Shaykh-ul-Islaam na Imaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Sharti za swalah ni tisa:

1- Mtu kuwa Muislamu.

2- Mtu kuwa na akili.

3- Mtu kuwa na uwezo wa kupambanua.

4- Mtu kutokuwa na hadathi.

5- Mtu kuondosha najisi.

6- Kufunika viungo ambavyo havitakiwi kuonekana (´Awrah).

7- Kuingia kwa wakati.

8- Kuelekea Qiblah.

9- Nia.

Sharti ya kwanza ni Uislamu na kinyume chake ni ukafiri (Kufr). Matendo ya kafiri ni yenye kurudishwa, bila ya kuzingatia sawa akifanya ´amali yoyote ile. Dalili ni Kauli Yake (Ta´ala):

مَا كَانَ لِلْمُشْرِكِينَ أَن يَعْمُرُواْ مَسَاجِدَ الله شَاهِدِينَ عَلَى أَنفُسِهِمْ بِالْكُفْرِ أُوْلَئِكَ حَبِطَتْ أَعْمَالُهُمْ وَفِي النَّارِ هُمْ خَالِدُونَ

“Si haki kwa washirikina kuamirisha misikiti ya Allaah hali kuwa wanajishuhudia nafsi zao kwa ukafiri. Hao yamebatilika matendo yao na katika Moto wao ni wenye kudumu.”[1]

وَقَدِمْنَا إِلَى مَا عَمِلُوا مِنْ عَمَلٍ فَجَعَلْنَاهُ هَبَاء مَّنثُورًا

”Na Tutayaendea yale waliyoyatenda ya matendo yoyote yale na Tutayafanya kuwa ni mavumbi yaliyotawanyika.”[2]

MAELEZO

Mwandishi Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema kuwa swalah ina sharti tisa. Hili ni jambo linalojulikana kwa wanachuoni. Kijitabu hiki wanachuoni walikuwa wakikifunza pamoja na ”Usuwl ath-Thalaathah”. Walikuwa wakiketi misikitini na wakiwafunza watu sharti hizi ili waweze kujifunza misingi ya dini yao na namna za swalah, nguzo zake na mambo yake ya wajibu. Ni jambo ambalo kila muislamu analihitajia.

Sharti ni kitu ambacho ni lazima kiwepo. Kusipokuwepo sharti, basi hakuna pia kile kinachoshurutishwa. Lakini kwa vile sharti imepatikana haina maana kwamba ni lazima vilevile kupatikane kitendo, lakini sharti isipokuwepo, basi kitendo pia hakiwepo. Lakini sharti hailazimishi kuwepo kwake kupatikane kitendo mpaka kitimize sharti, mambo mengine ya wajibu na ya faradhi. Masharti haya ni lazima yatimizwe katika swalah. Pindi masharti yanapotimizwa ndipo swalah inaposihi.

Sharti ya kwanza ni Uislamu. Ni lazima kwa yule mswaliji awe muislamu tokea pale anapoingia ndani ya swalah mpaka pale anapomaliza. Akianza swalah naye ni kafiri basi swalah yake si sahihi. Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

مَا كَانَ لِلْمُشْرِكِينَ أَن يَعْمُرُواْ مَسَاجِدَ الله شَاهِدِينَ عَلَى أَنفُسِهِمْ بِالْكُفْرِ أُوْلَئِكَ حَبِطَتْ أَعْمَالُهُمْ وَفِي النَّارِ هُمْ خَالِدُونَ

“Si haki kwa washirikina kuamirisha misikiti ya Allaah hali kuwa wanajishuhudia nafsi zao kwa ukafiri. Hao yamebatilika matendo yao na katika Moto wao ni wenye kudumu.”[3]

وَلَوْ أَشْرَكُوا لَحَبِطَ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ

”Wangemshirikisha, basi bila shaka yangeliharibika yale yote waliyokuwa wakitenda.”[4]

وَمَن يَكْفُرْ بِالْإِيمَانِ فَقَدْ حَبِطَ عَمَلُهُ وَهُوَ فِي الْآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ

”Na yeyote atakayekanusha imani, basi hakika yameharibika matendo yake naye huko Aakhirah atakuwa miongoni mwa waliokula khasirika.”[5]

وَقَدِمْنَا إِلَى مَا عَمِلُوا مِنْ عَمَلٍ فَجَعَلْنَاهُ هَبَاء مَّنثُورًا

”Na Tutayaendea yale waliyoyatenda ya matendo yoyote yale na Tutayafanya kuwa ni mavumbi yaliyotawanyika.”[6]

Watu wote ambao ni makafiri basi swalah zao si sahihi. Endapo mtu ataswali kabla ya kuingia katika Uislamu basi swalah yake haisihi mpaka pale atapoingia kwanza katika Uislamu.

[1] 09:17

[2] 25:23

[3] 09:17

[4] 06:88

[5] 05:05

[6] 25:23

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ash-Sharh al-Mumtaaz, uk. 62-63
  • Imechapishwa: 24/06/2018