02. Uwajibu wa kumuabudu Allaah pekee na kujitenga mbali na shirki

Himdi zote anastahiki Allaah, Mola wa walimwengu. Swalah na salaam zimwendee Mtume wetu Muhammad, kizazi chake na Maswahabah wake.

Wa ba´d:

Vitenguzi ni wingi wa kitenguzi. Linatokamana na neno kutengua kitu pale anapokifungua, kukiangamiza na kukiharibu. Amesema (Ta´ala):

وَلَا تَنقُضُوا الْأَيْمَانَ بَعْدَ تَوْكِيدِهَا

“Wala msivunje viapo baada ya kuvithibitisha.” (an-Nahl 16:91)

وَلَا تَكُونُوا كَالَّتِي نَقَضَتْ غَزْلَهَا مِن بَعْدِ قُوَّةٍ أَنكَاثًا

“Wala msiwe kama yule mwanamke aliyezongoa uzi wake vipande vipande baada ya kwishausokota ukawa mgumu.” (an-Nahl 16:92)

Uislamu maana yake ni kujisalimisha kwa Allaah (Jalla wa ´Alaa) kwa kumpwekesha na kumtakasia Yeye ´ibaadah pasi na wengine.

Asiyejisalimisha kwa Allaah ni mwenye kiburi. Mwenye kujisalimisha kwa Allaah na kwa wengine ni mshirikina. Kuhusu yule mwenye kujisalimisha kwa Allaah pekee ndiye mpwekeshaji. Kwa ajili hiyo ndio maana amesema:

“Ni kujisalimisha kwa Allaah kwa kumpwekesha.”

Tawhiyd ni kumpwekesha Allaah (Jalla wa ´Alaa) kwa ´ibaadah. Kwa msemo mwingine ni kule kumfanya mwabudiwa akawa Mmoja. Badala ya waungu kuwa wengi na wenye kufarikiana mtu akafanya yule mwabudiwa ni Mmoja tu, ambaye ndiye Allaah:

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا إِلَـٰهًا وَاحِدًا ۖ لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ ۚ سُبْحَانَهُ عَمَّا يُشْرِكُونَ

”Hawakuamrishwa jengine isipokuwa wamwabudu mungu Mmoja. Hapana mungu wa haki isipokuwa Yeye; Ametakasika kutokana na yale yote wanayomshirkisha nayo.” (Tawbah 09:31)

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاءَ وَيُقِيمُوا الصَّلَاةَ وَيُؤْتُوا الزَّكَاةَ ۚ وَذَٰلِكَ دِينُ الْقَيِّمَةِ

“Hawakuamrishwa jengine isipokuwa wamuabudu Allaah pekee hali ya kumtakasia yeye dini, wenye kupondoka kwenye haki na kuiacha batili, na wasimamishe swalah na watoe  zakaah – na hiyo ndio dini iliyosimama imara.” (al-Bayyinah 98:05)

Huu ndo Uislamu uliyosimama imara.

إِنِ الْحُكْمُ إِلَّا لِلَّـهِ ۚ أَمَرَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ ۚ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ

”Hakuna hukumu isipokuwa ya Allaah. Ameamrisha kwamba msimwabudu isipokuwa Yeye pekee. Hiyo ndio dini iliyonyooka lakini watu wengi hawaelewi.” (Yuusuf 12:40)

Huu ndio Uislamu.

Kunyenyekea Kwake kwa kumtii… – Bi maana pamoja na Tawhiyd na kunyenyekea maamrisho ya Allaah (Jalla wa ´Alaa). Unatakiwa kuyatekeleza na wakati huohuo uyaache na ujiepushe na yale aliyokukataza. Utiifu umejumuisha kufanya yawajibu na kuacha yaliyokatazwa. Haitoshi kuamini upwekekaji pasi na matendo yoyote.

… na kujitenga mbali na shirki… – Haitoshi kwa mtu akawa hamwabudu mwingine isipokuwa Allaah pekee. Bali ni lazima kwake ajitenge mbali na shirki na aitakidi ubatilifu wake na ukafiri wa washirikina na wakati huohuo awachukie na awajengee uadui kwa ajili ya Allaah (´Azza wa Jall). Ni wajibu kwako kuwajengea uadui maadui wa Allaah na upande mwingine uwapende wapenzi wa Allaah. Unatakiwa upende yale anayoyapenda Allaah na yule anayempenda Allaah na wakati huohuo uchukie yale anayoyachukia Allaah na yule anayemchukia Allaah. Hii ndio maana ya maneno yake:

“… na kujitenga mbali na shirki na watu wake.”

Kama jinsi Ibraahiym (´alayhis-Salaam) na wale walio pamoja naye walivyojitenga mbali na washirikina. Amesema (Ta´ala):

قَدْ كَانَتْ لَكُمْ أُسْوَةٌ حَسَنَةٌ فِي إِبْرَاهِيمَ وَالَّذِينَ مَعَهُ إِذْ قَالُوا لِقَوْمِهِمْ إِنَّا بُرَآءُ مِنكُمْ وَمِمَّا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ

”Hakika mna kigezo kizuri kwa Ibraahiym na wale walio pamoja naye walipowaambia watu wao: “Hakika sisi tumejitenga mbali nanyi na yale yote mnayoyaabudu badala ya Allaah… “

Walijiweka mbali nao na waungu wao:

كَفَرْنَا بِكُمْ وَبَدَا بَيْنَنَا وَبَيْنَكُمُ الْعَدَاوَةُ وَالْبَغْضَاءُ أَبَدًا حَتَّىٰ تُؤْمِنُوا بِاللَّـهِ وَحْدَهُ

”Tunakukanusheni na umedhihirika baina yetu na baina yenu uadui na bughudha ya daima mpaka mtapomuamini Allaah pekee.” (al-Mumtahinah 60:04)

لَّا تَجِدُ قَوْمًا يُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ يُوَادُّونَ مَنْ حَادَّ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَلَوْ كَانُوا آبَاءَهُمْ أَوْ أَبْنَاءَهُمْ أَوْ إِخْوَانَهُمْ أَوْ عَشِيرَتَهُمْ

”Hutowapata watu wanaomuamini Allaah na siku ya Mwisho wanawapenda wale wanaopinzana na Allaah na Mtume Wake japo wakiwa ni baba zao, au watoto wao, au ndugu zao au jamaa zao.” (al-Mujaadilah 58:22)

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَتَّخِذُوا آبَاءَكُمْ وَإِخْوَانَكُمْ أَوْلِيَاءَ إِنِ اسْتَحَبُّوا الْكُفْرَ عَلَى الْإِيمَانِ ۚ وَمَن يَتَوَلَّهُم مِّنكُمْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ

”Enyi mlioamini! Msiwafanye baba zenu na ndugu zenu wandani ikiwa wanapendelea ukafiri badala ya imani na yeyote miongoni mwenu atakayewafanya vipenzi na marafiki, basi hao ndio madhalimu.”(at-Tawbah 09:23)

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَتَّخِذُوا عَدُوِّي وَعَدُوَّكُمْ أَوْلِيَاءَ

”Enyi mlioamini! Msiwafanye adui Wangu na adui wenu kuwa marafiki wandani.”(al-Mumtahinah 60:01)

Hii ndio Tawhiyd iliyoamrishwa na Allaah (Jalla wa ´Alaa); kuwapenda watu wake na pia akaamrisha kujitenga mbali na shirki na watu wake kwa kuwa mambo haya yanatengua Uislamu.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 15-17
  • Imechapishwa: 06/02/2017