02. Kanuni juu ya sifa za mke mwema

Tunapozungumzia kuhusu sifa za mke mwema na wema hatutakiwi kupuuza kanuni kubwa ambayo ni kanuni ya msingi ya kufikia wema, nayo ni kwamba wema hauwezi kufikiwa isipokuwa kwa mambo mawili:

Jambo la kwanza ni uwafikishaji wa Allaah (Jalla wa ´Alaa), uongofu Wake, msaada Wake, usahali Wake na mafanikio Yake. Allaah ndiye Mwenye kuwafikisha. Mambo yote yako mikononi Mwake (Jalla wa ´Alaa). Allaah (Ta´ala) amesema:

مَن يَهْدِ اللَّـهُ فَهُوَ الْمُهْتَدِ ۖ وَمَن يُضْلِلْ فَلَن تَجِدَ لَهُ وَلِيًّا مُّرْشِدًا

“Ambaye Allaah amemwongoza, basi yeye ndiye aliyeongoka, lakini yule Anayempotoa, basi hutompatia mlinzi wa kumwongoza.”[1]

وَاللَّـهُ يَدْعُو إِلَىٰ دَارِ السَّلَامِ وَيَهْدِي مَن يَشَاءُ إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ

“Allaah anaita kuelekea nyumba ya amani na Anamwongoza amtakaye katika njia iliyonyooka.”[2]

Uongofu uko mikono Mwake, wema uko mikononi Mwake na uwafikishaji uko mikononi Mwake. Anayotaka huwa. Asiyotaka hayawi.

Jambo la pili ni kwamba mtu mwenyewe ajitahidi kufanya juhudi kufikia wema na kufuata sababu zake zinazopelekea katika hilo.

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekusanya kati ya mambo haya mawili wakati aliposema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth Swahiyh:

“Pupia katika yale yanayokunufaisha na mtake msaada Allaah.”[3]

Maana ya “Pupia katika yale yanayokunufaisha… “ ni kwa kufanya sababu zinazonufaisha na njia zenye faida ambazo hufikiwa kwazo wema na kupitia kwazo hufikiwa uongofu.

Maana ya “… na mtake msaada Allaah” ni kwa kumtegemea, kumuomba msaada Wake na kutaraji kutoka Kwake (Subhaanahu wa Ta´ala) akuwafikishe, kukupa ustawi na uimara na kukusaidia kufikia wema na msimamo. Hii ni kanuni kubwa inayokusanya viumbe wote.

Kanuni nyingine ambayo ni lazima kuizindua, nayo ni kwamba msingi wa wema, maarifa yake na njia ya kuuendea ni Kitabu cha Allaah na Sunnah za Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa ajili hiyo ni wajibu kwa kila ambaye anakumbusha na analingania katika wema na utengenezaji kujengea kila kitu juu ya Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall) na Sunnah za Mtume Wake mtukufu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Allaah (Ta´ala) anasema kuhusu Qur-aan:

إِنَّ هَـٰذَا الْقُرْآنَ يَهْدِي لِلَّتِي هِيَ أَقْوَم

“Hakika hii Qur-aan inaongoza katika yaliyonyooka kabisa.”[4]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema kuhusu Sunnah na uongofu wake:

“Nimewaachia mambo mawili ambayo mkishikamana nayo hamtopotea; Kitabu cha Allaah na Sunnah zangu.”[5]

Kujengea juu ya hayo maudhui yetu ni sifa za mke mwema kwa mujibu wa Kitabu cha Allaah na Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kila sifa itakayotajwa hapa itakuwa ikisapotiwa na dalili yake katika Kitabu cha Allaah au Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kanuni ya tatu na ndio msingi ambao kumejengeka juu yake ´ibaadah zote, fadhila na ukamilifu wote, nayo ni kumcha Allaah. Kumcha Allaah (Ta´ala) ndio msingi wa fadhila, kheri na furaha duniani na Aakhirah. Ni wajibu kwa mwanamke wa Kiislamu kutambua kuwa anamuabudu Allaah na kufikia radhi Zake na ujira na thawabu pindi atakapoishi kwa kushikamana na adabu za Kishari´ah na kuwa na sifa tukufu. Kwa upande mwingine huenda akakosa hilo kutokana na kiasi ambavyo atazembea juu ya sifa hizi. Hili litatajwa kwa kirefu wakati itakapokuja maudhui yake.

[1] 18:17

[2] 10:25

[3] Muslim (2664).

[4] 17:09

[5] al-Haakim (01/172). Ni Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaamiy´´” (2937).

  • Mhusika: Shaykh ´Abdur-Razzaaq bin ´Abdil-Muhsin al-´Abbaad
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifaat-uz-Zawjah as-Swaalihah, uk. 9-12
  • Imechapishwa: 04/06/2017