03. Hadiyth “Mwenye kumwondoshea muumini tatizo katika matatizo ya dunia… “

69- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kumwondoshea[1] muumini tatizo[2] katika matatizo ya dunia, basi Allaah atamwondoshea tatizo katika matatizo ya siku ya Qiyaamah. Mwenye kumsitiri muumini[3], basi Allaah atamsitiri duniani na Aakhirah. Mwenye kumrahisishia mkopaji aliye na uzito[4], basi Allaah atamrahisishia duniani na Aakhirah. Allaah ni mwenye kumsaidia mja midhali mja huyo ni mwenye kumsaidia nduguye. Mwenye kuchukua njia akifuta elimu katika njia hiyo, basi Allaah atamsahilishia njia ya kuelekea Peponi. Hawatokusanyika watu katika nyumba miongoni mwa nyumba za Allaah wakikisoma Kitabu cha Allaah na wakikidurusu kati yao, isipokuwa Malaika huwazunguka, utulivu huwateremkia, rehema huwafunika na Allaah huwataja kwa wale walioko Kwake. Yule mwenye kucheleweshwa na kitendo chake basi hatoharakishwa na nasabu yake[5].”[6]

Ameipokea Muslim, Abu Daawuud, at-Tirmidhiy, an-Nasaa´iy, Ibn Maajah, Ibn Hibbaan katika “as-Swahiyh” na al-Haakim amesema:

“Ni Swahiyh juu ya masharti ya Muslim.”[7]

[1] Kwa mali yake, nafasi yake, ishara yake, msaada wake, uombezi wake au kwa du´aa yake.

[2] Pasi na kujali ni mizongo gani miongoni mwa mizongo ya duniani. Inaweza kuwa mizongo midogo au mizongo mikubwa. Hapa inahusiana na yale mazongo yanayofaa kwa mtazamo wa Shari´ah. Kuhusiana na yale mizongo yaliyoharamishwa au yaliyochukizwa, haijuzu kuyafariji wala kuyaondosha.

[3] Bi maana akamsitiri kwa nguo yake au aibu zake kutokamana na watu. Haya yanafanyika kwa mtu ambaye kafanya kwa bahati mbaya na hatambuliki juu ya ufisadi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Kuwa na usamehevu kwa watu wenye kukosea isipokuwa inapohusiana na adhabu iliowekwa Kishari´h.”

Ni lazima vilevile ifungamanishwe na yale yanayohusiana na haki ya Allaah; kama mfano wa uzinzi, kunywa pombe, kinyume na haki za watu, kama mfano wa kuua na wizi. Katika hali hii kusitiri ni haramu na kumshtaki itakuwa ni wajibu.

[4] Ima kwa kumsubiria au kwa kumfutia kabisa deni lake. Inaweza kuwa na maana vilevile kwamba mtu ni masikini na akamrahisishia jambo lake kwa kumpa zawadi, swadaqah au mkopo.

[5] Yule mwenye kucheleweshwa na matendo yake maovu na akazembea juu ya matendo mema, basi utukufu wa ukoo wake na utukufu wa mababu zake hautomfaa kitu huko Aakhirah. Mambo hayo hayatomharakisha kuingia Peponi. Matendo ya mtendaji ndio yanayomharakisa mtu kuingia, japokuwa atakuwa ni mja wa kihabeshi, kabla ya asiyekuwa mtendaji, hata kama atakuwa ni mwenye kutokamana na kabila tukufu la Quraysh. Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنَّ أَكْرَمَكُمْ عِندَ اللَّـهِ أَتْقَاكُمْ

”Hakika mtukufu zaidi miongoni mwenu mbele ya Allaah ni mwenye kumcha Allaah zaidi kati yenu.” (49:13)

[6] Swahiyh.

[7] Muundo wa Hadiyth umepokelewa na Ibn Maajah tu. Cheni ya wapokezi ni Swahiyh kwa masharti ya al-Bukhaariy na Muslim.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Adhwiym bin ´Abdil-Qawiy al-Mundhiriy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (1/137)
  • Imechapishwa: 13/09/2018
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy