Suala la nne: Fadhilah za kufunga Ramadhaan na hekima ya kusuniwa kuifunga

1- Fadhilah zake. Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yule atakayesimama usiku wa makadirio kwa imani na kwa matarajio, basi atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia. Na yule atakayefunga Ramadhaan kwa imani na kwa matarajio, basi atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia.”[1]

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Swalah vipindi vitano, ijumaa hadi ijumaa nyingine na Ramadhaan hadi Ramadhaan nyingine ni vyenye kufuta yaliyo baina yake ikiwa mtu atajiepusha na madhambi makubwa.”[2]

Haya ni sehemu tu ya yale yaliyopokelewa kuhusu fadhilah za kufunga mwezi wa Ramadhaan. Ramadhaan ina fadhilah nyingi.

2- Hekima ya kusuniwa funga. Allaah  ameweka Shari´ah ya kufunga kwa hekima na faida nyingi. Miongoni mwazo:

1- Kuitakasa nafsi, kuitwahirisha na kuisafisha kutokamana na michanganyiko na tabia mbaya. Kwa sababu swawm inazifanya zile njia za mishipa zilizoko kwa mwanadamu kuwa nyembamba.

2- Funga inafanya kuipa nyongo dunia na matamanio yake na kuvutia Aakhirah na neema zake.

3- Funga inamfanya mtu kuwaonea huruma wale masikini na kuhisi machungu yao. Kwani mfungaji na yeye anapata kuonja uchungu wa njaa na kiu.

Funga ina hekima nyingi za hali ya juu na faida nyingi kabisa.

[1] al-Bukhaariy (1901) na Muslim (760).

[2] Muslim (233).

  • Mhusika: Nukhbatin minal-´Ulamaa´
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fiqh-ul-Muyassar, uk. 151
  • Imechapishwa: 14/04/2020