Swali 04: Naishi katika nyumba ilio mbali na msikiti na hulazimika kutumia gari kwenda kuswali. Mara nyingi nikitembea kwa miguu basi swalah inanipita pamoja na kuzingatia kwamba nasikia adhaana kupitia spika. Je, nina dhambi nikiswali nyumbani au tukiswali na majirani watatu au wanne katika nyumba ya mmoja wetu[1]?

Jibu: Ni lazima kwako kuswali pamoja na ndugu zako waislamu msikitini ikiwa unasikia adhaana maeneo ulipo kwa sauti ya kawaida isiyokuwa na kipaza sauti wakati sauti ziko kimya na hakuna kinachozuia kusikia. Ukiwa mbali kwa kiasi cha kwamba husikii adhaana pasi na spika basi itafaa kwako kuswali nyumbani kwako au pamoja na baadhi ya majirani zako. Imethibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba alisema kumwambia kipofu wakati alipomwomba idhini ya kuswali nyumbani kwake: “Je, wasikia wito wa swalah?” Akasema: “Ndio.” Akasema: “Basi imewajibika.”[2]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

“Mwenye kusikia adhaana na asiitikie basi hana swalah isipokuwa akiwa na udhuru.”[3]

Ameipokea Ibn Maajah, ad-Daaraqutwniy na al-Haakim kwa cheni ya wapokezi Swahiyh.

Pindi utapomwitika mwadhini, japo uko mbali, ukapata shida kwa miguu yako au kwa gari yako, basi ni kheri na bora kwako. Allaah anakuandikia athari ya kwenda kwako msikitini na kurejea kutoka huko midhali utamtakasia nia Allaah. Imethibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba alisema kumwambia bwana mmoja ambaye alikuwa mbali na msikiti wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na alikuwa hapitwi na swalah pamoja na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Akaambiwa ni kwa nini asinunue kipando cha mnyama wakati wa joto kali na usiku wa giza ambapo (Radhiya Allaahu ´anh) akasema:

“Sipendelei nyumba yangu iwe karibu na msikiti. Mimi napenda kuandikiwa kutembea kwangu kwenda msikitini na kurejea kwangu kwa familia yangu.” Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamwambia:

“Hakika Allaah amekukusanyia yote hayo.”[4]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (12/36-38).

[2] Muslim (653) na an-Nasaa´iy (850).

[3] Ibn Maajah (785).

[4] Muslim (1065).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam Swalaat-il-Jumu´ah wal-Jamaa´ah, uk. 27-28
  • Imechapishwa: 23/11/2021