Swali: Wako wanaosema kuwa imechukizwa kwa wanawake kuyatembelea makaburi kutokana na Hadiyth ya Umm ´Atwiyyah. Kutokana na hilo ndio yanafasiriwa maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Allaah amewalaani wanawake wenye kuyatembelea makaburi.”[1]

Mbali na kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na makaburi ya marafiki zake wawili (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ambayo imesuniwa kwa wanamme na wanawake kuyatembelea. Hayo ni kutokana kuenea kwa dalili ambazo ameomba atembelewa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Ni dalili zipo hizo? Ni yepi maoni yako juu ya masuala haya kwa ujumla?

Jibu: Imethibiti kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba amewalaani wanawake wenye kuyatembelea makaburi. Hayo yamethibiti kutoka katika Hadiyth ya Ibn ´Abbaas, Abu Hurayrah, Hassaan bin Thaabit al-Answaariy. Wanazuoni wakachukua kutoka katika hayo kwamba matembezi ya wanawake yameharamishwa. Kwa sababu laana haiwi isipokuwa kwa kitu ambacho ni haramu. Bali inafahamisha kwamba ni miongoni mwa madhambi makubwa. Kwa sababu wanazuoni wametaja kuwa maasi yalioambatanishwa na laana na matishio ya kuadhibiwa kwa Moto yanakuwa katika ile aina ya madhambi makubwa.

Kwa hiyo maoni ya sawa ni kwamba ni haramu kwa wanawake kuyatembelea makaburi na si jambo lililochukizwa peke yake. Sababu ya hilo – na Allaah ndiye mjuzi zaidi – ni kwamba wao mara nyingi wanakuwa wachache wa subira na ni wenye fitina. Hivyo wao kuyatembelea makaburi na kuyasindikiza majeneza kunaweza kuwafitinisha watu na kunaweza kusababisha matatizo kwa wanamme. Kwa hiyo ikawa ni katika huruma ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) kuwakataza kuyatembelea na akawaharamishia kuyatembelea makaburi kwa sababu ya kuziba njia ya wao kufitinisha au wakafitinishwa. Imesihi kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa amesema:

“Sijaacha baada yangu fitina yenye kuwadhuru zaidi wanamme kama wanawake.”[2]

Maneno ya baadhi ya wanazuoni ambapo wameona kuwa kunavuliwa katika hayo kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na makaburi ya marafiki zake wawili (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ni maoni yasiyokuwa na dalili. Usawa ni kwamba makatazo yanaenea makaburi yote mpaka kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na makaburi ya marafiki zake wawili (Radhiya Allaahu ´anhumaa). Haya ndio yenye kutegemewa upande wa dalili.

Kuhusu wanamme imependekezwa kwao kuyatembelea makaburi na kulitembelea kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na makaburi ya marafiki zake wawili. Lakini mtu afanye hivo pasi na kuyafungia safari. Sunnah ni kuyatembelea makaburi yaliyoko mjini mwa mtu pasi na kuyafungia safari. Kwa msemo mwingine haifai mtu akasafiri kwa ajili ya matembezi. Lakini mtu akiwa Madiynah basi atalitembelea kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), makaburi ya marafiki zake wawili, al-Baqiy´ na waliokuwa mashahidi.

Ama mtu kufunga safari kutokea mahali pa mbali kwa ajili ya matembezi peke yake, kitendo hichi hakifai kwa mujibu wa maoni sahihi ya wanazuoni. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kusifungwe safari isipokuwa kuelekea katika misikiti mitatu; msikiti Mtakatifu, msikiti huu na msikiti wa al-Aqswaa.”[3]

Lakini mtu akifunga safari kwa ajili ya kutembelea msikiti wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), basi matembezi yanaingia humo kwa kufuatia jambo hilo. Anapofika msikiti basi ataswali kile kiasi atakachoweza, kisha atalitembelea kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na makaburi ya marafiki zake wawili, atamwombea (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), atamswalia na kumtakia amani (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Baada ya hapo atamtolea salamu as-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ´anh) na kumwombea du´aa, kisha atamtolea salamu al-Faaruwq na kumwombea du´aa. Hivi ndio Sunnah. Vivyo hivyo katika makaburi mengine. Kwa mfano anatembelea Dameski, Cairo, Riyaadh au nchi yoyote basi imependekezwa kwake kuyatembelea makaburi kutokana na yale mazingatio yanayopatikana ndani yake. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yatembeleeni makaburi. Kwani hakika yanakukumbusheni Aakhirah.”[4]

Kwa hivyo ayatembelee kwa ajili ya ukumbusho, mazingatio, kuwaombea du´aa wafu na kuwaombea rehema. Hivi ndio Sunnah pasi na kuyafungia safari. Lakini asiwatembelee kwa ajili ya kuwaomba wao badala ya Allaah. Kuwaomba badala ya Allaah ni kumshirikisha Allaah (´Azza wa Jall). Kule kuwaomba, akawataka uokozi, akawachinjia, akajikurubisha kwao kwa kitu katika ´ibaadah au akawaomba msaada wa haraka ni mambo yasiyofaa. Mambo haya ni kumshirikisha Allaah (´Azza wa Jall). Kama ambavo haijuzu kwa masanamu, miti na mawe basi vivyo hivyo haijuzu kwa wafu. Kwa hiyo asiombe sanamu, asiliombe ulinzi, asiliombe uokozi na wala mti, jiwe na nyota. Vivyo hivyo watu waliyomo ndani ya makaburi haifai wakaombwa pamoja na Allaah, wasiombwe msaada na wala wasiombwe uokozi. Bali haya ni kumshirikisha Allaah (´Azza wa Jall). Amesema (Subhaanah):

وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّـهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا

“Hakika misikiti yote ni ya Allaah, hivyo basi msiombe yeyote pamoja na Allaah.”[5]

يُولِجُ اللَّيْلَ فِي النَّهَارِ وَيُولِجُ النَّهَارَ فِي اللَّيْلِ وَسَخَّرَ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ كُلٌّ يَجْرِي لِأَجَلٍ مُّسَمًّى ۚ ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ لَهُ الْمُلْكُ ۚ وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ مَا يَمْلِكُونَ مِن قِطْمِيرٍ إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ۚ وَلَا يُنَبِّئُكَ مِثْلُ خَبِيرٍ

“Anauingiza usiku ndani ya mchana na anauingiza mchana ndani ya usiku na anaitisha jua na mwezi; kila kimoja kinakwenda hadi muda maalum uliokadiriwa. Huyo ndiye Allaah, Mola wenu, ufalme ni Wake pekee.  Wale mnaowaomba badala Yake hawamiliki hata kijiwavu cha kokwa ya tende. Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu, na hata wakisikia, hawatakuitikieni na siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu na wala hakuna atakayekujulisha vyema kama Mwenye khabari zote za ndani.”[6]

Akabainisha (Subhaahah) kuwa kuwaomba wafu na mfano wake ni kumshirikisha (Subhaanah). Amesema (Subhaanah):

وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ

“… na siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu… “

Akafanya kuwa kuwaomba wafu na kuwataka uokozi waliyomo ndani ya makaburi ni kumshirikisha Yeye (´Azza wa Jall). Vivyo hivyo maneno Yake (Subhaanah):

وَمَن يَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ لَا بُرْهَانَ لَهُ بِهِ فَإِنَّمَا حِسَابُهُ عِندَ رَبِّهِ ۚ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الْكَافِرُونَ

“Yeyote yule anayeomba pamoja na Allaah mungu mwengine – hana ushahidi wa wazi juu ya hilo – basi hakika hesabu yake iko kwa Mola wake. Hakika hawafaulu makafiri.”[7]

Akaita kuwa kumwomba asiyekuwa Allaah ni ukafiri na akawahukumu watu wake ya kwamba ni makafiri na kwamba si wenye kufaulu. Kwa hivyo ni lazima kwa waislamu watahadhari na jambo hilo na ni lazima kwa wanazuoni wabainishe mambo haya ili watu watahadhari na kumshirikisha Allaah.

Wengi katika watu wa kawaida wanapopita kando na kaburi la mtu ambaye wanamtukuza wanamtaka uokozi na wanasema ´niokoe, niokoe, ee fulani au ee bwana fulani, niokoe, niokoe, ninusuru, mponye mgonjwa wangu`, hii ndio shirki kubwa. Mambo haya yanaombwa kutoka kwa Allaah; si kutoka kwa wafu, masanamu wala nyota. Ni mambo yanaombwa kutoka kwa Allaah (´Azza wa Jall). Kuhusu aliye hai anaombwa yale mambo anayoyaweza akiwa mbele yako na anayasikia maneno yako, kupitia njia ya uandishi, njia ya simu, njia ya faksi na mfano wazo miongoni mwa yale mambo yanayohisiwa. Hivyo mtu anaweza kumwomba yale mambo anayoyaweza kwa njia ya kwamba mtu akawasiliana naye, akamwandikia au akamzungumzisha kwa njia ya simu na akamwambia amkope kiwango fulani, amsaidie kujenga nyumba yake au kukarabati shamba lake. Kati yako wewe na yeye kukiwa kuna kitu katika kusaidiana kwa njia hii hapana vibaya.

Kuhusu kumwomba maiti au hata aliye hai mambo asiyoyaweza au aliyeko mbali pasi na njia za kuhisiwa ni shirki. Kwa sababu kumwomba asiyeko mbele yako pasi na zile njia zenye kuhisiwa maana yake ni kwamba unaamini kuwa anatambua, kwamba anasikia maombi yako hata ukiwa mbali, imani sampuli hii ni batili na ya kikafiri. Yeyote anayeona kuwa asiyekuwa Allaah anajua mambo yaliyofichana ni kufuru kubwa. Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

قُل لَّا يَعْلَمُ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ الْغَيْبَ إِلَّا اللَّـهُ

“Sema: “Hakuna katika mbingu na ardhi ajuaye yaliyofichikana isipokuwa Allaah.”[8]

Au ukaona kuwa Allaah amemjaalia siri katika ulimwengu kwa njia ya kwamba anauendesha; anampa amtakaye na anamnyima amtakaye – kama wanavofikiri baadhi ya wajinga – hii pia ni shirki kubwa.

Kuwatembelea wafu ni matembezi ya wema na ni matembezi ya kuwahurumia na kukumbuka Aakhirah na kujiandaa kwayo. Kumbuka kuwa utakufa kama walivokufa na hivyo ukajiandaa kwa ajili ya Aakhirah, ukawaombea ndugu zako waliokufa na hivyo ukawaombea rehema na msamaha. Hizi ndio faida za kuyatembelea; ndani yake kuna makumbusho na kuwaombea wafu.

Vivyo hivyo haifai akayatembelea makaburi kwa ajili ya kuomba karibu nayo, akaomba du´aa na huku ameketi karibu nayo, kutoa swadaqah karibu nayo au kwa ajili ya kufanya kisomo karibu nayo. Mambo haya hayakuwekwa katika Shari´ah. Bali ni miongoni mwa Bid´ah. Lakini ayatembelee kwa ajili ya kuwatolea salamu, kuwaombea du´aa na kuwatakia rehema. Kwa ajili hii: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiwafunza Maswahabah zake pindi wanapoyatembelea makaburi basi waseme:

السلام عليكم أهل الديار من المؤمنين والمسلمين وإنا إن شاء الله بكم لاحقون نسأل الله لنا ولكم العافية يرحم الله المستقدمين منا والمستأخرين

“Amani ya Allaah iwe juu yenu wakazi waumini na waislamu. Nasi – Allaah akitaka – tutaungana na nyinyi. Tunamuomba Allaah juu yetu sisi na nyinyi afya. Allaah amrehemu aliyetangulia katika sisi na atakayekuja baadaye.”[9]

Hivi ndivo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alivokuwa akiwafunza. Vilevile alikuwa yeye anapoyatembelea makaburi basi husema:

السلام عليكم دار قوم مؤمنين وإنا إن شاء الله بكم لاحقون اللهم اغفر لأهل بقيع الغرقد

“Amani ya Allaah iwe juu yenu wakazi waumini na waislamu. Nasi – Allaah akitaka – tutaungana na nyinyi. Ee Allaah! Wasamehe watu wa al-Baqiy´ al-Gharqad.”[10]

Mfano wa maneno kama haya ndio yamekuja katika Hadiyth ya ´Aaishah.

Kinacholengwa ni kwamba kuyatembelea makaburi ni kuwafanyia wema wale waliokufa na kuwaombea msamaha na rehema. Kama ambavo vilevile unaifanyia wema nafsi yako mwenyewe kwa sababu unajikumbusha kwa jambo hili Aakhirah na kukumbuka kifo ili ujiandae kukutana na Allaah (´Azza wa Jall). Lakini kama tulivotangulia kusema matembezi haya yafanyike pasi na kufunga safari.  Bali mtu ayatembelee makaburi ya wale watu wake wa mji anapoeshi. Kufunga safari kuwe kwa sababu nyingine kama vile kutembelea msikiti wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) Madiynah, kuswali ndani yake, kusoma ndani yake na mfano wa hayo. Atapoutembelea msikiti ndipo atatumia fursa ya kutembelea kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), atamtolea salamu yeye na marafiki zake wawili. Aidha itapendekeza kwake kutembelea al-Baqiy´ na makaburi ya mashahidi. Vilevile atayatembelea makaburi ya Qubaa´ na kuswali ndani yake. Yote haya ni mambo yaliyowekwa katika Shari´ah. Vivyo hivyo akizitembelea nchi zengine kwa ajili ya biashara, kumuona rafiki au ndugu itapendekeza kwake kuyatembelea makaburi ya mji huo ili aweze kuwaombea du´aa watu wake, kuwatakia rehema, kujikumbusha kupitia wao Aakhirah, kujiandaa kwayo na kukumbuka kifo. Namna hii ndivo walivobainisha wanazuoni na zikafahamisha Hadiyth Swahiyh kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kwa kumalizia wanawake kuyatembelea makaburi ni jambo limekatazwa kwa hali yoyote. Haya ndio maoni ya sawa kutokana na usahihi wa Hadiyth zilizowakataza na kutojulisha juu ya kubagua.

[1] Ahmad (2844), at-Tirmidhiy (1056) na Ibn Maajah (1574).

[2] al-Bukhaariy (5096) na Muslim (2741).

[3] al-Bukhaariy (1864) na Muslim (1397).

[4] Muslim (976).

[5] 72:18

[6] 35:13-14

[7] 23:117

[8] 27:65

[9] Muslim (974).

[10] Muslim (974).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 17-25
  • Imechapishwa: 07/04/2022