02. Dalili nyingi juu ya kwamba Allaah yuko juu ya viumbe

Tambua – Allaah akurehemu – ya kwamba si katika masharti ya kusihi kwa mapokezi mengi yanayofidisha yakini kwamba yapokelewe na wapokezi wengi. Inatosha kuwe kumepokelewa mapokezi mengi yakiwa na maana moja na kwa njia zinazosadikishana na kusiwe kitu chenye kuyapinga au kuyatia kasoro mpaka yakakita kwenye mioyo ili mapokezi hayo yawe yamepokelewa kwa njia nyingi, yaliyothibiti na ya yakini. Kwani tunaamini ukarimu wa Haatim hata  kama hakukupokelewa juu ya hilo upokezi hata mmoja ukiwa na mlolongo wa wapokezi Swahiyh, kwa sababu kumepatikana yale tuliyotaja. Kadhalika tunaamini uadilifu wa ´Umar, ushujaa wa ´Aliy na elimu ya ´Aaishah na kwamba alikuwa mke wake Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na msichana wa Abu Bakr (Radhiya Allaahu ´anh). Hapana shaka yoyote juu ya haya. Kunakaribia kutokuwepo upokezi uliopokelewa kwa njia nyingi isipokuwa kwa sura kama hii.

Maudhui tutayozungumzia imepokelewa kwa mapokezi mengi na yakini pamoja na kusihi kwa milolongo ya wapokezi na yamenukuliwa na wapokezi waaminifu na watu wema. Hakika kuna mapokezi mengi na vyanzo kiasi cha kwamba si yenye kudhibitika idadi yake na ni jambo lisilowezekana kwa maimamu kuyafupiza katika vitabu. Ummah umeyapokea kwa kuyakubali bila ubishi wala kipingamizi. Khaswa khaswa kwa kuzingatia kwamba mapokezi haya ni yenye kuafikiana na Qur-aan tukufu ambayo haiingiliwi na batili kwa mbele yake wala kwa nyuma yake, ni uteremsho kutoka kwa Yule Mwingi wa hekima na anayestahiki kuhimidiwa. Allaah (Ta´ala) amesema:

ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ

“Kisha akalingana juu ya ´Arshi.” [1]

Tamko hili limetajwa sehemu nyingi katika Qur-aan. Amesema (Ta´ala):

أَأَمِنتُم مَّن فِي السَّمَاءِ

“Je, mnadhani mko katika amani na Aliye juu ya mbingu.” [2]

Tamko hili limetajwa sehemu mbili katika Qur-aan. Vilevile amesema (Ta´ala):

إِلَيْهِ يَصْعَدُ الْكَلِمُ الطَّيِّبُ وَالْعَمَلُ الصَّالِحُ يَرْفَعُهُ

“Kwake linapanda neno zuri na tendo zuri hulitukuza.”[3]

يُدَبِّرُ الْأَمْرَ مِنَ السَّمَاءِ إِلَى الْأَرْضِ ثُمَّ يَعْرُجُ إِلَيْهِ فِي يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ أَلْفَ سَنَةٍ مِّمَّا تَعُدُّونَ

”Anayaendesha mambo kutoka mbinguni mpaka ardhini, kisha inapanda Kwake katika siku ambayo kipimo chake ni sawa na miaka elfu katika yale mnayoihesabu nyinyi.”[4]

تَعْرُجُ الْمَلَائِكَةُ وَالرُّوحُ إِلَيْهِ فِي يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ خَمْسِينَ أَلْفَ سَنَةٍ

”Malaika na Roho wanapanda Kwake katika siku kipimo chake ni sawa na miaka khamsini elfu.”[5]

Alisema kumwambia ´Iysaa:

يَا عِيسَىٰ إِنِّي مُتَوَفِّيكَ وَرَافِعُكَ إِلَيَّ

 “Ee ‘Iysaa! Hakika Mimi nitakusinzisha na Mwenye kukupandisha Kwangu.”[6]

بَل رَّفَعَهُ اللَّـهُ إِلَيْهِ ۚ وَكَانَ اللَّـهُ عَزِيزًا حَكِيمًا

”Bali Allaah alimnyanyua Kwake. Allaah ni Mwenye nguvu kabisa, Mwenye hekima.”[7]

وَهُوَ الْقَاهِرُ فَوْقَ عِبَادِهِ

”Naye ni Mwenye kudhibiti juu ya waja Wake.”[8]

يَخَافُونَ رَبَّهُم مِّن فَوْقِهِمْ وَيَفْعَلُونَ مَا يُؤْمَرُونَ

“Wanamuogopa Mola wao Aliye juu yao na wanafanya yale wanayoamrishwa.”[9]

Alieleza (Subhaanah) ya kwamba Fir´awn alisema:

يَا هَامَانُ ابْنِ لِي صَرْحًا لَّعَلِّي أَبْلُغُ الْأَسْبَابَ أَسْبَابَ السَّمَاوَاتِ فَأَطَّلِعَ إِلَىٰ إِلَـٰهِ مُوسَىٰ وَإِنِّي لَأَظُنُّهُ كَاذِبًا

“Ee Haamaan nijengee mnara ili nifikie njia; njia za mbinguni ili nimchungulie Mungu wa Muusa, kwani hakika mimi namdhania ni mwongo.” [10]

Bi maana Muusa (´alayhis-Salaam) anadanganya pale anaposema kuwa Allaah, Mola wake, yuko juu mbinguni.

Wapinzani juu ya masuala haya wanadai kwa kukata na kwa yakini kwamba Muusa (´alayhis-Salaam) alisema uongo, wanapingana na Mola wa walimwengu, wanamtia kwenye makosa Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye ni mkweli mwaminifu na wanapuuzilia mbali mfumo wa Maswahabah, Taabi´uun, maimamu wa hapo kabla na viumbe wengine wote. Tunamuomba Allaah (Ta´ala) atukinge kutokamana na Bid´ah kwa huruma Yake na atuwafikishe kuifuata njia Yake.

[1] 7:54, 10:3, 13:2, 25:59 na 32:4.

[2] 67:16 na 67:17

[3] 35:10

[4] 32:5

[5] 70:4

[6] 3:55

[7] 4:158

[8] 6:18

[9] 16:50

[10] 40:36-37

  • Mhusika: Imaam Muwaffaq-ud-Diyn bin Qudaamah al-Maqdisiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ithbaatu Swifat-il-´Uluww, uk. 63-65
  • Imechapishwa: 26/02/2018