2- Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Ameangamia mja wa dinari! Ameangamia mja wa dirhamu! Ameangamia mja wa Khamiyswah! Ameangamia mja wa Khamiylah! Akipewa huridhia na kama hakupewa hukasirika. Ameangamia na amehiliki mtu huyo! Kama mwiba ukimchoma basi asipate mtu wa kumchomoa! Twuubaa kwa mja ambaye amechukua khitamu za farasi wake kwa ajili ya kupigana Jihaad katika njia ya Allaah; niywele zake ziko timtim na miguu yake imejaa vumbi. Anapowekwa kuchunga [kikosi cha jeshi] basi huchunga kikwelikweli na anapowekwa nyuma kuchunga basi anachunga kikwelikweli. Akiomba idhini asingeliidhinishwa na akiombea basi maombi yake yasingekubaliwa.”[1]

Hadiyth imepokelewa na al-Bukhaariy katika mlango wa jihaad. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Ameangamia mja wa dinari! Ameangamia mja wa dirhamu!”

Bi maana wameangamia. Amesema (Ta´ala):

وَالَّذِينَ كَفَرُوا فَتَعْسًا لَّهُمْ وَأَضَلَّ أَعْمَالَهُمْ

“Wale waliokufuru, basi ni maangamizo kwao na atapoteza matendo yao.”[2]

Maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ameangamia mja wa Khamiyswah! Ameangamia mja wa Khamiylah!”

Khamiyswah ni kitambara kinachovaliwa cha rangi nyeusi na ina michoromichoro miekundu. Khamiylah ni kitambara kilichoshonywa vya watu maarufu na hakina michoromichoro.

Amewaita waja kwa sababu ni wenye kuabudu vitu hivi. Hivyo ndio maana wakawa ni waja wavyo. Yule anayeabudu kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) huyo ni mja wa Allaah. Halafu akazitaja alama zao:

“Akipewa huridhia na kama hakupewa hukasirika.”

Hiyo ni alama ya mtu ambaye anatenda kwa ajili ya dunia. Akipewa huridhia na asipopewa hayuko radhi. Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amesema kuhusu wanafiki:

وَمِنْهُم مَّن يَلْمِزُكَ فِي الصَّدَقَاتِ فَإِنْ أُعْطُوا مِنْهَا رَضُوا وَإِن لَّمْ يُعْطَوْا مِنْهَا إِذَا هُمْ يَسْخَطُونَ

“Miongoni mwao wako wanaokufedhehesha kwa kushutumu katika swadaqah. Wakipewa humo wanaridhika na wasipopewa humo, basi tahamaki wao hukasirika.”[3]

Muumini yeye akipewa anashukuru na asipopewa basi husubiri na wala hakasiriki. Kwa sababu anatenda kwa ajili ya Allaah na wala hatendi kwa ajili ya mambo ya kidunia. Baadhi yao hawako radhi kupewa chochote katika mambo ya kidunia. Walikuwepo Maswahabah ambao hawataki kupewa chochote katika mambo ya kidunia. Wala walikuwa hawatafuti chochote kwa sababu wanataka Pepo. Kwa sababu ya kuchunga matendo yao na kutaraji thawabu huko Aakhirah, hivyo hawataki kuharakisha malipo hapa duniani. Lakini hata hivyo walikuwa wakipokea zawadi pale wanapopewa bila ya kutamani na kuomba. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kile kitachokujia katika hali hii na wewe si mwenye kuipupia basi ipokee. Vinginevyo usiitabishe nafsi yako.”[4]

Muumini ni mwenye furaha, sawa amepewa kutoka katika dunia au hakupewa. Hakupunguzi chochote katika kutenda kwake kwa ajili ya Allaah. Kwa sababu anampenda Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ilikuwa inaweza kutokea anawapa baadhi ya watu kwa ajili ya kuzilaini nyoyo zao na kuchelea juu yao unafiki na kuritadi. Upande wa pili anazuia kuwapa watu ambao ni wapendwa zaidi kwake na kuwaacha wategemee imani zao. Kwa sababu anaamini imani na ´Aqiydah zao. Alikuwa anajua kuwa hawatoathirika asipowapa. Hii ndio alama ya muumini. Ni mwenye kubaki juu ya imani na yakini yake ni mamoja amepewa katika mambo ya kidunia au hakupewa. Ama mtu ambaye tamaa yake ni dunia akipewa ndio anafurahi na asipopewa anakasirika. Yuko tayari kufurahi na kuchukia kwa ajili ya dunia.

Hichi ndicho kinachokusudiwa katika Hadiyth. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amemwita kuwa ni mja wa vitu hivi pamoja na kwamba ni muislamu muumini. Lakini midhali ya kwamba anatenda na huku anatafuta mambo haya ndio akawa ni mja wavyo. Huu ndio uja wa shirki, lakini ni shirki ndogo. Haimtoi mtu nje ya Uislamu, lakini hata hivyo inapunguza Tawhiyd na imani yake.

[1] al-Bukhaariy (2887).

[2] 47:08

[3] 09:58

[4] al-Bukhaariy (7163), Muslim (2406) na Ahmad (100).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: I´aanat-ul-Mustafiyd bi Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 449-450
  • Imechapishwa: 03/09/2019