12- Hali ilipokuwa kwa watu wengi katika zama hizi ni kuzua katika dini yao – na khaswakhaswa inapokuja katika masuala yaliyofungamana na mazishi – basi ikawa ni wajibu muislamu aache anausia aandaliwe na kuzikwa kwa mujibu wa Sunnah. Hilo ni kwa kutendea kazi maneno Yake (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا قُوا أَنفُسَكُمْ وَأَهْلِيكُمْ نَارًا وَقُودُهَا النَّاسُ وَالْحِجَارَةُ عَلَيْهَا مَلَائِكَةٌ غِلَاظٌ شِدَادٌ لَّا يَعْصُونَ اللَّـهَ مَا أَمَرَهُمْ وَيَفْعَلُونَ مَا يُؤْمَرُونَ

“Enyi walioamini! Zilindeni nafsi zenu na ahli zenu na Moto ambao kuni zake ni watu na mawe, juu yake wako Malaika washupavu hawana huruma, wakali, hawamuasi Allaah kwa yale anayowaamrisha na wanafanya yale wanayoamrishwa.”[1]

Kwa ajili hiyo Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walikuwa wakiusia juu ya hilo. Mapokezi kutoka kwao kutokana na tuliyoyataja ni mengi. Hapana ubaya kutaja baadhi yake:

1- ´Aamir bin Sa´d bin Abiy Waqqaas amesimulia kwamba baba yake alisema wakati wa maradhi yake aliyofikia juu yake:

“Nifanyieni mwanandani aina ya Lahd na nipangieni matofali ya udongo juu yangu, kama alivofanyiwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”

Ameipokea Muslim, al-Bayhaqiy (03/407) na wengineo.

2- Abu Burdah amesimulia:

“Abu Muusa aliacha anausia wakati alipofikiwa na ishara ya kutaka kufa akasema: “Mtapoondoka mkiwa mmebeba mwili wangu basi kazeni mwendo na wala msinisindikize hali ya kuwa mmewasha moto, msiweke juu ya mwanandani wangu chochote kitachozuia baina yangu mimi na uongo na wala msitengeneze juu ya kaburi langu lengo. Nakushuhudisheni ya kwamba mimi niko mbali kabisa na kila mwanamke atakayenyoa nywele zake, atayeinua sauti yake au atayerarua nguo zake.” Wakasema: “Ulisikia chochote kuhusu hayo?” Akajibu: “Ndio, kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”

Ameipokea Ahmad (04/395) kwa utimilifu huu na Ibn Maajah kwa cheni ya wapokezi nzuri.

3- Hudhayfah ameeleza:

“Nitapokufa basi msitangazie juu yangu yeyote. Kwani mimi nachelea isije kuwa Na´y. Mimi nimemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akikataza Na´y.”

Ameipokea at-Tirmidhiy (02/129) ambaye amesema:

“Hadiyth ni nzuri.”

Wengine wamepokea mfano wake na itakuja katika “an-Na´y´”. Katika mlango huu kuna mapokezi mengine yatayokuja katika masuala ya 47. Kutokana na yaliyotangulia an-Nawawiy (Rahimahu Allaah) amesema katika “al-Adhkaar”:

“Inapendekezwa kwake kwa njia ya mapendekezo yaliyokokotezwa aache anawausia kujiepusha na zile Bid´ah za maziko zilizozoeleka kikawaida na asisitize juu ya hilo.”

[1] 66:06

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz wa Bid´ahaa, uk. 08-09
  • Imechapishwa: 19/12/2019