04. Sababu ya kwanza: kuyapamba maisha kwa kumuabudu Allaah pekee

Miongoni mwa sababu ya familia kupata furaha – na ndio sababu kubwa na ndio msingi, kilele na roho ya furaha zote na pia ndio siri ya maisha, siri ya raha na ndio siri ya utulivu ambayo atayeipata basi amepata kheri kubwa mno – ni kumuabudu Allaah. Kila mmoja katika familia akimbilie kuihakikisha imani na matendo mema. Hakika hayo ndio msingi wa maisha mazuri. Allaah (´Azza wa Jall) anasema:

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ

“Mwenye kutenda mema miongoni mwa wanamume au wanawake ilihali ni muumini… ” 16:97

Sharti hii imeshurutisha nani? Mola wa walimwengu. Sharti hii ni ipi?

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا

“Mwenye kutenda mema.”

Ni kipi kitendo chema? Ni kile ambacho mwenye nacho ameruka nacho kwa mbawa mbili; ubawa wa kumtakasia nia Allaah. Kwa msemo mwingine akawa ni mwenye Ikhlaasw kwa Allaah. Na ubawa wa kumfuata Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa msemo mwingine kitendo kiwe kimewekwa katika Qur-aan na Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hili ndio tendo jema:

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ

“Mwenye kutenda mema miongoni mwa wanamume au wanawake ilihali ni muumini… ” 16:97

Amehakikisha imani. Matendo mema pia ni katika imani. Ni lipi jibu la sharti na malipo yake?

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَلَنُحْيِيَنَّهُ حَيَاةً طَيِّبَةً ۖ وَلَنَجْزِيَنَّهُمْ أَجْرَهُم بِأَحْسَنِ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ

“Mwenye kutenda mema miongoni mwa wanamume au wanawake ilihali ni muumini, Tutamhuisha maisha mazuri na tutawalipa ujira wao kwa mazuri zaidi ya yale waliyokuwa wakiyatenda.” 16:97

Ni nani awezae kuyafanya mabaya maisha ya yule ambaye Allaah amemuhuishia maisha mazuri? Ikiwa Allaah ambaye mikononi Mwake ndio mna uendeshaji wa mambo yote ameyafanya maisha yake kuwa mazuri, ni nani ambaye anaweza kuyafanya maisha yake yakawa mabaya? Iwapo watakusanyika majini na watu wote kutaka kuyafanya mabaya maisha yake hawatoweza kutikisa kitu katika raha ya maisha yake. Kwa kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ndiye ambaye kayafanya maisha yake kuwa mazuri na atamlipa mazuri duniani na Aakhirah. Atampa mazuri kwa yale aliyotenda duniani kwa njia ya kuyafanya maisha yake kuwa mazuri. Kadhalika atamlipa Aakhirah kwa kuyafanya maisha yake kuwa mazuri na hatimae awe miongoni mwa watu wa Peponi. Hii ni ahadi ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala).

Ambaye Allaah atamhuishia maisha mazuri basi Allaah atamruzuku kukinai na anakuwa ni mwenye kukinai kutokana na ile kheri anayopata na Allaah (´Azza wa Jall) anamruzuku utulivu wa moyo na hatimaye moyo wake unaishi kwenye furaha, inatapakaa nyumbani kwake na wanapata furaha waliyoko pambizoni mwake. Akipata nyumbani kwake na kwa wale waliyoko pambizoni mwake kuwa ni wenye furaha anashukuru na anawalipa waliyoko pambizoni mwake kwa kheri. Akipata katika familia yake na kwa wale waliyoko pambizoni mwake kuwa ni wenye madhara anasubiri na anajaribu kumsamehe katika familia yake yule aliyemfanyia vibaya. Hakuna awezae hayo isipokuwa muumini tu. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anasema:

“Ajabu iliyoje juu ya jambo la muumini… “

Ndugu zangu! Zingatieni!

Ni nani anayeshangazwa? Ni Muhammad bin ´Abdillaah ambaye ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

“Ajabu iliyoje juu ya jambo la muumini… “

Kwa nini?

“… hakika mambo yake yote kwake ni kheri. Anapopatwa na la kumfurahisha, anashukuru na inakuwa ni kheri kwake. Anapopatwa na dhara anasubiri na inakuwa ni kheri kwake. Hayo hayawi isipokuwa kwa muumini tu.” Muslim (2999).

Mwenye kuhakikisha imani basi furaha humhakikikia katika jambo hili kubwa. Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) anasema:

“Ndani ya moyo kuna kufarikiana kusikoondoka isipokuwa kwa kumwelekea Allaah. Vilevile kuna mahuzuniko yasiyoondoka isipokuwa kwa kuanasika na Allaah. Kuna huzuni usiotoweka isipokuwa kwa furaha ya kumbuka Allaah na kuwa na matamanio ya kweli. Kuna wasiwasi usioishi isipokuwa kwa kukusanyika juu yake na kuukimbilia. Kuna moto wa khasara usiozimika isipokuwa kwa kuridhia maamrisho na makatazo na mipango Yake na kustahamili juu ya hayo mpaka wakati wa kukutana Naye. Kuna ufukara usioondoka isipokuwa kwa kumpenda, kurejea Kwake, kudumu kumdhukuru na kumtakasia nia kikweli. Lau angelipewa dunia na vilivyomo ndani yake basi kamwe visingeliondosha ufukara huo.” Madaarij-us-Saalikiyn (03/156).

Lau angelipewa dunia nzima kwa ujumla wake pasi na kumwelekea Allaah usingeliondosha ufukara huo kamwe. Kinachoondosha yale yanayoutia moyo dhiki mbalimbali ni kumwelekea Allaah kwa kutenda matendo mema.

  • Mhusika: Shaykh Sulaymaan bin Saliymillaah ar-Ruhayliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Asbaab sa´aadat-il-Usrah, uk. 16-17
  • Imechapishwa: 08/10/2016