05. Injili inatoa bishara njema juu ya utume wa Muhammad

“15Ikiwa mnanipenda basi shikamaneni na maamrisho yangu. 16Nami nitamuomba Baba, naye atawapa msaidizi mwingine, ili awe pamoja nanyi milele.”[1]

Wanachuoni wa Uislamu wanasema kuwa huyu msaidizi mwingine ni Muhammad Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kubaki pamoja nao milele maana yake ni kubaki Shari´ah na Kitabu chake alichoteremshiwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kitachobaki milele.

“26Pindi atapokuja huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye atakuja kutoka kwa Baba, atanishuhudilia. 27Nanyi mtamshuhudilia, kwa sababu nyinyi mlikuwa pamoja nami tangu hapo mwanzo.”[2]

“Sikuwaambia hayo tangu mwanzo, kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi. 5Ama hivi sasa mimi naenda zangu kwa yule aliyenituma, wala hakuna yeyote katika nyinyi aniulizaye: Unakwenda wapi? 6ila kwa sababu nimewaambieni hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu. 7Lakini mimi nawaambieni ukweli: ni wema kwenu mimi niondoke. Kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatokujieni. Lakini mimi nikienda zangu basi nitakutumieni naye, 8naye pindi atapokuja, atauonyesha ulimwengu dhambi na haki na hukumu ni kitu gani.”[3]

“12Hakika mimi bado nina mengi ya kukwelezeni, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. 13Lakini pale atakapokujieni, huyo Roho wa kweli, basi atakuongozeni katika ukweli wote; kwa maana hatoongea kutoka kwake mwenyewe, bali atafikisha yale yote anayosikia na kukujuzeni mambo yanayokuja. 14Yeye atanitukuza mimi, kwa kuwa atachukua katika yaliyo yangu na kuwajuzeni nayo.”[4]

“16Baada ya muda kidogo hamtoniona, na baada ya muda kidogo mtaniona tena.” 17Ndipo baadhi ya wanafunzi wake wakasema: “Anamaanisha nini anaposema: ´Baada ya muda kidogo hamtoniona, na baada ya muda kidogo mtaniona tena´, na pale anaposema: ´Mimi naenda kwa Baba´?”[5]

Wanachuoni wa Uislamu wanasema kuwa sifa hizi zilizotajwa na Masihi juu ya atayechukua nafasi yake baada yake hazikukusanyika kwa mwengine isipokuwa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Mtume huyu ambaye Masihi alimtolea bishara njema ndani ya Injili alikuwa akiitwa “Paaraklet”. Namna zama zilivyokuwa zinaenda wafasiri waliokuja nyuma wakalifuta na kulibadilisha kwa “Roho wa kweli, msaidizi na roho Mtakatifu. Paaraklet ni neno la kigiriki na maana yake ni “mwenye kuhimidiwa sana”, ambalo ndio maana ya neno Muhammad.

[1] Yohana 14:15-16

[2] Yohana 15:26-27

[3] Yohana 16:05-08

[4] Yohana 16:12-13

[5] Yohana 16:16-17

  • Mhusika: ´Allaamah Muhammad Taqiyy-ud-Diyn al-Hilaaliy al-Maghribiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Baraahiyn al-Injiylyyah ´alaa anna ´Iysaa daakhil fiyl-´Ubuudiyyah wa la hadhdhwa lahu fiyl-Uluuhiyyah, uk. 17-18
  • Imechapishwa: 16/10/2016