703- Jaabir (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Siku ya ijumaa ina saa kumi na mbili. Hapatikani mja yeyote muislamu anayemuomba Allaah (´Azza wa Jall) kitu isipokuwa humpa nacho. Hivyo basi, itafuteni katika ile saa ya mwisho baada ya swalah ya ´Aswr.”[1]

Ameipokea Abu Daawuud, an-Nasaa’iy na tamko ni lake na al-Haakim ambaye amesema:

“Ni Swahiyh juu ya sharti za Muslim.”

Mambo ni kama alivosema. at-Tirmidhiy amesema:

“Baadhi ya wanachuoni katika Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wengineo wanaona kuwa saa inayotarajiwa ndani yake kunapoitikiwa wito ni baada ya ´Aswr mpaka pale kunapozama jua. Haya ndio maoni ya Ahmad na Ishaaq. Ahmad amesema: “Hadiyth nyingi zinazotaja saa inayotarajiwa kunapoitikiwa wito zinataja kwamba ni baadhi ya ´Aswr.” Amesema: “Inatarajiwa baada ya jua kupondoka.” Kisha akataja Hadiyth ya ´Amr bin ´Awf iliyotangulia[2].”

Haafidhw Abu Bakr al-Mundhir amesema:

“Yapo maoni mbalimbali kuhusu saa ambayo du´aa inakuwa yenye kuitikiwa siku ya ijumaa. Imepokelewa kwetu kwamba Abu Hurayrah amesema:

“Saa hiyo ni pale kunapoingia alfajiri mpaka kunapochomoza jua, baada ya swalah ya ´Aswr mpaka kuzama kwa jua.”[3]

al-Hasan al-Baswriy na Abul-´Aaliyah wamesema:

“Ni pale ambapo jua linapondoka.”

Yapo maoni mengine ya tatu kwamba ni pale ambapo muadhini anaadhini kwa ajili ya swalah ya ijumaa. Hayo yamepokelewa kutoka kwa ´Aaishah.

Imepokelewa kwetu kwamba al-Hasan al-Baswriy amesema:

“Saa hiyo ni pale ambapo imamu anaketi juu ya mimbari mpaka akamaliza.”

Abu Burdah amesema:

“Saa hiyo ni ile ambayo Allaah amechagua kuswaliwe ndani yake.”

Abus-Sawwaar al-´Adawiy amesema:

“Walikuwa wakiona kuwa du´aa ni yenye kuitikiwa kuanzia pale ambapo jua linapondoka mpaka kuanza kwa swalah.”

Yako maoni ya saba yanayosema kwamba ni kuanzia pale ambapo jua linapondoka kwa shibiri moja kwenda mpaka dhiraa moja. Haya yamepokelewa kutoka kwa Abu Dharr.

Kuna maoni mengine ya nane yanayosema kwamba ni baina ya ´Aswr mpaka kuzama kwa jua. Hayo ndio maoni ya Abu Hurayrah, Twaawuus na ´Abdullaah bin Salaam na Allaah ndiye mjuzi zaidi[4].

[1] Swahiyh.

[2] Ilioko katika vigawanyo vya Hadiyth ambazo ni dhaifu.

[3] Haya yamepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah, kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), lakini pia  ni dhaifu. Nimeyataja katika ”ad-Dhwa´iyfah” (5299).

[4] Yapo maoni mengine mengi tu, yamefikia kiasi cha 43, kama alivoyataja Haafidhw katika ”Fath-ul-Baariy”. Yeye mwenyewe ameegemea katika haya maoni yaliyochaguliwa na Imaam Ahamd na Ishaaq. Mimi mwenyewe nimechagua maoni hayo kwa sababu Hadiyth nyingi juu ya maudhui haya zinasema hivo. Yanayosema kinyume na hivo hakuna kitu ndani yake ambacho kimesihi. Ambayo ina nguvu zaidi katika hizo ni Hadiyth ya Abu Muusa ilioko kwa Muslim na wengineo, ambayo iko katika kitabu hichi kwenye vigawanyo vya zile Hadiyth ambazo ni dhaifu. Wameipendelea Hadiyth hiyo kwa sababu iko katika Muslim. Haafidhw amesema:

”Wa mwanzo wamejibu kwa kutumia hoja kwamba Hadiyth zilizoko kwa al-Bukhaariy na Muslim zinapendelewa pale ambapo wanachuoni hawakuzikosoa, jambo ambalo limefanyika juu ya Hadiyth hii ya Abu Muusa. Imetiwa dosari ya kukatika kwa cheni ya wapokezi na mgongano.

Halafu akapambanua jambo hilo. Kwa ajili hiyo ndio maana nikaitaja katika ”Dhwa´iyf Sunan Abiy Daawuud” (193). Yamepokelewa makubaliano ya Maswahabah juu ya kwamba ni ile saa ya mwisho ya ijumaa na hivyo haijuzu kuonelea nyengine. Rejea katika ”Fath-ul-Baariy”.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Adhwiym bin ´Abdil-Qawiy al-Mundhiriy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (1/438-440)
  • Imechapishwa: 07/05/2020
  • taaliki: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy