04. Kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah ni shirki kubwa

Kuna watu wanaochinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah kwa ajili ya kujikurubisha kwa viumbe, kwa wafu, makaburi – wanachinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah. Wanamshirikisha Allaah shirki kubwa. Kwa sababu kujikurubisha kwa kuchinja inakuwa kwa ajili ya Allaah (´Azza wa Jalla) pekee. Haifai kwa mtu akajikurubisha kwa kitendo hicho kwa mwengine yeyote asiyekuwa Allaah. Amesema (Ta´ala):

قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ لَا شَرِيكَ لَهُ ۖ وَبِذَٰلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ

“Sema: “Hakika swalah yang na kichinjwa changu na uhai wangu na kufa kwangu ni kwa ajili ya Allaah pekee, Mola wa walimwengu hali ya kuwa hana mshirika – na kwa hayo ndio nimeamrishwa nami ni muislamu wa kwanza.” (06:162-163)

Vilevile amesema (Ta´ala):

فَصَلِّ لِرَبِّكَ وَانْحَرْ

“Basi swali kwa ajili ya Mola wako na [pia ukichinja] na chinja [kwa ajili Yake].” (108:02)

Amefanya kuchinja ni mwenza wa swalah. Kama ambavyo haifai kwa mtu akaswali kwa ajili ya asiyekuwa Allaah hali kadhalika haifai kwake kuchinnja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah.

Baadhi ya watu wanachinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah. Wanawachinjia wafu kwa ajili wawanufaishe na wawaondoshee madhara, wawaponye maradhi walionayo au maradhi yaliyo na watoto wao. Anawachinjia kwa ajili ya ponyo na kujitibu kama alivyowapambia mashaytwaan wa kiwatu na wakijini. Wanachinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah (´Azza wa Jalla). ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Allaah amemlaani mwenye kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Allaah.”[1]

Shirki kubwa inaporomosha ´Aqiydah kuanzia msingi wake. Nayo ni pindi mtu atapofanya aina yoyote ya ´ibaadah kumfanyia asiyekuwa Allaah (´Azza wa Jall). Mfano wa ´ibaadah hizo ni kama du´aa, kuchinja, kuweka nadhiri na mengineyo. Na ni wingi ulioje wa watu ambao wametumbukia katika mambo haya katika makaburi yaliyoko katika miji mingi ya waislamu! Na huenda mjinga akadanganyika kwa hilo na khaswa pale anapopambiwa na kuambiwa:

“Utapata kadhaa na kadhaa.”

Matokeo yake akachinja na kuweka nadhiri kwa ajili ya asiyekuwa Allaah na akadanganywa na kuambiwa kwamba ni kwa ajili tu ya kufanya Tawassul kwa watu wema. Hii ni shirki. Hata kama wataita kuwa ni ´Tawassul`. Ni shirki. Majina hayabadilisha uhakika wa mambo.

[1] Muslim (1978).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-´Aqiydah al-Islaamiyyah as-Swahiyhah https://www.youtube.com/watch?v=KqoTCYds6Cs&t=13s
  • Imechapishwa: 28/01/2019