Imaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu

MAELEZO

Mwandishi (Rahimahu Allaah) ameanza kitabu hichi kwa Basmalah kwa kukiiga Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall). Kitu cha kwanza unachoona pindi unapofungua msahafu kabla ya kila Suurah ni “Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu”. Kuanza kwayo pindi mtu unapoandika barua, vitabu na vijitabu ni kuiga Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall). Vilevile Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akianza kuandika “Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu” mwanzoni mwa barua zake pindi anapowaandikia viongozi na maraisi sehemu mbalimbali ulimwenguni akiwalingania katika Uislamu. Hali kadhalika (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiyafungua maneno yake kwa kuanza kusema “Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu”. Ni dalili inayofahamisha kuwa kuanza kwa Basmalah ni Sunnah ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Sulaymaan (´alayis-Salaam) pia pindi alipomwandikia barua Balqiys ambaye alikuwa ni mfalme wa Sabaa’ aliianza “Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu”:

يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ إِنِّي أُلْقِيَ إِلَيَّ كِتَابٌ كَرِيمٌ إِنَّهُ مِن سُلَيْمَانَ وَإِنَّهُ بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

“Enyi wakuu! Hakika nimeletewa barua tukufu. Hakika hiyo ni kutoka kwa Sulaymaan na imeanza na “Kwa jina la Allaah Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.””[1]

Kwah hivyo inatakiwa kuanza kwa Basmalah katika kila kitu ambacho ni muhimu na chenye thamani kama mfano wa kitabu na barua.

Kujengea juu ya haya wale ambao hawaanzi vitabu na barua zao kwa Basmalah wameacha Sunnah ya kinabii na kuiga Kitabu cha Allaah (´Azza wa Jall). Huenda vitabu na barua zao hizi zikawa hazina baraka na faida. Zisipokuwa na Basmalah basi zinaondoshewa baraka na faida. Kwa sababu wameiacha Basmalah ambayo ni Sunnah na kwa kufanya hivo watakuwa ni wenye kukimbiza mbali na Sunnah au watakuwa wanawafuata kipofu wale ambao wanawakimbiza watu mbali na Sunnah. Hili linatakiwa kutiwa maanani.

Maana ya “Kwa jina la Allaah, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu” ni kutafuta kinga kwa Allaah. Kwa hiyo maana yake inakuwa naomba kinga au naanza kwa jina la Allaah Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu. Lengo ni kutafuta baraka kwalo na msaada kutoka kwa Allaah (´Azza wa Jall). Ni kitu kizuri sana cha kuanza nacho kabla ya kuzungumza, vitabu na barua. Mtu anatakiwa kuanza nalo kwa kuomba ulinzi kwa Allaah na kutafuta baraka kwa jina Lake (Subhaanahu wa Ta´ala).

[1] 27:29-30

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 04-05