02. Sharti ili mtu aweze kuswali kisawasawa

Baada ya kumaliza kusoma kitabu kinachozungumzia swalah katika “at-Targhiyb wat-Tarhiyb” cha Haafidhw al-Mundhiriy (Rahimahu Allaah) miaka mine iliyopita na nikawafunza nacho baadhi ya ndugu zetu Salafiyyuun, ndipo tukabainikiwa sote umuhimu na nafasi ya swalah katika Uislamu na ni ujira mkubwa kiasi gani kwa yule mwenye kuitekeleza na kuiswali ipasavyo. Hata hivyo yote hayo yanatagemea na ni kiasi gani inavyoafikiana na swalah ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameashiria hilo pale aliposema:

“Mja huswali swalah ambayo haandikiwi isipokuwa sehemu ya kumi, tisa, nane, saba, sita, tano, nne au nusu yake.”[1]

Kwa ajili hiyo mimi niliwaeleza ndugu kwamba hatuwezi kuiswali ipasavyo isipokuwa ni mpaka tujue ni vipi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliswali kwa upambanuzi na yale mambo ya wajibu, adabu, staili, du´aa na adhkaar zilizomo ndani yake. Baada ya hapo tujibidiishe juu ya kuyatendea kazi kimatendo. Hapo ndipo tutaweza sasa kutaraji kuwa swalah yetu itatuzuia kutokamana na machafu na maovu na kuandikiwa zile thawabu na kheri zilizopokelewa.

Elimu hiyo ya kina ni kitu kisichowezekana kwa watu wengi mpaka kwa wanachuoni wengi, kwa sababu wameshikamana na madhehebu maalum. Kila anayejishughulisha kuitumikia Sunnah kikamilifu anatambua kuwa katika kila madhehebu kuna Sunnah isiyopatikana katika madhehebu mengine na kwamba yote hayo yana maneno na matendo ambayo unasibishwaji wake kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) haukusihi. Mara nyingi hayo yanapatikana katika vitabu vya wale waliokuja nyuma[2]. Ni mara chache tutawaona wakiyathibitisha hayo kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)[3]. Kwa ajili hiyo wanachuoni wa Hadiyth wametunga vitabu kwa ajili ya kuhakikisha vyanzo na usahihi wake. Baadhi ya vitabu hivyo ni ”al-´Inaayah bi Ma´rifati Ahaadiyth-il-Hidaayah” na ”at-Twuruq wal-Wasaa-il fiy Takhriyj Khulaaswat-id-Dalaa-il” vya Shaykh ´Abdul-Qaadir bin Muhammad al-Qurashiy al-Hanafiy, ”Nasb-ur-Raayah li Ahaadiyth-il-Hidaayah” cha Haafidhw az-Zayla-iy, ufupisho wake ”ad-Diraayah” na ”at-Talkhisw al-Habiyr fiy Takhriyj Ahaadiyth ar-Raafi´iy al-Kabiyr” vya Haafidhw Ibn Hajar al-´Asqalaaniy.

Ndipo nikatunga kitabu hiki ili wajifunze namna ya swalah ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ili waige. Natarajia kwa Mola kunipa kile Alichoahidi kupitia Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye amesema:

“Atakayeita katika uongofu basi atapata ujira mfano wa ujira wa atakayemfuata pasi na kupungua chochote katika ujira wao.”[4]

[1] Swahiyh. Ameipokea Ibn-ul-Mubaarak katika ”az-Zuhd” (1-2/21/10), Abu Daawuud na an-Nasaa’iy kwa cheni ya wapokezi nzuri. Nimeitaja katika ”Swahyth Sunan Abiy Daawuud” (796).

[2] Abul-Hasanaat al-Luknawiy amesema baada ya kutaja daraja ya vitabu vya Hanafiyyah na vyenye kutegemewa na vile visivyotegemewa:

“Tumepangilia vitabu vyote kwa mujibu wa vitabu vya Fiqh na sio vya Hadiyth. Ni vitabu vingapi vyenye kutegemewa na wanachuoni mabingwa ilihali vimejaa Hadiyth zilizotungwa! Khaswakhaswa fataawaa. Hata kama wanachuoni hao ni wakamilifu lakini wanachukulia wepesi wale wapokezi.” (an-Naafi´ al-Kabiyr li man yutwaali´ al-Jaami´ al-Kabiyr, uk. 122-123)

Baadhi ya Hadiyth hizo zilizozuliwa na bali za batili zilizopokelewa na baadhi ya vitabu vya watu watukufu ni:

“Yule atakayelipa swalah zake za faradhi zilizompita ijumaa ya mwisho ya Ramadhaan basi itakuwa ni kadhaa ya swalah zote zilizompita mpaka miaka 70.”

al-Luknawiy (Rahimahu Allaah) amesema baada ya kutaja Hadiyth hii:

”´Aliy al-Qaariy amesema katika ”al-Mawdhuu´aat as-Sughraa” na ”al-Mawdhuu´aat al-Kubraa”: “Ni batili kabisa kwa sababu inaenda kinyume na maafikiano ya kwamba kitendo cha ´ibaadah hakiwezi kulipiza matendo yaliyoachwa kwa miaka mingi. Aidha hakuzingatiwi yale mtunzi wa “an-Nihaayah” wala mfafanuzi wa “al-Hidaayah” aliyonakili, kwa sababu wao sio Muhaddithuun na wala hawazipokei Hadiyth zao kwa cheni za wapokezi. ash-Shawkaaniy ameitaja katika ”al-Fawaa-id al-Majmuu´ah fiyl-Ahaadiyth al-Mawdhuu´ah” na akasema:

“Hapana shaka kwamba imezuliwa. Sikuipata kwenye kitabu chochote kilichokusanya Hadityh zilizotungwa. Hata hivyo imetangaa kwa wanachuoni wengi wa leo San´aa´ na wengi wao wameanza kuitendea kazi. Sijui ni nani kawatungia nayo. Allaah akawakebehi waongo.” (Uk. 54)

Kisha al-Luknawiy akasema:

“Ili kuthibitisha kwamba Hadiyth hii imetungwa nimeandika kijitabu kwa jina ”Rad´-ul-Ikhwaan ´an Muhdathaat Aakhir Jum´ati Ramadhwaan”. Nimetaja vilevile faida kubwa. Rejea huko, ni chenye faida katika maudhui haya.”

Hadiyth kama hiyo uwepo wake katika vitabu vya Fiqh ni jambo linaloshusha chini zaidi uaminifu kwa sababu hawazirejeshi Hadiyth katika vyanzo vyake. Maneno ya ´Aliy al-Qaariy yalikuwa yakiashiria hivo. Hivyo ni wajibu kwa muislamu kuzichukua Hadiyth kutoka kwa wataalamu wake.

[3] Imaam an-Nawawiy (Rahimahu Allaah) amesema kwa kufupiza:

“Wanachuoni wakaguzi katika Ahl-ul-Hadiyth na wengineo wanasema kwamba Hadiyth ikiwa ni dhaifu, basi haitakikani kusema kwa kukata kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema hivi, amefanya hivi, ameamrisha hivi, amekataza hivi au vinginevyo kwa njia ya kukata. Badala yake inatakiwa kusema kwamba imepokelewa kutoka kwake, imesimuliwa kutoka kwake na mfano wa hivo. Njia ya kukata inatumika tu kwenye Hadiyth zilizo Swahiyh na nzuri. Zengine zote inatakiwa kutumia njia isiyokuwa ya kukata moja kwa moja. Njia ya kukata inapelekea kwamba Hadiyth ni Swahiyh, jambo ambalo si la sawa kulitumia katika kitu ambacho hakikusihi. Vinginevo mtu anakuwa amemsemea uongo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Adabu hii waandishi wameikosa, wanachuoni wengi katika marafiki zetu na wengineo na bali watu wengi wa elimu. Isipokuwa tu wale Muhaddithuun mabingwa. Huko ni kuchukulia wepesi kubaya. Kwa ajili hiyo mara nyingi walikuwa wakisema wakati wa Hadiyth Swahiyh “imepokelewa kutoka kwake” na wakati wa Hadiyth dhaifu “ameipokea fulani”. Si jambo la sawa.” (al-Majmuu´ (1/60))

[4] Muslim na wengineo. Imetajwa katika ”Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah” (863).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifatu Swalaat-in-Nabiy, uk. 32