Imethibiti kutoka kwa Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Salaf-us-Swaalih wakitahadharisha juu ya Bid´ah. Si kwa jengine isipokuwa ni kwa sababu ni nyongeza katika dini na Shari´ah ambayo Allaah hakuiidhinisha. Huko ni kujifananisha na maadui wa Allaah miongoni mwa mayahudi na manaswara ambao wameongeza katika dini zao na kufuata yale ambayo Allaah hakuyapa idhini. Hilo linalazimisha kuutukana Uislamu na kuutuhumu kutokamilika. Ni jambo lenye kujulikana kuwa kufanya hivi ni ufisadi mkubwa na maovu yenye kutia aibu. Isitoshe ni kupingana na maneno ya Allaah (´Azza wa Jall):

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ

“Leo Nimekukamilishieni dini yenu.”[1]

Vilevile ni kwenda kinyume waziwazi na Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambazo zinatahadharisha Bid´ah na kuwakimbiza watu kwazo.

Tunataraji zile dalili tulizotaja ndani yake mna kutosheleza na ukinaishaji kwa yule mwenye kutaka haki juu ya kutahadharisha Bid´ah hizi na kusherehekea usiku wa Israa´ na Mi´raaj na kutahadharisha nayo na kwamba ni kitu kisichokuwa na uhusiano wowote kabisa na Uislamu.

Pale ambapo Allaah aliwajibisha kutoa nasaha kwa waislamu, kuwabainishia yale aliyoyawekea Shari´ah katika dini na akaharamisha kuficha elimu ndipo nikaonelea kuwazindua ndugu zangu juu ya Bid´ah hii ambayo imeenea katika miji mingi mpaka ikafia kiasi cha kwamba baadhi ya watu wakafikiria kuwa ni katika dini. Allaah ndiye mwenye jukumu la kuzitengeneza hali za waislamu wote na kuwatunuku uelewa katika dini na kutuwafikisha sisi na wao kushikamana na haki na kuwa na uthabati juu yake na wakati huo huo kuachana na yale yenye kwenda kinyume nayo. Hakika Yeye ndiye mwenye kusimamia na muweza wa hilo.

Swalah na amani zimwendee mja na Mtume Wake Muhammad, kizazi chake na Maswahabah zake.

[1] 05:03

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr minal-Bid´ah, uk. 19-20
  • Imechapishwa: 23/01/2022