Mwezi huu una fadhila kubwa. Moja wapo ni kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) anawaamrisha Malaika Wake kufungua milango ya Pepo na kusifungwe wowote. Sambamba na hilo anawaamrisha Malaika Wake kufunga milango ya Moto na kusifunguliwi wowote. Kisha anawaamrisha Malaika Wake kuwafunga minyororo mashaytwaan wenye kusumbua. Mikono yao inafungwa mpaka kwenye shingo zao ili wasiweze kufanya lolote. Haina maana kuwa mashaytwaan wote ndio wenye kufungwa, isipokuwa tu wale wenye kusumbua na wale wakubwa. Wale walio na taathira kubwa kwa waislamu ndio wenye kufungwa minyororo.

Nyingine ni kuwa Allaah anayalipa maradufu matendo mema na anafuta madhambi. Katika Ramadhaan kuna watu huachiwa huru kutokana na Moto.

Ee waja wa Allaah! Ni wajibu kutumia fursa mwezi huu. Mwezi huu ni fursa mbayo muislamu anatakiwa kuichunga. Kimbilieni kufunga Ramadhaan na kuswali nyusiku zake. Tumieni fursa hii. Huenda isikujieni tena mara nyingine. Huenda ukafa kabla ya kufikia Ramadhaan nyingine. Mche Allaah, Mola Wako.

Peponi kuna mlango unaoitwa ar-Rayyaan. Ndio mlango wataoingilia wafungaji. Kutasemwa “Wako wapi wafungaji?” ambapo watasimama na waingizwe Peponi kupitia mlango huo. Baada ya hapo utafungwa[1]. Wako wapi wafungaji wataopita kwenye mlango huo unaoitwa ar-Rayyaan? Unaitwa ar-Rayyaan, wastahamilivu wa kiu, kwa sababu walishinda na kiu, wakashinda na njaa na wakajiepusha na matamanio katika Ramadhaan na katika mnasaba wa swawm za Sunnah. Kwa ajili hiyo Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) akawalipa thawabu ya wastahamilivu wa kiu badala ya kiu walichojifaradhishia juu ya nasfi zao kwa ajili ya kumtii Mola Wao na kutarajia malipo kutoka Kwake.

Ee mja wa Allaah! Ni lipi bora kwako kufunga siku hii ambayo inakuwa kati ya masaa kumi mpaka masaa kumi na nne ili uje kufufuliwa siku ya Qiyaamah na kupewa maji na usihisi kiu wala njaa tena? Siku hiyo itakuwa miaka elfu khamsini. Watu watasimama sehemu ambayo itakuwa miaka mia tano au miaka mia tatu. Kumetajwa vilevile maoni mengine. Allaah ndiye anajua uhakika wa mambo ulivyo. Allaah amesema kuwa siku hiyo atamfanya mtoto kuwa na mvi na mbingu kuchanikachanika.

Ukifunga katika dunia hii na ukajiahidi mwenyewe kushinda na kiu, njaa na kujiepusha na matamanio yako kwa ajili ya kumtii Mola Wako (Subhaanahu wa Ta´ala), basi Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) atakulipa siku ya Qiyaamah. Utafufuliwa na kupewa maji ilihali watu wako na kiu. Siku hiyo jua litajongezwa karibu na vichwa vya watu lifike takriban mita 1609. Majasho yao yatawatoka na jasho ya kafiri yatafika mpaka kwenye pua yake. Muumini atapewa kivuli kwa sababu ya matendo yake mema, kama vile swadaqah na kisomo cha Qur-aan, aliyofanya kwa ajili ya Allaah. al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kupitia kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Watu saba Allaah atawaweka kwenye kivuli cha ´Arshi ya Allaah siku ambayo hakutokuwa kivuli isipokuwa kivuli Chake; kiongozi mwadilifu, kijana aliyekulia katika kumtii Allaah, mtu ambaye moyo wake umefungamana na misikiti, watu wawili waliopendana kwa ajili ya Allaah wakakutana kwa ajili ya Allaah na kuachana kwa ajili ya Allaah, mtu aliyeitwa na mwanamke aliye na nafasi na mzuri akasema: “Mimi namwogopa Allaah, Mola wa walimwengu”, mtu aliyetoa swadaqah akaificha mpaka mkono wake wa kushoto usijue kilichotolewa na mkono wake wa kulia na mtu mwenye kumkumbuka Allaah akiwa faragha na akatokwa na machozi.”[2]

Katika dunia hii tunatakiwa kufanya mambo yenye kutukurubisha kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala).

[1] al-Bukhaariy (1896) na Muslim (1152).

[2] al-Bukhaariy (6806) na Muslim (1031).

  • Mhusika: ´Allaamah Ahmad bin Yahyaa an-Najmiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Istiqbaal Shahri Ramadhwaan, uk. 27-31
  • Imechapishwa: 09/06/2017