilia mfumo wao kwa elimu na uadilifu, ataona kuwa unaenda sambamba na Qur-aan na Sunnah kikamilifu. Ni lazima iwe hivyo. Kwa sababu Allaah (Ta´ala) ameteremsha Qur-aan ili watu waweze kuzitafakari Aayah zake na kuzitendea kazi inapohusiana na hukumu na kuzisadikisha ikiwa zinahusiana na maelezo. Ni jambo lisilokuwa na shaka ya kwamba Salaf ndio wenye kuzielewa, kuzisadikisha na kuzitendea kazi bora zaidi. Haya kwa sababu imeteremshwa kwa lugha yao na katika kipindi chao. Ndio maana haishangazi wakawa wao ndio wajuzi na matendo yao yakawa bora zaidi.

Ya pili: Haki katika suala hili ima iko kwa Salaf au kwa wale waliokuja nyuma. Chaguo la pili ni batili kwa sababu itakuwa na maana ya kwamba Allaah, Mtume Wake na wale wa awali waliotangulia kati ya al-Muhaajiruun na al-Answaar walizungumza kwa batili kwa wazi au angalau kwa uchache kidhahiri. Hawakupatapo hata mara moja kuzungumza kwa haki ambayo ni wajibu kuiamini, si kwa wazi wala kwa dhahiri. Hivyo ina maana uwepo wa maandiko ya Qur-aan na Sunnah ni madhara matupu katika msingi wa dini. Katika hali hii itakuwa ni bora zaidi kuwaacha watu bila ya Kitabu na Sunnah. Hili bila ya shaka ni batili.

Baadhi ya wapumbavu wamesema kuwa mfumo wa Salaf umesalimika zaidi na mfumo wa waliokuja nyuma ni wajuzi na wenye hekima zaidi. Chimbuko ya matamshi haya ni mambo mawili:

Ya kwanza: Mtu anafikiria, kutokana na utata batilifu alionao, ya kwamba Allaah hasifiwi kwa sifa zozote za kihakika ambazo zimefahamishwa na Quraan na Sunnah.

Ya pili: Anafikiria kwamba mfumo wa Salaf ni kuamini maandiko yanayozungumzia Sifa pasi na kuthibitisha maana yake. Hivyo suala hili linakuwa ni lenye kuzunguka kati ya kuamini maandiko pasi na maana, jambo ambalo anafikiria kuwa ndio mfumo wa Salaf, au pia mtu akayathibitishia maandiko maana inayopingana na udhahiri wa dalili, mfumo ambao ndio wa wale waliokuja nyuma. Ni jambo lisilokuwa na shaka ya kwamba ni ujuzi na hekima zaidi kuthibitisha maana ya maandiko kuliko kuyaamini bila ya maana yoyote. Ndio maana mpumbavu huyu amefadhilisha mfumo wa waliokuja nyuma kwa ujuzi na hekima zaidi kuliko mfumo wa Salaf.

Maneno ya mpumbavu huyu ndani yake kuna haki na batili. Kuhusu haki, inapatikana katika maneno yake “Mfumo wa Salaf umesalimika zaidi”. Ama batili, inapatikana katika maneno yake “Mfumo wa waliokuja baada yao ni mjuzi na wenye hekima zaidi”. Ni batili kutokana na sababu mbili:

Ya kwanza: Maneno yake yanapingana na “Mfumo wa Salaf umesalimika zaidi”. Kule mfumo wa Salaf kuwa umesalimika zaidi hilo linalazimisha pia uwe mjuzi na wenye hekima zaidi. Hakuna usalama usiokuwa na elimu na hekima. Ni lazima kwa mtu awe na elimu ili kufikia usalama na ni lazima kwa mtu awe na hekima ili ajue ataenda namna gani ili afikie sababu hizo. Hivyo inabainika kuwa mfumo wa Salaf ndio ulio salama, mjuzi na wenye hekima zaidi. Hili mpumbavu huyu hana namna ya kulikwepa.

Ya pili: Kufikiria kwake kuwa Maandiko hayathibitishi sifa yoyote ile ya kihakika kwa Allaah ni batili. Ni batili kwa sababu kumejengeka juu ya utata batili na kwa sababu sifa za Allaah (Ta´ala) kamilifu zimethibitishwa kwa akili, hisia, maumbile na Shari´ah.

Kuhusiana na akili, kila kitu kilichopo ni lazima kiwe na sifa. Sifa hii inaweza kuwa ima kamilifu au yenye mapungufu. Chaguo hili la pili Allaah (Ta´ala) hawezi kusifika nalo kwa sababu Yeye Mola ni mkamilifu ambaye anastahiki kuabudiwa. Kwa ajili hiyo ndio maana Allaah (Ta´ala) ametolea dalili ubatilifu wa ´ibaadah wanayofanyiwa masanamu kwa kuwa na sifa zenye mapungufu na zisizokuwa na uwezo. Mfano wa sifa hizi ni kuwa hayasikii, hayaoni, hayanufaishi, hayadhuru, hayaumbi wala hayanusuru. Chaguo hili la pili likibatilika, kunathibiti lile la kwanza la kuthibitisha sifa kamilifu kwa Allaah.

Vilevile imethibiti kupitia hisia na ushuhuda ya kwamba viumbe nao wana sifa kamilifu. Sifa hizi wamezipata kutoka kwa Allaah (Subhaanah) – Yule mwenye kutunuku ukamilifu Yeye ana haki zaidi ya kuwa nao.

Kuhusiana na maumbile, mioyo iliosalimika imeumbwa kwa njia ya kumpenda, kumuadhimisha na kumuabudu Allaah. Je, utampenda, utamuadhimisha na kumuabudu mwengine isipokuwa Yule ambaye unajua kuwa anasifika na sifa kamilifu zenye kulingana na uola na uungu Wake?

Ama kuhusu Shari´ah, dalili ziko nyingi. Kwa mfano Allaah (Ta´ala) anasema:

هُوَ اللَّهُ الَّذِي لا إِلَهَ إِلَّا هُوَ عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ هُوَ الرَّحْمَنُ الرَّحِيمُ* هُوَ اللَّهُ الَّذِي لا إِلَهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلامُ الْمُؤْمِنُ الْمُهَيْمِنُ الْعَزِيزُ الْجَبَّارُ الْمُتَكَبِّرُ سُبْحَانَ اللَّهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ* هُوَ اللَّهُ الْخَالِقُ الْبَارِئُ الْمُصَوِّرُ لَهُ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَى يُسَبِّحُ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ

“Yeye ni Allaah; ambaye hakuna mungu wa haki isipokuwa Yeye. Anayajua ya ghaibu na ya dhahiri, Yeye ni Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu. Yeye ni Allaah ambaye hakuna mungu wa haki isipokuwa Yeye; Mfalme, Mtakatifu, Mwenye amani, Mwenye kusadikisha, Mwenye kutawala na kuendesha, Mwenye nguvu kabisa zisizoshindikana Mwenye kustahiki kiburi – Utakasifu ni wa Allaa kwa yale yote wanayomshirikisha nayo. Yeye ni Allaah; Muumbaji, Mwanzishi viumbe bila kasoro, Mtengeneza sura, ana Majina mazuri kabisa, kinamtukuza pekee kila kilichokuweko katika mbingu na ardhi – Naye ni Mwenye nguvu kabisa zisizoshindikana, Mwenye hekima.”[1]

وَلَهُ الْمَثَلُ الأَعْلَى فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ

“Naye ni Mwenye wasifu wa juu katika mbingu na ardhi.[2]

اللَّهُ لا إِلَهَ إِلَّا هُوَ الْحَيُّ الْقَيُّومُ لا تَأْخُذُهُ سِنَةٌ وَلا نَوْمٌ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ مَنْ ذَا الَّذِي يَشْفَعُ عِنْدَهُ إِلاَّ بِإِذْنِهِ يَعْلَمُ مَا بَيْنَ أَيْدِيهِمْ وَمَا خَلْفَهُمْ وَلا يُحِيطُونَ بِشَيْءٍ مِنْ عِلْمِهِ إِلاَّ بِمَا شَاءَ وَسِعَ كُرْسِيُّهُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَلا يَؤُودُهُ حِفْظُهُمَا وَهُوَ الْعَلِيُّ الْعَظِيمُ

”Allaah, hakuna mungu wa haki isipokuwa Yeye – Aliyehai daima, Msimamizi wa kila kitu. Haumchukuwi usingizi wala kulala. Ni Vyake pekee vilivyomo katika mbingu na vilivyomo katika ardhi. Nani huyu ambaye anashufai [anayeombea] mbele Yake bila ya idhini Yake? Anajua yaliyo mbele yao [viumbe] na yaliyo nyuma yao. Wala hawakizunguki chochote kile katika elimu Yake isipokuwa kwa alitakalo. Kursiy Yake imeenea mbingu na ardhi. Wala hakumchoshi kuvihifadhi viwili hivyo. Na Yeye ndiye aliye juu, na ndiye mkuu.”[3]

Vilevile Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Enyi watu! Zihurumieni nafsi zenu! Kwani hakika hamumuombi ambaye ni kiziwi wala asiyekuwepo. Hakika Yule mnayemwomba ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona na Aliye karibu. Hakika yule mnayemwomba Yuko karibu na mmoja wenu kuliko shingo ya mpando wenu.”[4]

Kuna Aayah na Hadiyth nyingi mfano wa hizo.

Ya tatu: Kufikiria kwake ya kwamba Salaf walikuwa wakiamini tu maandiko bila ya kuthibitisha maana yake, ni I´tiqaad batili na ni uongo juu ya Salaf. Salaf walikuwa ndio wajuzi zaidi katika Ummah kwa kutambua maandiko kuhusu sifa ni mamoja kimatamshi na kimaana. Isitoshe hakuna yeyote aliyethibitisha maana ya sifa inayolingana na Allaah kwa njia ile aliyoikusudia Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kama walivyofanya Salaf.

Ya nne: Salaf ndio walikuwa warithi wa Manabii na Mitume. Walichukua elimu yao kutoka kwenye chemchem ya Ujumbe wa kiungu na imani ya kweli. Upande mwingine waliokuja baada yao walichukua elimu yao kutoka kwa waabudu moto, washirikina na wapotevu wa mayahudi na wagiriki. Ni vipi basi vizazi vya waabudu moto, washirikina, mayahudi, wagiriki na vifaranga vyao watakuwa ni wajuzi na wenye hekima zaidi katika majina na sifa za Allaah kuliko warithi wa Mitume?

Ya tano: Watu hawa waliokuja nyuma, ambao mpumbavu huyu amewafadhilisha kwamba ni wajuzi na wenye hekima zaidi kuliko Salaf, walikuwa ni wenye kuchanganyikiwa kwa sababu ya kuupa kisogo ujumbe na uongofu ambao Allaah amemtuma kwao Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Walitafuta elimu yao kuhusu Allaah (Ta´ala) kutoka kwa watu ambao wao wenyewe hawamtambui. Haya yameshuhudiwa na wao wenyewe na Ummah. ar-Raaziy, ambaye ni mmoja katika viongozi wao, amebainisha namna ambavyo mambo yao yalivyoishilia na kusema:

“Mwisho wa akili ni maangamivu

Jitihada za viumbe wengi ni bure

Roho zetu zimetelekezwa katika viwiliwili vyetu

Mwisho wa dunia yetu ni mabalaa na adhabu

Wakati wa uhai wetu wote hatukufaidika lolote katika utafiti wetu

Isipokuwa tumekusanya porojo tu.”

Baada ya hapo akasema:

“Nimetafakari mifumo inayofuatwa na wanafalsafa na kuona kuwa haifidishi lolote. Nimekuta mfumo ulio karibu zaidi ni mfumo wa Qur-aan. Soma kuhusu kuthibitisha:

الرَّحْمَنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَى

“Mwingi wa Rahmah amelingana juu ya ´Arshi.”[5]

إِلَيْهِ يَصْعَدُ الْكَلِمُ الطَّيِّبُ وَالْعَمَلُ الصَّالِحُ يَرْفَعُهُ

 “Kwake Yeye linapanda neno zuri na kitendo chema hukinyanyua.”[6]

Soma kuhusu kukanusha:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[7]

وَلا يُحِيطُونَ بِهِ عِلْماً

“Na wala wao hawawezi kuzunguka elimu Yake.”[8]

Mwenye kukutana na niliyokutana nayo, ataelewa nilichokielewa.”[9]

Ni vipi basi mfumo wa watu hawa wenye kuchanganyikiwa ambao wao wenyewe wamekubali kuwa ni wapotevu na wamechanganyikiwa utakuwa mjuzi na wenye hekima zaidi kuliko mfumo wa Salaf? Salaf wao walikuwa ni maimamu wa uongofu na taa zenye kungaa. Allaah aliwapa elimu yenye kuwashinda wafuasi wengine wa Mitume. Walifahamu uhakika wa imani na elimu kiasi cha kwamba, lau mtu huyu angelipata yale yote ambayo walipata waliokuja baada yao, basi angelistahi kuwalinganisha na Salaf seuze kudai kwamba ni bora kuliko wao. Kwa haya inapata kubainika kuwa mfumo wa Salaf ndio ulio salama, mjuzi na wenye hekima zaidi.

[1] 59:22-24

[2] 30:27

[3] 02:255

[4] al-Bukhaariy (2992).

[5] 20:05

[6] 35:10

[7] 42:11

[8] 20:110

[9] Tazama ”Majmuu´-ul-Fataawaa” (5/11).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fath Rabb-il-Bariyyah, uk. 23-29
  • Imechapishwa: 07/01/2020