02. Maswahabah wametangulia katika kila kheri

Maswahabah wao wametangulia katika kila kheri. Lau kusherehekea usiku huu ingelikuwa ni kitu kimechowekwa katika Shari´ah basi wao wangelikuwa ni wa kwanza kutangulia kukifanya. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndio mtu wa kwanza mwenye kuwatakia watu mema. Amefikisha ujumbe wake vile inavyostahiki na akatekeleza amana. Lau kuadhimisha usiku huu na kuusherehekea ingelikuwa ni sehemu katika dini ya Uislamu basi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) asingeghafilika kwacho na asingeweza kuficha hilo. Ilipokuwa hakukupitika kitu katika hayo, basi ikajulikana kuwa kuusherehekea na kuuadhimisha ni kitu kisichokuwa na uhusiano wowote ule na Uislamu. Allaah ameukamilishia Ummah huu dini na kuutimizia neema na akamkemea yule mwenye kuweka Shari´ah katika dini yale ambayo hakuyaidhinisha. Allaah (Ta´ala) amesema:

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ وَأَتْمَمْتُ عَلَيْكُمْ نِعْمَتِي وَرَضِيتُ لَكُمُ الْإِسْلَامَ دِينًا

“Leo Nimekukamilishieni dini yenu na nimekutimizieni neema Yangu na nimekuridhieni kwenu Uislamu uwe ndio dini yenu.”[1]

أَمْ لَهُمْ شُرَكَاءُ شَرَعُوا لَهُم مِّنَ الدِّينِ مَا لَمْ يَأْذَن بِهِ اللَّـهُ ۚ وَلَوْلَا كَلِمَةُ الْفَصْلِ لَقُضِيَ بَيْنَهُمْ ۗ وَإِنَّ الظَّالِمِينَ لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“Je, wanao washirika waliowaamuru dini yale ambayo Allaah Hakuyatolea kwayo idhini? Na lau si neno la uamuzi [ulokwishapita], bila shaka ingelikidhiwa baina yao; na hakika madhalimu watapata adhabu iumizayo.”[2]

[1] 05:03

[2] 42:21

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr minal-Bid´ah, uk. 17
  • Imechapishwa: 23/01/2022