04. al-Albaaniy na jamii ya kipindi cha kikafiri

Pili ni kwamba malengo ya al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) kwa nukuu hii ni kwamba alikuwa anataka kuraddi mazingira maalum na ´Aqiydah walionayo baadhi ya jamii. Yule ambaye atasoma utangulizi wa al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) wa kitabu “Mukhtaswar-ul-´Uluw” basi ataliona hilo. Hilo litaonekana pale alipowaraddi wale wenye kupinga ujuu wa Allaah (Ta´ala) na akabainisha kwamba watu hao wamegawanyika mafungu mawili: fungu la kwanza wanasema kwamba Allaah yuko kila mahali na kundi lingine wanasema kuwa Hayuko juu, chini, kuliani, kushotoni, kwa mbele, kwa nyuma, ndani ya ulimwengu wala nje ya ulimwengu. Vilevile akasema:

“Wengine wamezidisha kwa kusema kwamba hakufungamana na walimwengu na wala hakutengana na walimwengu.”

Kisha akasema tena:

“Jambo linalosikitisha sana ni kwamba hiyo fikira ya kwanza ndio walionayo watu wote katika nchi hii[1]. Unakaribia kutokaa katika kikao chochote kinachomzungumzia Allaah isipokuwa utamsikia mtu anasema kwamba Allaah yuko kila mahali. Wengine wanasema kwamba yuko katika kila kilichokuwepo. Unaporaddi maoni haya basi wanakimbilia kuyabadili na kusema kwamba Yuko kila mahali kwa ujuzi Wake, kama kwamba ni Aayah ya Qur-aan au ya Hadiyth ambayo inatakiwa kufasiriwa.”[2]

Watu wametumbukia katika waliyotumbukia kwa sababu ya tafsiri zao za kimakosa juu ya Qur-aan na Sunnah na kupuuzia ufahamu wa Salaf. Kisha akasema:

“Masikini hawa hawajui kuwa haya ndio maoni na ´Aqiydah walionayo Jahmiyyah na Mu´tazilah. Unapowasikia wakifasiri na kusema kwamba Allaah yuko kila mahali kwa ujuzi Wake, basi unawadhania vyema. Lakini utaona kwa haraka namna dhana yako ilivokosea wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomuuliza yule mjakazi:

“Allaah yuko wapi?” Akajibu: “Juu ya mbingu.” Akamuuliza: “Mimi ni nani?” Akajibu: “Wewe ni Mtume wa Allaah.” Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam): “Mwache huru. Kwani hakika ni muumini.”[3]

Pindi unapowauliza swali kama hili wale ambao si wasomi na wale ambao ni wasomi basi utawaona namna wanavyokutazama hali ya kukupinga. Ima ni wajinga au wanajifanya wajinga juu ya kwamba ni Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndiye ambaye katuwekea msingi wa swali hilo.”

Kisha akaendelea – Allaah amjaze kheri – katika maneno yake marefu:

“Nadhani kwamba sisi wote tunaamini kwamba Allaah ni Mungu mmoja asiyekuwa na mshirika, mikononi Mwake ndiko kuna kheri na ufalme Naye juu ya kila jambo ni muweza.”

al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

“Ni kweli kwamba sisi tunamwamini Allaah, lakini imani za waumini zinatofautiana kiasi kikubwa. Imani ya kuamini ujuu wa Allaah ni dalili ya wazi kabisa juu ya hilo.”

Halafu akaendelea na radd yake ndefu ambapo ndani yake alimnukuu Sayyid Qutwub. Malengo yake ilikuwa kumraddi daktari yule aliyedai kwamba watu hawahitajii kubainishiwa ´Aqiydah, kwa sababu wote wanamwamini Allaah. Badala yake anaonelea kuwa matatizo yao makubwa yanapatikana katika tabia yao ilioharibika. Baada ya hapo akasema:

“Ni mamoja unakubaliana na sisi au hukubaliani na sisi, makundi yote mawili yanawakilisha mamilioni ya waislamu tangu hapo mamia ya miaka nyuma mpaka hii leo. Katika kundi ambalo linaamini swali na jawabu katika ile Hadiyth iliotajwa punde tu ni Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah, mwanafunzi wake mhakiki Ibn-ul-Qayyim-il-Jawziyyah na ndugu zetu wengine wote Hanaabilah wa leo hii ambao ni wafuasi wa Shaykh Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah). Makundi yote mawili yanaingia ndani ya maneno yako uliyosema:

“Nadhani kwamba sisi wote tunaamini kwamba Allaah ni Mungu mmoja asiyekuwa na mshirika, mikononi Mwake ndiko kuna kheri na ufalme Naye juu ya kila jambo ni muweza.”[4]

Ama kuhusu mimi, naamini kwamba hata kama makundi yote mawili watakuwa na zile adabu za Kiislamu basi wataambizana ima moja kwa moja au kinyume chake:

وَإِنَّا أَوْ إِيَّاكُمْ لَعَلَىٰ هُدًى أَوْ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ

“Hakika ima sisi au nyinyi bila shaka tuko juu ya uongofu au katika upotevu  wa wazi.”[5]

Mimi naamini kuwa daktari anatambua kuwa moja katika makundi hayo mawili liko upotevuni – maswala hayahusiani na kuwa na adabu; ni masuala yanayohusiana na fikira na ´Aqiydah. Makundi yote mawili yanawakilisha mamilioni ya waislamu hii leo, katika masuala haya na masuala mengineyo ya I´tiqaad. Je, hivi kweli watu hawa hawahitajii kuisoma ´Aqiydah?”

Haya yanabainisha kwamba jamii za kipindi cha kikafiri anamaanisha maneno yake:

“Jambo linalosikitisha sana ni kwamba hiyo fikira ya kwanza ndio walionayo watu wote katika nchi hii… “

[1] Bila shaka anamaanisha Syria.

[2] Mukhtaswar-ul-´Uluww, uk. 53-54

[3] Muslim (537).

[4] Uk. 09

[5] 34:24

  • Mhusika: ´Allaamah Ahmad bin Yahyaa an-Najmiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Fath ar-Rabbaaniy fiyd-Difaa´ ´an-ish-Shaykh Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy, uk. 23-2
  • Imechapishwa: 26/10/2018